Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ndoa Inaweza Kustahimili Msukosuko?

Je, Ndoa Inaweza Kustahimili Msukosuko?

Je, Ndoa Inaweza Kustahimili Msukosuko?

“Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—MATHAYO 19:6.

NYUMBA zilizoonekana kuwa imara zilibomolewa kabisa. Hivi karibuni dhoruba kali zilipokumba maeneo makubwa ulimwenguni, ubora na udumifu wa majengo mengi ulijaribiwa.

Leo, ndoa zinaweza kulinganishwa na nyumba ambayo msingi wake unapigwa na dhoruba. Stephanie Coontz, mwanahistoria wa masuala ya ndoa, anasema kwamba “watu na jamii hawaiheshimu tena ndoa.”

Je, unaona madhara yanayoletwa na mtazamo huo? Je, unahisi kwamba jamii haiheshimu tena ndoa? Ikiwa ndivyo, kwa nini? Na mtu anaweza kuwa na tumaini gani la kuwa na ndoa yenye furaha au kuidumisha ikiwa hivyo? Hata hivyo, kwanza kabisa ni nini kinachohatarisha ndoa?

Ndoa Yashambuliwa

Ndoa imekuwa ikishambuliwa tangu mwanzo wa historia ya wanadamu. Sifa na mitazamo iliyokuzwa na wazazi wetu wa kwanza imetokeza msukosuko tunaoona leo katika ndoa. Adamu na Hawa walifanya dhambi walipojiruhusu washindwe na tamaa za kibinafsi na hivyo ‘dhambi ikaingia katika ulimwengu.’ (Waroma 5:12) Rekodi ya historia ya Biblia inasema kwamba punde baada ya hapo, “kila mwelekeo wa fikira za moyo [wa mwanadamu] ulikuwa mbaya tu wakati wote.”—Mwanzo 6:5.

Hali haijabadilika sana tangu wakati huo. Kati ya maelekeo yenye kudhuru ambayo yanakabili ndoa ni kujaribu kujitosheleza bila kujizuia. Huenda mpango wa ndoa ukaonekana kuwa umepitwa na wakati na kwamba haufai katika ulimwengu wa kisasa unaoongozwa na maadili mapya. Na kulegezwa kwa sheria ambazo huzuia kuvunjika kwa ndoa kumeondoa aibu ambayo hapo awali ilihusianishwa na talaka.

Watu wasio na subira ambao hutaka kujitosheleza mara moja, hawafikirii sana au hawafikirii hata kidogo kuhusu madhara ya talaka. Wakidhani kwamba watapata uhuru, wanaamini kuwa talaka italeta furaha.

Watu fulani wanapokabili matatizo magumu katika ndoa, wao hutafuta msaada wa washauri wa ndoa au vitabu vilivyoandikwa na watu hao. Kwa kusikitisha, baadhi ya “wataalamu” wa ndoa wa kisasa wamekuwa wakichochea talaka badala ya kutetea ndoa. Kitabu The Case for Marriage kinasema kwamba “labda kwa mara ya kwanza katika historia ya wanadamu, ndoa, mpango ambao umeheshimiwa kwa muda mrefu, inazidi kushambuliwa kwa mafanikio. Nyakati nyingine ndoa hushambuliwa moja kwa moja na ‘wataalamu’ wanaoamini kwamba ni jambo lenye kukandamiza au lisilopatana na akili kuweka nadhiri ya kuishi pamoja muda wote wa maisha.”

Maoni ya Watu Yamebadilika

Pia maoni ya watu kuhusu ndoa na kusudi la ndoa yamebadilika. Labda umeona kwamba watu hawaoni umuhimu wa wenzi wa ndoa kuwa waaminifu na kutegemezana. Jambo kuu kwao ni kujitosheleza hata ikiwa mara nyingi kufanya hivyo kutamuumiza mwenzi yule mwingine. Jarida Journal of Marriage and Family linasema kwamba badiliko hilo la maoni ya ubinafsi kuhusu ndoa “lilianza katika miaka ya 1960 na kuongezeka haraka katika miaka ya 1970.” Sababu za msingi ambazo ziliwafanya watu wafunge ndoa, kama vile kutamani kupendwa, kuwa na uhusiano wa karibu, uaminifu, watoto, na kutoshelezana, hazionwi kuwa muhimu sana.

Matukio mengine ya hivi karibuni yamechangia sana kubadilika kwa ndoa katika nchi nyingi. Kwanza, katika nchi nyingi, majukumu ya mwanamume ya kutafuta riziki na ya mwanamke ya kutunza nyumba yamebadilika. Kwa kuwa wanawake wameanza kufanya kazi za kuajiriwa, kumekuwa na ongezeko la familia ambazo waume na wake hufanya kazi. Pili, kupata watoto nje ya ndoa ni jambo linalozidi kukubaliwa, hivyo kuongeza idadi ya familia zenye mzazi mmoja. Tatu, watu wengi zaidi wanaishi pamoja bila kufunga ndoa. (Ona sanduku “Si Thabiti Kama Ndoa.”) Nne, ndoa kati ya watu wa jinsia moja na harakati zinazotetea kuhalalishwa kwa ndoa hizo zimeungwa mkono na watu wengi. Je, matukio hayo ya kisasa yameathiri maoni yako kuhusu ndoa?

Ongezeko la Talaka

Na tuchunguze nchi kadhaa ili tuone jinsi ambavyo kuongezeka kwa talaka kumeathiri ndoa sana. Ripoti moja ya hivi karibuni inasema kwamba nchini Marekani, “idadi ya wenzi waliotalikiana iliongezeka mara nne kati ya mwaka wa 1970 na 1996.” Inakadiriwa kwamba ndoa 1 kati ya 5 zimeishia katika talaka. Ni ndoa zipi ambazo huvunjika kwa urahisi? Takwimu zinaonyesha kwamba asilimia 60 hivi ya talaka hutukia katika miaka kumi ya kwanza ya ndoa.

Pia, katika nchi nyingine idadi ya talaka imeongezeka. Mnamo 2004, jumla ya talaka nchini Uingereza na Wales ilifikia 153,490. Nchini Australia, inatazamiwa kwamba karibu asilimia 40 ya ndoa zitaishia kwenye talaka. Katika Jamhuri ya Korea, kulikuwa na ongezeko la talaka 21,800 katika mwaka mmoja tu, kuanzia 2002 hadi 2003. Katika kipindi hicho, jumla ya wenzi wa ndoa 167,100 walitalikiana. Idadi ya talaka nchini Japani, ambako ndoa 1 kati ya 4 huishia katika talaka, sasa inakaribia ile ya Ulaya. “Hapo zamani ndoa mbaya kabisa ndizo ziliishia kwenye talaka,” akasema mtaalamu wa masuala ya familia katika Chuo Kikuu cha Red Cross nchini Japani. “Sasa talaka zimekuwa mtindo wa maisha.”

Katika nchi nyingi dini na desturi za kijamii zilichangia kuimarishwa kwa kifungo cha ndoa. Hata hivyo, haziwezi kuzuia mwelekeo wa jamii wa kukubali talaka. Kwa mfano, fikiria Kanisa Katoliki, ambalo huiona ndoa kuwa takatifu. Mnamo 1983 kanisa hilo lililegeza sheria zake kuhusu ndoa na kufanya iwe rahisi zaidi kwa Wakatoliki kuvunja ndoa. Kwa hiyo, ndoa nyingi zimevunjwa tangu wakati huo.

Ni wazi kwamba, kanuni ambazo hushikilia ndoa zinazorota. Lakini si visababishi vyote vinavyoonekana wazi. Kwa kweli, mbali na kuzorota kwa jamii, kuna kisababishi kingine kikubwa cha kuongezeka kwa kuvunjika kwa ndoa ambacho hakionekani waziwazi na wanadamu wengi.

Kisababishi Kisicho Wazi cha Msukosuko Uliopo

Biblia inatuambia kwamba Shetani Ibilisi, ambaye ndiye chanzo cha ubinafsi, ametokeza uvutano mbaya usioonekana ulimwenguni. Kwa nini? Kwa sababu ametupwa kutoka mbinguni hadi kwenye ujirani wa dunia naye ana hasira kali. Kwa kweli, amekusudia kusababisha “ole,” au taabu nyingi iwezekanavyo, na mpango wa Mungu wa ndoa ni moja tu kati ya shabaha za hasira kali ya Shetani.—Ufunuo 12:9, 12.

Akizungumza kuhusu jinsi ambavyo hali ingekuwa baada ya Shetani kufukuzwa kutoka mbinguni, Yesu alisema hivi: “Kwa sababu ya kuongezeka kwa uasi-sheria upendo wa walio wengi zaidi utapoa.” (Mathayo 24:12) Vivyo hivyo, mtume Paulo aliandika: “Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili [au wa kifamilia], wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:2-4) Sikuzote watu wamedhihirisha tabia hizo mbaya kwa kadiri fulani, lakini zimeongezeka katika nyakati za karibuni kama watu wengi wanavyoweza kukubali.

Kwa kufikiria msukosuko unaokumba ndoa, tunawezaje kujikinga na kuwa na ndoa yenye furaha kwelikweli na yenye kudumu? Swali hilo litajibiwa katika makala inayofuata.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

“Katika jamii ambayo imezoea kutupa vitu, huenda watu wakawa na mtazamo huohuo kuhusu mahusiano.”—SANDRA DAVIS, MTAALAMU WA SHERIA YA FAMILIA

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]

“Si Thabiti Kama Ndoa”

Wenzi wengi wa jinsia tofauti huishi pamoja bila kufunga ndoa. Hata hivyo, maisha hayo “si thabiti kama ndoa,” inasema ripoti moja ya Vituo vya Marekani vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa. Baadhi ya wenzi hao huishi pamoja ili kuona kama watafaana kabla ya kuoana. Lakini je, kuishi pamoja kabla ya kufunga ndoa huwafanya watu wafaane kabisa na kuboresha ndoa zao? Kulingana na jarida Journal of Marriage and Family, uthibitisho unaonyesha kwamba sivyo ilivyo. “Kati ya watu waliooana, wale walioishi pamoja kabla ya ndoa walikosa uradhi katika ndoa . . . , walikuwa na matatizo mengi zaidi ya ndoa, na . . . uwezekano mkubwa wa kuvunjika kwa ndoa,” lasema jarida hilo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

Maisha Marefu na Ndoa

Leo watu huishi muda mrefu zaidi. Ingawa jambo hilo linapendeza, limeongeza mkazo katika ndoa. Zamani ndoa nyingi zilikoma mwenzi wa ndoa alipokufa, lakini leo zinavunjwa kwa talaka. Fikiria hali isiyo ya kawaida ambayo inaathiri wanawake ambao wameolewa kwa muda mrefu nchini Japani. Kulingana na gazeti The Washington Post, wataalamu wanasema hali hiyo inaitwa “tatizo la wanaume waliostaafu.” Akikumbuka wakati mume wake alipostaafu, mwanamke mmoja ambaye ameolewa kwa miaka 40 alisema kwamba wakati huo alifikiri: “Sasa itanibidi kumtaliki. Alipokuwa akirudi nyumbani kutoka kazini nilikuwa nikimfanyia kila jambo, nami sikufurahia hilo. Lakini siwezi kuvumilia kuwa pamoja naye nyumbani wakati wote.”