Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Roho Takatifu Ni Mtu?

Je, Roho Takatifu Ni Mtu?

Maoni ya Biblia

Je, Roho Takatifu Ni Mtu?

ROHO TAKATIFU ya Mungu ni nini? Katika maneno yake ya utangulizi, Biblia inasema kwamba roho takatifu, ambayo pia inaitwa “nguvu za utendaji za Mungu,” ilikuwa ‘ikienda huku na huku juu ya uso wa maji.’ (Mwanzo 1:2) Katika simulizi la ubatizo wa Yesu, Mungu anatajwa kuwa katika “mbingu,” na roho takatifu inaonekana “ikishuka kama njiwa” juu ya Yesu. (Mathayo 3:16, 17) Pia, Yesu aliitaja roho takatifu kuwa “msaidizi.”—Yohana 14:16.

Maandiko hayo pamoja na maandiko mengine katika Biblia yamefanya watu fulani wakate kauli kwamba roho takatifu ni mtu, kama vile Mungu, Yesu, na malaika walivyo watu wenye miili ya roho. Kwa kweli, kwa karne nyingi, baadhi ya dini zenye uvutano mkubwa zinazodai kuwa za Kikristo zimefundisha kwamba roho takatifu ni mtu. Licha ya kwamba fundisho hilo limedumu kwa muda mrefu, bado linawatatanisha washiriki wengi wa makanisa, na huenda hata wengine wakakosa kukubaliana na viongozi wao wa kidini kuhusu fundisho hilo. Kwa mfano, katika uchunguzi mmoja uliofanywa hivi majuzi, asilimia 61 ya wale waliohojiwa wanaamini kwamba roho ya Mungu ni “ishara ya kuwepo kwa Mungu au nguvu zake lakini hiyo si mtu.” Hata hivyo, Biblia inasema nini?

Biblia Inasema Nini?

Mtu anayesoma Biblia kwa unyoofu hana budi kukata kauli kwamba roho takatifu si mtu kama vile makanisa yanavyofundisha. Fikiria masimulizi yafuatayo ya Biblia.

1. Maria, mama ya Yesu, alipomtembelea Elisabeti, binamu yake, Biblia inasema kwamba mtoto aliyekuwa katika tumbo la uzazi la Elisabeti aliruka, “na Elisabeti akajazwa roho takatifu.” (Luka 1:41) Je, ni jambo linalopatana na akili kuwazia kwamba mtu anaweza ‘kujazwa’ mtu mwingine?

2. Alipokuwa akiwaambia wanafunzi wake kwamba Yesu ndiye angechukua nafasi yake, Yohana Mbatizaji alisema hivi: “Mimi ninawabatiza ninyi kwa maji . . . , lakini yule anayekuja nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, ambaye viatu vyake mimi sistahili kuvivua. Huyo atawabatiza ninyi kwa roho takatifu.” (Mathayo 3:11) Kwa kweli Yohana hakuwa akimrejelea mtu aliposema kuhusu kuwabatiza watu kwa roho takatifu.

3. Alipokuwa akimtembelea ofisa-jeshi mmoja wa Roma na familia yake, mtume Petro alisema kwamba Mungu alikuwa amemtia mafuta Yesu “kwa roho takatifu na nguvu.” (Matendo 10:38) Muda mfupi baadaye, ‘roho takatifu iliangukia’ familia ya ofisa-jeshi huyo. Simulizi hilo linasema kwamba wengi walishangaa “kwa sababu zawadi ya bure ya roho takatifu ilikuwa ikimiminwa pia juu ya watu wa mataifa.” (Matendo 10:44, 45) Katika simulizi hilo pia maneno yanayotumiwa hayapatani na wazo la kwamba roho takatifu ni mtu.

Ni jambo la kawaida kwa Biblia kutaja vitu fulani kana kwamba ni watu. Vitu hivyo vinatia ndani hekima, utambuzi, dhambi, kifo, na fadhili zisizostahiliwa. (Methali 8:1–9:6; Waroma 5:14, 17, 21; 6:12) Yesu mwenyewe alisema kwamba “hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa watoto wake wote,” au kwa matokeo yake mazuri. (Luka 7:35) Ni wazi kwamba hekima si mwanadamu ambaye ana watoto halisi! Vivyo hivyo, roho takatifu si mtu kwa sababu tu nyakati nyingine inatajwa kana kwamba ni mtu.

Roho Takatifu Ni Nini?

Katika Biblia, roho takatifu ya Mungu inafafanuliwa kuwa wonyesho wa nguvu za Mungu. Hivyo, tafsiri sahihi ya maandiko ya Kiebrania inarejelea roho takatifu kuwa “nguvu za utendaji za Mungu.” (Mwanzo 1:2) Wazo hilo linaungwa mkono na Maandiko.—Mika 3:8; Luka 1:35; Matendo 10:38.

Tofauti na imani ya watu wengi, Mungu hayuko kila mahali kila wakati. Badala yake, yeye huishi katika makao ya roho, ‘makao yaliyofanywa imara.’ (1 Wafalme 8:39; 2 Mambo ya Nyakati 6:39) Maandiko pia yanataja kwamba Mungu huishi mahali hususa palipo na ‘kiti chake cha ufalme.’ (1 Wafalme 22:19; Isaya 6:1; Danieli 7:9; Ufunuo 4:1-3) Hata hivyo, kutoka ‘makao yake yaliyofanywa imara,’ anaweza kutumia nguvu zake za utendaji mahali popote pale katika makao ya roho na ya kidunia.—Zaburi 139:7.

Huko nyuma katika mwaka wa 1879, msomi wa Biblia Charles L. Ives, alitoa mfano unaofaa kuonyesha kwamba Mungu anaweza kutumia nguvu zake akiwa mahali fulani hususa. Aliandika hivi: “Kwa mfano, sisi husema, ‘Fungua dirisha ili jua liingie chumbani.’ Hatumaanishi kwamba jua halisi litakuja, bali tunamaanisha miale inayotoka kwa jua.” Vivyo hivyo, Mungu hahitaji kusafiri hadi mahali ambapo anataka kutumia nguvu zake za utendaji. Yeye hutumia roho takatifu ambayo inaweza kufika mahali popote katika uumbaji wake. Kuelewa roho takatifu ni nguvu za utendaji za Mungu, kunaweza kukuhakikishia kwamba Yehova atatimiza ahadi zake.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Je, Biblia inafundisha kwamba roho takatifu ni mtu?—Matendo 10:44, 45.

▪ Roho takatifu ni nini?—Mwanzo 1:2.

▪ Roho takatifu ya Mungu inaweza kufika mbali kadiri gani?—Zaburi 139:7.