Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwa na Ndoa Yenye Furaha

Jinsi ya Kuwa na Ndoa Yenye Furaha

Jinsi ya Kuwa na Ndoa Yenye Furaha

“Mwanamume . . . atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.”—MWANZO 2:24.

MUUMBA wetu, Yehova Mungu, alianzisha ndoa ikiwa kifungo cha kudumu kati ya mwanamume na mwanamke. Andiko la Mwanzo 2:18, 22-24 linasema hivi: “Yehova Mungu akaendelea kusema: ‘Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.’ Na Yehova Mungu akaufanya ubavu ambao alikuwa ameuchukua kutoka kwa mwanamume kuwa mwanamke na kumleta kwa huyo mwanamume. Ndipo huyo mwanamume akasema: ‘Mwishowe huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu. Huyu ataitwa Mwanamke, kwa sababu huyu alitolewa katika mwanamume.’ Hiyo ndiyo sababu mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.”

Ni kweli kwamba si rahisi kuwa na ndoa yenye furaha na yenye kudumu, lakini inawezekana. Wenzi wengi wa ndoa wameishi pamoja kwa furaha kwa miaka 50, 60, au zaidi. Ni nini kimewasaidia kufanikiwa? Wao hujitahidi kufanikisha ndoa yao sikuzote na bila ubinafsi kwa kujitahidi “kupata kibali” cha mwenzi wao. (1 Wakorintho 7:33, 34) Jambo hilo hutaka jitihada. Ikiwa uko tayari kutumia wakati na kujitahidi, wewe pia unaweza kuwa na ndoa yenye furaha, ambayo itadumu kwa muda mrefu.

Fuata Maagizo kwa Makini

Mjenzi yeyote mwenye kutegemeka hawezi kuanza kujenga kabla ya kuchunguza ramani kwanza. Vivyo hivyo, hatuwezi kufaulu kuwa na ndoa yenye furaha bila kuchunguza kwa makini maagizo ya Mungu ya kufanya hivyo. Maagizo hayo yanapatikana katika Neno la Mungu. “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida . . . kwa kunyoosha mambo,” aliandika mtume Paulo.—2 Timotheo 3:16.

Waume na wake wanaweza kujifunza mengi kuhusu ndoa kwa kufikiria jinsi Yesu alivyoshughulika na wanafunzi wake. Jinsi gani? Katika Biblia, uhusiano kati ya Yesu na wale watakaotawala pamoja naye mbinguni unalinganishwa na uhusiano kati ya mwanamume na mke wake. (2 Wakorintho 11:2) Yesu aliendelea kuwa mshikamanifu kwa wanafunzi wake, hata katika nyakati za taabu. ‘Aliwapenda mpaka mwisho.’ (Yohana 13:1) Akiwa kiongozi mwenye huruma, sikuzote Yesu alifikiria kupungukiwa na udhaifu wa wafuasi wake. Hakudai kamwe wafanye mambo yaliyozidi uwezo wao.—Yohana 16:12.

Hata rafiki zake wa karibu waliposhindwa kufanya yale aliyotarajia, Yesu aliendelea kuwa mpole. Hakuwakemea, lakini badala yake alijaribu kuwarekebisha kwa unyenyekevu na fadhili za kimungu. (Mathayo 11:28-30; Marko 14:34-38; Yohana 13:5-17) Hivyo, ukichunguza kwa makini jinsi Yesu alivyoshughulika kwa wororo na wafuasi wake na jinsi walivyomtendea, utajifunza mambo mazuri unayoweza kufanya ili kuwa na ndoa yenye furaha.—1 Petro 2:21.

Jenga Juu ya Msingi Imara

Bila shaka, majaribu yaliyo kama dhoruba yatashambulia msingi wa ndoa yako. Hilo litaathiri msingi wa uhusiano wako na mwenzi wako. Hata hivyo, msingi imara zaidi wa kuwa na ndoa yenye furaha ni kuwajibika kwa upendo. Yesu alikazia umuhimu wa kuwajibika aliposema: “Basi aliyewaunganisha Mungu, mutu asiwatenganishe.” (Mathayo 19:6, Zaire Swahili Bible) Neno “mutu” linatia ndani mume na mke wake, ambao wameweka nadhiri ya kuwa waaminifu kwa mmoja na mwenzake.

Huenda wengine wakaona kuwajibika kuwa mzigo, na kwamba kunadai wakati, mali, na jitihada nyingi. Leo, watu wengi huchagua kufanya mambo ambayo hayatawalazimu kujidhabihu kwa watu wanaowajibika kwao.

Ni nini kinachoweza kuwasaidia watu wawajibike kwa ndoa? Mtume Paulo aliandika: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” (Waefeso 5:28, 29) Basi, kwa kiasi fulani, ‘kuunganishwa’ kunamaanisha kwamba unafikiria hali ya mwenzako kana kwamba ni yako. Watu waliooana wanapaswa kubadili kufikiri kwao. Neno “changu” linapaswa kuwa “chetu” na “mimi” kuwa “sisi.”

Kukabiliana kwa mafanikio na msukosuko katika ndoa yenu kutawafanya mwe na hekima. Hekima hiyo inaweza kutokeza furaha. Methali 3:13 inasema: “Mwenye furaha ni mtu ambaye amepata hekima.”

Tumia Vifaa Visivyoteketea kwa Moto

Ili nyumba idumu na iwe salama, lazima ijengwe vizuri. Kwa hiyo, azimia kufanya ndoa yako iwe yenye kudumu. Tumia vifaa vyenye kudumu, ambavyo vinaweza kuhimili majaribu makali ya ushikamanifu wako. Thamini sana sifa nzuri kama vile hekima ya kimungu, ukarimu, utambuzi, kumwogopa Mungu, uchangamfu, kuonyesha uthamini wenye upendo kwa ajili ya sheria za Mungu, na imani ya kweli.

Furaha na uradhi katika ndoa haipatikani kupitia vitu vya kimwili au vyeo vya kilimwengu. Inapatikana tu moyoni na akilini, na sifa hizo huimarishwa na kweli kutoka katika Neno la Mungu. Himizo la kwamba “kila mmoja na aendelee kuangalia jinsi anavyojenga” linaweza kutumiwa kuhusu ndoa.—1 Wakorintho 3:10.

Matatizo Yanapotokea

Ili jengo lidumu kwa muda mrefu, lazima kuwe na ratiba nzuri ya kulidumisha. Mume na mke wanaposaidiana kwa ukawaida ili kutimiza miradi yao na wanapoheshimiana, ndoa yao itakuwa thabiti. Hawawi na ubinafsi, na hudhibiti hasira.

Mambo yanayosababisha hasira na kuudhika yasipotatuliwa yanaweza kufanya ndoa isiwe na upendo. Mtume Paulo aliwashauri hivi wanaume: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.” (Wakolosai 3:19) Kanuni hiyohiyo inawahusu wake. Wenzi wa ndoa wanapojitahidi kuwa wenye ufikirio, fadhili, na wenye kuelewa hali, hilo hufanya wapate furaha na uradhi. Kuepuka hasira na uchokozi husaidia kuzuia ugomvi matatizo yanapotokea. Paulo alituhimiza “iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari.”—Waefeso 4:32.

Vipi ukiudhika kwa sababu ya kuhisi kuwa hoi, umechokozeka, au huthaminiwi? Kwa utulivu, mweleze mwenzi wako waziwazi mambo yanayokuhangaisha. Hata hivyo, huenda ikafaa kufunika mambo madogo-madogo kwa upendo.—1 Petro 4:8.

Mume mmoja ambaye ndoa yake ya miaka 35 imepatwa na majaribu mbalimbali, anasema kwamba hata mwenzi wako akukasirishe kadiri gani, hupaswi kamwe “kuacha kuzungumza naye.” Anaendelea kusema hivi kwa hekima, “Msiache kupendana kamwe.”

Unaweza Kuwa na Ndoa Yenye Furaha!

Ni kweli kwamba si rahisi kuwa na ndoa yenye furaha. Hata hivyo, wenzi wa ndoa wanapojitahidi sana kumtia Mungu katika ndoa yao, watakuwa na furaha na usalama. Kwa hiyo, chunguza kwa makini hali ya kiroho ya familia yako; wajibika kabisa katika ndoa yako. Na kumbuka kwamba kama vile Yesu alivyosema, ndoa inapokuwa yenye furaha si mume wala mke anayesifiwa bali ni Mwanzilishi wa ndoa, Yehova Mungu. “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—Mathayo 19:6.

USOMAJI WA ZIADA

Kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, kina madokezo mazuri ya kuwa na ndoa yenye furaha na mafanikio. Mamia ya maelfu ya watu waliooana ulimwenguni pote wameona kwamba shauri lake linalofaa na ambalo linategemea Biblia limewasaidia kuboresha ndoa zao.—Ona ukurasa wa 32 wa gazeti hili.

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Unachoweza Kufanya Ili Ndoa Yako Iwe Yenye Furaha

▪ Jifunzeni Neno la Mungu pamoja kwa ukawaida, na kusali kwa Mungu ili mpate msaada na mwongozo wa kutatua matatizo.—Methali 3:5, 6; Wafilipi 4:6, 7; 2 Timotheo 3:16, 17.

▪ Vutiwa kingono na mwenzi wako tu.—Methali 5:15-21; Waebrania 13:4.

▪ Zungumzeni waziwazi, kwa unyoofu, na kwa upendo kuhusu matatizo yenu na hali ya kutoelewana.—Methali 15:22; 20:5; 25:11.

▪ Zungumza na mwenzi wako kwa fadhili na ufikirio; epuka milipuko ya hasira, chokochoko, na maneno makali ya kuchambua.—Methali 15:1; 20:3; 21:9; 31:26, 28; Waefeso 4:31, 32.

▪ Fuata kwa unyenyekevu shauri la Biblia hata unapohisi kwamba mwenzi wako hafanyi yote anayopaswa.—Waroma 14:12; 1 Petro 3:1, 2.

▪ Jitahidi kusitawisha sifa za kiroho zinazotajwa katika Biblia.—Wagalatia 5:22, 23; Wakolosai 3:12-14; 1 Petro 3:3-6.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Fuata maagizo ya Mungu kuhusu ndoa yanayopatikana katika Biblia

[Picha katika ukurasa wa 7]

Fanya ushikamanifu na upendo usio na ubinafsi uwe msingi imara wa ndoa yako

[Picha katika ukurasa wa 8]

Sitawisha sifa za kiroho zinazoweza kuhimili majaribu makali

[Picha katika ukurasa wa 8]

Dumisha furaha katika ndoa yako