Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Ushirikiano Ni Muhimu kwa Uhai (Septemba 8, 2005) Kusema kweli, nilipoona jalada la gazeti hilo, sikufikiri habari hiyo ingenivutia. Lakini nilisoma makala zote za mfululizo huo nami nilizifurahia sana! Mara nyingi nilipokuwa nikisoma, nilitua na kumshukuru Yehova kwa kuumba viumbe kwa njia ya ajabu. Nilifurahia kuona jinsi ambavyo wanyama hushirikiana.

B. K., Marekani

Vijana Huuliza . . . Ninawezaje Kuepuka Kupendezwa na Watu Wasiofaa? (Agosti 22, 2005) Nilipendezwa na mtu ‘asiyefaa’ ambaye hakuwa na msimamo imara katika kweli ya Biblia. Habari hiyo ilinisaidia kuelewa hatari ya kushirikiana na mtu dhaifu kiroho. Ni vizuri kujua kwamba Yehova anatujali. Asanteni kwa msaada huo wa wakati unaofaa.

A.B.K., Zambia

Makala hiyo ilinisaidia kuona uhitaji wa kubadili mashirika yangu. Ingawa haikuwa rahisi kufanya hivyo, makala hiyo, ambayo mimi huiweka karibu, inaendelea kuniimarisha. Asanteni kwa msaada na kitia-moyo ambacho mnatutolea sisi vijana.

L. R., Marekani

Maoni ya Biblia—Je, Usali kwa Bikira Maria? (Septemba 8, 2005) Ninawaheshimu Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya mwenendo wenu usio na lawama na nimefaidika sana kutokana na magazeti yenu. Lakini, mnawezaje kusema kwamba hatupaswi kumwomba Maria? Yeye hutuombea kwa Baba, ili tuwe na amani.

E. R., Hispania

“Amkeni!” lajibu: Kama makala hiyo ilivyoeleza, hakuna mahali ambapo Biblia inaturuhusu tusali kwa mtu mwingine isipokuwa tu kwa Mungu. Kulingana na kasisi Mkatoliki na mwandishi Andrew Greeley, “sanamu ya Maria inahusianisha Ukristo moja kwa moja na dini za kale za miungu-mama ya kike.” Hivyo, ibada ambayo Maria hupewa imetokana na wapagani bali si Wakristo. Huenda jambo hilo likawa geni kwa wengi wa wasomaji wetu, na tunawatia moyo wachunguze Biblia ili wafahamu inafundisha nini hasa. Wengi wa Mashahidi wa Yehova waliwahi kuwa Wakatoliki, lakini walipojifunza Neno la Mungu, walitambua kwamba Mungu hataki tusali kupitia yeyote ila Yesu Kristo, mpatanishi wetu wa pekee. (Waebrania 7:25) Ili upate habari zaidi, ona kitabu “Biblia Inafundisha Nini Hasa?” * Sura ya 15 yenye kichwa, “Ibada Ambayo Mungu Anakubali,” inazungumzia umuhimu wa kupatanisha imani yetu na Maandiko Matakatifu.

Kukabili Ugonjwa kwa Ucheshi (Aprili 22, 2005) Mke wangu alikufa kutokana na ugonjwa wa ini mnamo Desemba 2002. Aliteseka kwa miezi minane hivi. Hata hivyo, bado alizungumza tu kuhusu mambo mazuri. Alisimulia mambo yaliyotuchekesha. Alikuwa mchangamfu sikuzote hadi alipokufa. Baada ya kusoma makala hiyo, ninaweza kuelewa sababu iliyomfanya awe hivyo. Alihitaji kuwa na mtazamo mzuri kama sisi. Lazima mtazamo huo uwe ulimfanya ahisi vizuri, kama Conchi. Asanteni kwa kunisaidia kuelewa sababu iliyomfanya mke wangu awe na mtazamo huo.

D. H., Marekani

Kutoka kwa Wasomaji Wetu Sikuzote mimi hutazamia kwa hamu kusoma sehemu ya “Kutoka kwa Wasomaji Wetu.” Nyakati nyingine mimi husoma barua kutoka kwa mtu fulani na kujiambia, ‘Hata mimi ninahisi hivyo!’ Nyakati nyingine mimi hujiuliza, ‘Je, nilikosa kuona jambo hilo katika makala hiyo?’ Kisha mimi husoma makala hiyo tena, nami hufurahishwa na kutiwa moyo ninapofanya hivyo.

M. T., Japani

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.