Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Niyatumieje Maisha Yangu?

Niyatumieje Maisha Yangu?

Vijana Huuliza . . .

Niyatumieje Maisha Yangu?

“Mwanzoni, sikuwa na wasiwasi kuhusu wakati ujao. Lakini nilipokuwa karibu kumaliza shule, nilitambua kwamba nilikuwa nikiingia katika ulimwengu wenyewe, unaohusisha kazi na kulipia gharama.”—Alex, 17.

ULIPOKUWA mtoto, je, ulifikiria kile ambacho ungefanya utakapokuwa mkubwa? Unahisije kuhusu mambo hayo sasa? Je, umechanganyikiwa kuhusu jinsi utakavyojitegemeza ukiwa mtu mzima? Ikiwa ndivyo, basi si wewe tu unayekabili mawazo hayo. Kitabu Career Coaching Your Kids kinasema, “kuamua kazi ambayo mtu atafanya maishani ni mojawapo ya mambo magumu zaidi ambayo vijana hukabili.”

Kwa upande mwingine, huenda ikawa kwa sasa hufikiri kuhusu kazi utakayofanya maishani. Huenda ukawa unafikiria zaidi jinsi ya kujifurahisha. Hakuna ubaya wowote kujifurahisha kwani Biblia inakuambia “furahia ujana wako.” (Mhubiri 11:9, Biblia Habari Njema) Hata hivyo, sasa ndio wakati unaofaa zaidi wa kuanza kufikiri kuhusu jinsi utakavyotumia maisha yako. “Mtu mwerevu huzifikiria hatua zake,” linasema andiko la Methali 14:15. Unaweza kufikiriaje hatua zako?

“Fikiria Njia Utakayochukua”

Wazia unapanga kusafiri kilometa nyingi sana mbali na nyumbani. Labda kwanza utachunguza ramani ili kuamua ni barabara gani inayofaa zaidi. Hali hiyo ni sawa na kupangia wakati wako ujao. “Una mambo mengi unayoweza kuchagua kufanya,” anasema Michael, kijana ambaye hufanya kazi katika mojawapo ya ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova. Unaweza kuchaguaje jambo la kufanya? “Inategemea hasa miradi yako,” anasema Michael.

Fikiria mradi wako kuwa mahali unakotaka kwenda. Hutafaulu kufika huko kwa kutanga-tanga. Inafaa zaidi kwanza uchukue ramani na kupanga njia utakayotumia. Kwa njia hiyo, utakuwa ukifuata himizo la Methali 4:26: “Lainisha mapito ya mguu wako.” Biblia Habari Njema inasema hivi katika mstari huo: “Fikiria njia utakayochukua.”

Katika miaka inayokuja, utafanya maamuzi mengi muhimu kuhusu ibada, kazi ya kuajiriwa, ndoa, familia, na mambo mengine muhimu. Itakuwa rahisi kufanya maamuzi yenye hekima ikiwa kwanza utajua unakoelekea. Na unapopanga maisha yako, kuna jambo moja ambalo huwezi kupuuza.

“Mkumbuke Muumba Wako”

Ikiwa kweli unataka kuwa na furaha, lazima uzingatie maneno haya ya Mfalme Sulemani mwenye hekima: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako.” (Mhubiri 12:1, Union Version) Barabara ambazo unachagua kufuata maishani zinapaswa kuongozwa na tamaa ya kumpendeza Mungu.

Kwa nini hilo ni muhimu? Biblia inasema hivi katika Ufunuo 4:11: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” Naam, viumbe vyote mbinguni na duniani vina sababu ya kumshukuru Muumba. Je, wewe unamshukuru kwa kukupa “uhai na pumzi na vitu vyote”? (Matendo 17:25) Je, huchochewi kumpa Yehova Mungu kitu ili kuonyesha unathamini yote ambayo amekupa?

Kwa sababu wanamkumbuka sana Muumba wao, vijana wengi Mashahidi wa Yehova wamechagua kuwa watumishi wa wakati wote. Ukweli ni kwamba, utumishi wa wakati wote ni mradi wenye kuheshimika, nao huleta baraka nyingi sana. (Malaki 3:10) Hata hivyo, utahitaji kupanga mambo kimbele. Kwa mfano, jiulize, ‘Nina ustadi na ujuzi gani mbalimbali ninaoweza kutumia kujitegemeza katika utumishi wa wakati wote?’

Kelly, ambaye sasa ana miaka 27, alianza kufanya mipango mapema maishani. Alikuwa na mradi wa kuwa mtumishi wakati wote. Muda fulani kabla ya kufikia umri wa miaka 20, Kelly alianza kufikiria kazi ya kuajiriwa atakayofanya. Anasema, “Nilihitaji kuchagua kazi ambayo ingeniruhusu kujitegemeza katika utumishi.”

Kelly alisomea kuwa msaidizi wa daktari wa meno kupitia programu ya elimu ya ufundi alipokuwa katika shule ya sekondari. Hata alipata tuzo katika jimbo lao. Lakini mafanikio yake hayakufanya akengeushwe kutoka kwa mradi wake. Kelly anasema, “Nilitaka tu kuwa mtumishi wa wakati wote. Mambo yote mengine yalichukua nafasi ya pili.” Bado Kelly anafurahia utumishi wa wakati wote. Anasema, “Ninahisi kwamba uamuzi niliofanya ndio uamuzi bora zaidi.”

Omba Mwelekezo

Ikiwa ulikuwa unasafiri mahali usipopajua, inaelekea sana kwamba ungehitaji kuomba mwelekezo wakati fulani, hata ikiwa una ramani. Unaweza kufanya hivyohivyo unapopangia wakati wako ujao. Uliza maoni ya wengine. Methali 20:18 inasema hivi: “Kwa shauri mipango yenyewe hufanywa imara.” Bila shaka, wazazi wako ni chanzo kimoja muhimu cha mashauri. Unaweza pia kutafuta mashauri kutoka kwa Wakristo wakomavu ambao wanaonyesha hekima ya kimungu maishani mwao. Roberto anapendekeza hivi: “Watazame watu wazima ambao ni mifano mizuri katika kutaniko lako au katika maeneo jirani. Wanaweza kukueleza mambo fulani ambayo huenda hukuwa umefikiria.”

Zaidi ya mtu mwingine yeyote, Yehova Mungu anataka kukusaidia kuchagua mambo yatakayokufurahisha sana maishani. Kwa hiyo mwombe akusaidie ‘uendelee kufahamu yale yaliyo mapenzi yake,’ kuhusiana na wakati wako ujao. (Waefeso 5:17) Ukimtegemea Yehova kwa moyo wako wote, “atanyoosha mapito yako.”—Methali 3:5, 6.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Una ustadi na ujuzi gani?

▪ Je, unaweza kufikiria njia unazoweza kutumia ustadi wako kumsifu Yehova?

▪ Ni aina gani hususa ya utumishi wa wakati wote iliyotajwa katika makala hii inayokupendeza?

[Sanduku katika ukurasa wa 23]

HALI ISIYOTOKEZA MAFANIKIO

Biblia inasema: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu.” Barabara ya kupata utajiri ina mashimo mengi sana! Mwishowe hata inaweza kumwingiza mtu kwenye madeni, mahangaiko, na kuanguka kiroho.—1 Timotheo 6:9, 10.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24, 25]

UPAINIA

Mhubiri aliye painia ni Mkristo aliyebatizwa mwenye mfano mzuri. Yeye hupanga kutumia angalau saa 70 kila mwezi ili kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Kupitia mazoezi na uzoefu, mapainia huboresha ustadi wao wa kufundisha Biblia.

UTUMISHI WA BETHELI

Washiriki wa familia ya Betheli hutumika katika ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova ambako wao husaidia katika kutayarisha, kutokeza, na kusafirisha vichapo vya Biblia. Kila mgawo Betheli ni pendeleo takatifu la utumishi.

KUTUMIKA MAHALI PENYE UHITAJI MKUBWA

Mapainia fulani wanaweza kuhamia maeneo yenye uhitaji mkubwa wa watangazaji wa Ufalme. Wengine hujifunza lugha nyingine na kutumika katika nchi ya kigeni au na kutaniko linalotumia lugha hiyo.

UTUMISHI WA KIMATAIFA

Watumishi wa kimataifa husafiri kwenda nchi nyingine ili kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme na ofisi za tawi. Huo ni utumishi mtakatifu sawa na kazi ya wale watu waliojenga hekalu la Sulemani.—1 Wafalme 8:13-18.

SHULE YA MAZOEZI YA KIHUDUMA

Masomo hayo ya majuma manane huwazoeza wazee na watumishi wa huduma waseja wanaostahili kuhusu mambo ya usimamizi na kutoa hotuba. Ndugu fulani wanaohitimu hupewa mgawo kutumikia katika nchi yao. Wengine hukubali kutumikia katika nchi za kigeni.

UTUMISHI WA UMISHONARI

Mapainia wanaostahili wenye afya nzuri na nguvu huzoezwa ili watumike katika nchi za kigeni. Wamishonari huishi maisha yenye kusisimua na yenye kuridhisha kwelikweli.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]

WHAT WILL I DO WITH MY LIFE?

DVD hii, iliyotayarishwa na Mashahidi wa Yehova, huonyesha mahojiano ya vijana kutoka Brazili, Marekani, Uingereza, na Ujerumani. Itapatikana hivi karibuni katika lugha nyingine.

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Inategemea hasa miradi yako.”—Michael, mshiriki wa familia ya Betheli

[Picha katika ukurasa wa 24]

“Uamuzi niliofanya ndio uamuzi bora zaidi.”—Kelly, ambaye amekuwa painia kwa miaka sita

[Picha katika ukurasa wa 25]

‘Watazame watu ambao ni mifano mizuri.’—Roberto, mshiriki wa familia ya Betheli