Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sikuwa na Tumaini Lakini Sasa Nina Furaha

Sikuwa na Tumaini Lakini Sasa Nina Furaha

Sikuwa na Tumaini Lakini Sasa Nina Furaha

SIMULIZI LA VICENTE GONZÁLEZ

Majirani waliposikia kwamba nilikuwa nimejipiga risasi mara nne lakini sikufa, walianza kuniita Superman, yaani, mtu mwenye nguvu zisizo za kawaida. Lakini hiyo haikuwa kweli. Acheni niwaeleze sababu iliyofanya nitake kujiua.

NILIZALIWA mnamo 1951 huko Guayaquil, Ekuado. Wazazi wangu walijenga nyumba katika eneo la maskwota karibu na bahari kwa ajili ya watoto wao tisa. Familia maskini zilikuwa “zimevamia” eneo hilo isivyo halali, na kujenga nyumba kwa fito za mianzi na mapaa ya mabati. Kwa kuwa nyumba zilijengwa mahali tambarare karibu tu na bahari na kwenye vinamasi vya mikoko, zilijengwa juu ya nguzo za mbao. Hatukuwa na umeme. Tulipika kwa kutumia makaa, na tulitembea kilometa moja kwenda na kurudi ili kuteka maji ya kunywa.

Ili kugharimia mahitaji ya familia, ndugu na dada zangu wakubwa walianza kufanya kazi wakiwa wadogo. Nilipokuwa na umri wa miaka 16, baada ya kuacha shule, niliajiriwa kama tarishi katika kiwanda fulani. Mimi na rafiki zangu tulianza kunywa vileo na kujiendesha kwa njia isiyo ya adili. Dhamiri yangu ilipoanza kunisumbua, nilienda kuungama dhambi zangu. Kasisi alikuwa akiniambia, “kijana, umeungama dhambi zako vizuri,” kisha angeniambia niende bila kunipa msaada wowote wa kiroho. Kwa hiyo niliendelea kufanya mambo yaleyale. Hatimaye nilianza kuona zoea la kuungama dhambi kuwa upuuzi, na nikaacha kwenda kanisani. Wakati huohuo, nilianza kuona ukosefu wa usawa katika jamii. Watu wengi waliokuwa maskini waling’ang’ana ili kupata riziki, huku matajiri wachache wakiishi maisha ya anasa. Maisha hayakuwa na kusudi. Nilihisi kwamba sina tumaini au kusudi maishani.

Kisha siku moja nikagundua kwamba dada zangu wanne walikuwa wakisoma vichapo vya Mashahidi wa Yehova. Mimi pia nikaanza kuvisoma. Nilivutiwa hasa na kitabu kimoja—Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Kilinifunza habari nyingi za Biblia kwa njia yenye kueleweka. Ninakumbuka nikijiambia hivi: ‘Hii ndiyo kweli!’ Lakini baada ya miaka 15 ndipo niligundua kwamba ni vigumu sana kuishi kupatana na kweli.

Nilianza kufanya kazi kwenye benki nikiwa na umri wa miaka 22. Siku moja mfanyakazi mwenzangu alinionyesha jinsi “alivyokopa” pesa kisiri kutoka kwenye benki na baadaye akalipa “mkopo” huo. Mimi pia nilianza kuchukua “mikopo” mingi sana hivi kwamba singeweza tena kuficha kosa langu. Nilishuka moyo, kwa kuwa nilijua kwamba singeweza kulipa pesa hizo kamwe. Kwa hiyo niliamua kuungama, na kuchukua hatua kali sana ya kujiadhibu, yaani, kujiua.

Baada ya kuandikia benki barua, nilinunua bastola ndogo, nikaenda mahali pasipo na watu ufuoni, na kujipiga risasi mara mbili kichwani na mara mbili kifuani. Ingawa nilijeruhiwa vibaya, sikufa. Mtu fulani aliyekuwa na baiskeli alinipata hapo na kunipeleka hospitali. Baada ya kupona, nilishtakiwa kwa kosa la wizi na kufungwa gerezani. Nilipoachiliwa, nilishuka moyo na kuaibika, kwa kuwa sasa nilikuwa nimehusika katika uhalifu. Kwa kuwa sikufa baada ya kujipiga risasi nne, majirani walianza kuniita Superman.

Fursa ya Kubadilika

Karibu wakati huohuo, nilitembelewa na Paul Sánchez, mmishonari wa Mashahidi wa Yehova. Jambo la kwanza nililotambua ni kwamba alitabasamu. Paul alikuwa mtu mwenye furaha na mwenye kutia moyo sana hivi kwamba nilikubali kujifunza Biblia pamoja naye. Nilijiambia, ‘labda anaweza kunisaidia nipate furaha na kusudi la maisha.’

Kupitia msaada wa Paul, nilijifunza kwamba Mungu ana kusudi kwa wanadamu na kwamba wale wanaompenda na kumtii Yeye siku moja wataishi katika dunia paradiso. (Zaburi 37:29) Pia nilijifunza kwamba si mapenzi ya Mungu kuwe na ukosefu wa haki na umaskini, bali mambo hayo yalitokea mwanadamu alipomwasi Mungu. (Kumbukumbu la Torati 32:4, 5) Kweli hizo zilikuwa kama nuru maishani mwangu. Hata hivyo, ilikuwa vigumu zaidi kubadili utu wangu kuliko kujifunza Biblia.

Nilipata kazi ya ofisini iliyohusisha kushughulika na pesa za kampuni. Kwa mara nyingine tena, nilishindwa na kishawishi na kuanza kuiba. Nilipojua kwamba nitagunduliwa, nilikimbilia jiji lingine la Ekuado kwa mwaka mmoja hivi. Nilijaribu kutoroka nchini, lakini sikufanikiwa, kwa hiyo nilirudi nyumbani.

Paul alinipata tena, na tukaanza kujifunza upya. Wakati huu, niliazimia kutumia kanuni za Biblia maishani na kumtumikia Yehova. Nikiwa na lengo hilo akilini, nilimfunulia Paul mambo niliyokuwa nimefanya, naye akanishauri bila kuficha mambo. Alinionyesha maandiko ya Biblia kama vile Waefeso 4:28, ambalo linasema: “Mwizi asiibe tena, bali afanye kazi ya bidii.” Niliona uhitaji wa kukiri kosa langu la wizi na nikubali matokeo yake.

Nilipokuwa nikifikiria kuhusu hali yangu, nilianza kufanya kazi ya uchoraji. Siku moja, mwanamume fulani alikuja kwenye studio yangu na kusema anavutiwa na picha fulani. Hata hivyo, alikuwa mpelelezi na akanionyesha idhini ya kunikamata. Kwa hiyo nilipelekwa tena mahakamani kisha gerezani. Paul alinitembelea, nami nikamwahidi, “Hutaghairi kwa kujitahidi kunisaidia kuielewa Biblia.” Tuliendelea kujifunza nikiwa gerezani.

Nilithibitisha Kwamba Nilikuwa Mnyoofu

Nilipoachiliwa, niliazimia kumtumikia Yehova kwa moyo wangu wote, na nikathibitisha hilo katika miaka miwili iliyofuata. Mnamo 1988, nilibatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nikiwa na bidii ya kulipia wakati niliopoteza, nilianza utumishi wa wakati wote nikiwa painia, na kufanya jitihada ya pekee kuhubiria magenge ya vijana.

Genge moja lilipenda sana kuandika-andika ukuta wa Jumba letu la Ufalme. Kwa kuwa nilijua washiriki wa genge hilo na mahali walipoishi, niliwatembelea, nikawaeleza kusudi la Jumba la Ufalme, na kuwaomba kwa fadhili waheshimu jumba letu. Baada ya hapo, ukuta wetu haukuandikwa tena.

Baadaye, tulipokuwa tukirekebisha jumba na kuondoa rangi ya zamani, Shahidi mmoja mchanga anayeitwa Fernando aliona neno “Chura” (La Rana, katika Kihispania) ukutani. Alisema, “Hilo lilikuwa jina langu!” Akiwa mshiriki wa genge fulani, Fernando alikuwa ameandika jina lake la utani ukutani. Sasa alikuwa analifuta!

Mara ya kwanza nilipomwona Fernando, alikuwa ametumia dawa za kulevya. Hapo awali, mama yake alikuwa amempeleka kwenye vituo viwili vya kurekebisha tabia, lakini hakubadilika. Kwa hiyo, aliacha kumsaidia, akahama na kumwacha peke yake katika nyumba waliyoishi. Fernando aliuza kila kitu chenye thamani kutia ndani milango, madirisha, na paa la nyumba hiyo ili kupata pesa za kununua dawa za kulevya. Siku moja nilikutana naye barabarani, nikampa kinywaji baridi, na kumwuliza kama tunaweza kujifunza Biblia pamoja naye. Alikubali nami nilifurahi kwamba alipendezwa na kweli. Aliacha kushirikiana na genge hilo, akaacha kutumia dawa za kulevya, akaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na muda si muda akabatizwa.

Nilipokuwa nikihubiri na Fernando nyumba kwa nyumba, mara nyingi watu walitutambua na kutuita “Chura!” au “Superman” na kutuuliza tulilokuwa tukifanya. Walishangaa kuona watu wawili ambao hapo zamani, mmoja alishirikiana na genge na yule mwingine alikuwa mwizi, wakiwatembelea wakiwa na Biblia.

Pindi moja nilikuwa nikimhubiria mtu fulani naye Fernando alikuwa akizungumza na jirani yake. Akimwelekezea Fernando kidole, mtu huyo aliniambia: “Unamwona jamaa yule pale? Pindi moja alinitisha kwa bunduki.” Nilimhakikishia kwamba Fernando ameacha tabia zake za zamani na sasa anaishi kupatana na kanuni za Biblia. Fernando alipomaliza kuzungumza na jirani, nilimwita na kumtambulisha kwa mtu huyo. Mwenye nyumba huyo alisema: “Kijana, ningependa kukupongeza kwa mabadiliko ambayo umefanya maishani mwako.”

Siwezi kukumbuka mara ambazo mimi na Fernando tumeambiwa hivyo. Maelezo hayo yametuwezesha kutoa ushahidi mzuri, na hivyo kupata mafunzo kadhaa ya Biblia. Naam, mimi na Fernando tunafurahia pendeleo la kujulikana kuwa Mashahidi wa Yehova.

Tukio Muhimu Maishani Mwangu

Mnamo 2001, nilipokuwa na umri wa miaka 50, nilishangaa na kusisimuka kualikwa kwenye Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ambayo ingefanywa Peru. Kwa majuma manane, shule hii huwafundisha Mashahidi wanaostahili mambo mazito ya kiroho yatakayowasaidia katika huduma yao.

Nilifurahia kila jambo kuhusu shule hiyo isipokuwa kuzungumza mbele ya watu kwani kufanya hivyo kuliniogopesha. Wanafunzi wengi wenye umri mchanga walitoa hotuba nzuri sana na walionekana kuwa na uhakika. Lakini nilipoamka kwenda jukwaani nikatoe hotuba yangu ya kwanza, nilihisi kuwa sifai. Hisia hizo zimenisumbua tangu nilipokuwa mtoto. Magoti yangu, mikono yangu yenye jasho, na sauti yangu ilitetemeka. Hata hivyo, Yehova alinitegemeza kupitia roho yake takatifu na ndugu wenye upendo. Mmoja wa walimu hata alipendezwa nami kibinafsi na baada ya masomo alinisaidia kutayarisha hotuba zangu. Zaidi ya yote, alinifundisha kumtumaini Yehova. Kabla ya shule hiyo kwisha, kwa mara ya kwanza maishani, nilifurahia kuzungumza mbele ya watu.

Nilikabili mtihani mkubwa wa kusimama mbele ya watu kwenye kusanyiko moja la Mashahidi wa Yehova lililofanywa huko Guayaquil. Nikiwa mbele ya umati wa watu 25,000, nilisimulia jinsi nilivyokuwa Shahidi. Hata hivyo, nilipokuwa nikizungumza, nililemewa na hisia ya kupewa pendeleo la kuwatia moyo watu wengi hivyo, na sauti yangu ikaanza kutetemeka. Baadaye, mmoja wa wahudhuriaji alikuja na kuniambia, “Ndugu González, ulipokuwa ukisimulia kisa chako, kila mtu alikuwa akilengwa-lengwa na machozi.” Kupitia simulizi langu, nilikusudia hasa kuwatia moyo wale ambao labda walikuwa wakipambana kuacha mwenendo wao wa zamani.

Sasa mimi ni mzee wa kutaniko na painia wa kawaida na ninafurahi kwamba nimewasaidia watu 16 kupata ujuzi sahihi wa kweli ya Biblia. Pia ninafurahi kwamba wazazi wangu na dada zangu wanne wamejiweka wakfu kwa Yehova. Mama alikufa akiwa mwaminifu kwa Mungu mnamo 2001. Ninamshukuru Yehova sana kwa kuniruhusu nimjue, na ninajua kwamba njia bora zaidi ya kumshukuru ni kuwasaidia wengine wamkaribie pia.—Yakobo 4:8.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Fernando, Chura, aliyeshirikiana na genge hapo awali ambaye nilimsaidia

[Picha katika ukurasa wa 12]

Paul Sánchez, mmishonari aliyenifunza Biblia

[Picha katika ukurasa wa 13]

Vicente González leo