Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wanadamu Huwa Malaika Wanapokufa?

Je, Wanadamu Huwa Malaika Wanapokufa?

Maoni ya Biblia

Je, Wanadamu Huwa Malaika Wanapokufa?

MSICHANA mdogo aliyeitwa Argyro alikufa akiwa na umri wa miaka saba tu. Wakiwa wamejawa na huzuni, wazazi wake walimtazama akiwa amelala ndani ya jeneza huku amevishwa nguo nyeupe. Akitaka kuwafariji, kasisi aliwaambia hivi: “Mungu alitaka malaika mwingine, kwa hiyo alimchukua Argyro ili awe pamoja naye. Sasa nafsi yake inazunguka-zunguka kiti cha ufalme cha Mweza-Yote.”

Watu wengi wanaamini kwamba malaika ni nafsi za wanadamu waliokufa, hata ingawa ni dini chache sana zinazounga mkono maoni hayo waziwazi. Vyombo vya habari vimeeneza maoni hayo kupitia vipindi vya televisheni na sinema ambazo huonyesha watu waliokufa kisha wakageuka na kuwa malaika baada ya kuwasaidia au kuwalinda wanadamu walio hai.

Je, kweli unaweza kutarajia kwamba wapendwa wako watakuwa malaika watakapokufa? Biblia inafundisha nini kuhusu jambo hilo? Ili kujibu maswali hayo, kwanza na tuone yale ambayo Maandiko Matakatifu yanasema kuhusu malaika na hali halisi ya wafu.

Malaika—Viumbe wa Ajabu

Malaika ni watumishi wa Mungu wasioonekana, walio na nguvu, na ambao huishi katika makao ya roho. Hawategemei wanadamu ili kuendelea kuwa hai. Malaika ni viumbe wa roho walioumbwa na Mungu. Biblia inasema: ‘Na malaika walisifu jina la Yehova; kwa maana yeye mwenyewe aliamuru, nao wakaumbwa.’Zaburi 148:2, 5.

Biblia inafunua kwamba mamilioni ya malaika waaminifu, kutia ndani maserafi na makerubi, hutimiza kwa uaminifu majukumu hususa waliyopewa kulingana na vyeo na migawo yao. (Zaburi 103:20, 21; Isaya 6:1-7; Danieli 7:9, 10) Je, ilibidi wanadamu wafe ili Mungu atokeze malaika hao wote? Kwa kweli hilo haliwezekani. Kwa nini?

Biblia inaonyesha kwamba malaika waliumbwa muda mrefu sana kabla ya wanadamu. Yehova alipoumba dunia ambayo wanadamu wangeishi ndani yake muda mrefu baadaye, malaika wanaotajwa kwa njia ya kishairi kuwa nyota za asubuhi ‘walipiga vigelegele pamoja kwa shangwe na wakaanza kupaaza sauti kwa kushangilia.’ (Ayubu 38:4-7) Hivyo malaika waliumbwa miaka mingi sana kabla ya mwanadamu.

Isitoshe, malaika na wanadamu hutofautiana sana kimaumbile na pia kuhusiana na wajibu wao katika kusudi la Yehova. * Mungu alimuumba mwanadamu akiwa “mdogo kidogo kuliko malaika,” kwa hiyo, viumbe hao wa roho huonwa kuwa wana nguvu na akili inayopita ile ya mwanadamu. (Waebrania 2:7) “Makao yanayofaa” kwa malaika ni mbinguni. (Yuda 6) Lakini, kulingana na kusudi la Mungu la awali, mwanadamu alipaswa kuishi duniani. (Mwanzo 1:28; 2:17; Zaburi 37:29) Kama wanadamu wawili wa kwanza wangemtii Mungu, hawangekufa. Kwa hiyo, tangu mwanzo, wanadamu na malaika wamekuwa na wajibu tofauti kabisa katika kusudi la Mungu.

Inakuwaje Mtu Anapokufa?

Maswali mengine muhimu ambayo tunahitaji kuchunguza ni: Inakuwaje wanadamu wanapokufa? Je, wao huendelea kuishi lakini katika umbo lingine, pengine wakiwa malaika katika makao ya roho? Biblia inatoa jibu hili rahisi na lenye kueleweka: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Kwa hiyo wanadamu hawaendelei kuwa hai wanapokufa. Wafu hawajui wala hawahisi lolote.

Je, kuna tumaini lolote kwa wafu? Ndiyo! Biblia inaonyesha kwamba wanadamu wengi waliokufa wana tumaini la kufufuliwa. Wengi wao watafufuliwa wakiwa wanadamu, nao wataishi katika dunia itakayokuwa paradiso.—Luka 23:43; Yohana 5:28.

Wanadamu wachache wana tumaini la kufufuliwa na kuishi mbinguni. Idadi yao ni ndogo, yaani, 144,000. Hata hivyo, hawa 144,000 wanatofautiana kabisa na viumbe ambao kwa kawaida wanaitwa malaika. Wakiwa viumbe wasioweza kufa, wale 144,000 watatawala pamoja na Kristo wakiwa wafalme na makuhani. Wamepewa mamlaka ya kuhukumu. (1 Wakorintho 6:3; Ufunuo 20:6) Je, wao ni watoto ambao wamekufa? La. Wao ni wafuasi wa Kristo ambao wamejaribiwa kikamili!—Luka 22:28, 29.

Fikiria pia tofauti iliyopo kati ya wanadamu waliokufa na malaika walio hai. Wanadamu waliokufa “hawajui lolote kamwe,” lakini malaika wako macho kabisa, wana hisia, na wanaweza kufanya maamuzi. Wana uhuru wa kuchagua. (Mwanzo 6:2, 4; Zaburi 146:4; 2 Petro 2:4) Wafu wanafafanuliwa kuwa “wasiojiweza,” au wasio na nguvu, hali malaika wana “uwezo katika nguvu.” (Isaya 26:14; Zaburi 103:20) Na ingawa wanadamu ambao ni wazao wa Adamu hufa kwa sababu ya dhambi na kutokamilika, malaika wanaomwogopa Mungu ni wakamilifu, nao wana kibali cha Yehova.—Mathayo 18:10.

Wazo la kwamba malaika ni nafsi za wanadamu waliokufa linaweza kutumiwa kuwa msingi wa hadithi katika vipindi vya televisheni au sinema, lakini haliungwi mkono na Maandiko. Kweli za Biblia zilizotajwa katika makala hii zinatusaidia kuepuka kuwa na maoni yasiyo sahihi kuhusu hali ya wapendwa wetu wanapokufa. Nayo Biblia inatuhakikishia kwamba malaika waaminifu, walioumbwa wakiwa malaika na ambao ni watumishi wa Mungu wenye nguvu, wana uwezo mkubwa kuliko wanadamu nao sikuzote huwa tayari kufanya mapenzi ya Yehova. Inapendeza kujua kwamba mapenzi ya Mungu yanatia ndani kuwatumia malaika kuwalinda na kuwasaidia wale ambao wanamheshimu Yehova kikweli na kumtumikia.—Zaburi 34:7.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

Je, wapendwa wako waliokufa sasa ni malaika wanaomtumikia Mungu mbinguni?Mhubiri 9:5, 10.

Je, watoto hufa kwa sababu Mungu anataka kuongeza idadi ya malaika wanaomzunguka?Ayubu 34:10.

Je, wafu wanaweza kurudi na kuwalinda wale walio hai?Isaya 26:14.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Neno “malaika,” ambalo kihalisi humaanisha “mjumbe,” nyakati nyingine huwa na maana pana. Linaweza kurejelea viumbe mbalimbali wa roho hata wanadamu wanaomtumikia Mungu. Hata hivyo, katika makala haya, tunarejelea viumbe wa roho ambao kwa kawaida Biblia huwaita malaika.

[Blabu katika ukurasa wa 29]

‘Na malaika walisifu jina la Yehova; kwa maana yeye mwenyewe aliamuru, nao wakaumbwa.’—Zaburi 148:2, 5