Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naweza Kuwasaidiaje Wenye Uhitaji?

Naweza Kuwasaidiaje Wenye Uhitaji?

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kuwasaidiaje Wenye Uhitaji?

“Natumaini kwamba nikimaliza shule, nitakuwa fundi wa umeme. Ninataka kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme.”—Tristan, miaka 14.

“Ninatoa mchango wa dola 20 kwa ajili ya mashine mpya za kuchapishia. Hizo zilikuwa pesa zangu za matumizi, lakini nataka kuwapa.”—Abby, miaka 9.

VIJANA wengi, kutia ndani wale walionukuliwa, wanathibitisha kwamba vijana hawana ubinafsi kama vile watu fulani leo wanavyodhani. Vijana wengi Mashahidi wa Yehova, hutumia wakati, nguvu, na mali zao kuwatumikia wengine. (Zaburi 110:3) Fikiria mifano mingine.

Muda mfupi tu baada ya nyanya yake kufa, Jirah, mwenye umri wa miaka saba, anayeishi Australia alipokea zawadi ya dola 50 kutoka kwa babu yake. Jirah alifanya nini na pesa hizo? Katika mkutano uliofuata, alitumbukiza pesa hizo zote kwenye sanduku la mchango. Kwa nini? Jirah alimwambia hivi mama yake: “Nina vitu vingi vya kuchezea, lakini nilikuwa na nyanya mmoja tu. Najua kwamba nyanya angetaka nitoe pesa hizo kama mchango kwa kuwa alimpenda sana Yehova.”

Hannah, mwenye umri wa miaka mitano anaishi Marekani na anapenda farasi. Alitaka kununua farasi bandia ambaye angegharimu dola 75. Ili kumfunza Hannah umuhimu wa kuweka akiba, mara kwa mara wazazi wake walimpa pesa alizohifadhi kwenye kisanduku kidogo. Muda si mrefu, Hannah alikuwa na pesa za kutosha kununua farasi huyo.

Hata hivyo, karibu wakati huohuo, Tufani Katrina ilisababisha madhara kwenye pwani ya Marekani inayopakana na Ghuba ya Mexico. Hannah alihangaikia hali ya walioathiriwa na tufani hiyo, kwa hiyo akaamua kutoa pesa zote alizokuwa nazo akibani, yaani, zaidi ya dola 100, ili kuwasaidia. Hannah aliandikia makao makuu ya Mashahidi wa Yehova barua iliyosema hivi: “Nawapa pesa hizi kwa sababu ninampenda Yehova na nataka kusaidia.” Je, Yehova huona vitendo kama hivyo vya ukarimu? Biblia inasema: “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.”—Waebrania 13:16.

Msichana mmoja mchanga anayeitwa Tiffany, ambaye pia anatoka Marekani, aliandikia makao makuu ya Mashahidi wa Yehova barua baada ya tufani mbili kukumba Florida mwaka wa 2004. Alisema hivi: “Mimi na ndugu yangu Timothy tungependa kutoa dola 110 kama mchango. Nyumba yetu haikuharibiwa sana, lakini tuliona jinsi nyumba nyingi zilivyoharibiwa na dhoruba hiyo. Tulitaka kusaidia, kwa hiyo tukaanza kuweka pesa zetu akiba. Timothy alilipwa dola 10 kwa kusaidia kuondoa karatasi zilizokuwa zimebandikwa ukutani kwa chokaa katika nyumba moja, nami nilifaulu kuweka akiba dola 100.” Tiffany ana miaka 13, naye Timothy, ndugu yake ana miaka 7 tu! Inakuwaje tunapotanguliza faida za wengine? Methali 11:25 inasema hivi: “Anayenywesha wengine kwa ukarimu yeye mwenyewe pia atanyweshwa kwa ukarimu.”

Kikundi cha vijana Mashahidi huko Marekani waliokuwa na umri wa kati ya miaka 4 na 15, walipata habari kwamba waamini wenzao barani Afrika wanahitaji Majumba ya Ufalme. Hivyo, waliamua kuchukua hatua. “Tuliuza keki na kupata dola 106.54. Tuliwaambia watu kwamba huenda pesa hizo zikatumiwa Afrika kujenga mahali pa kujifunzia Biblia. Wengi walinunua keki hizo. Ilichukua saa tisa kuziuza, lakini hatukuchoka kwa kuwa tulikuwa tukifanya hivyo kwa ajili ya Yehova!”

Unaweza Kusaidia

Vijana waliotajwa katika makala hii wameona ukweli wa maneno ya Yesu: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Wewe pia unaweza kupata furaha ya kutoa. Unaweza kutoa katika njia zipi?

Je, umepata habari kwamba waamini wenzako wanahitaji msaada? Kwa mfano, je, kumetokea msiba wa asili? Hebu wazia jinsi ambavyo ungehisi ikiwa ungepoteza makao, mali, au hata kufiwa na mpendwa. Mtume Paulo aliandika kwamba Wakristo wanapaswa ‘kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yao wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’ (Wafilipi 2:4) Hata kama unaishi mbali na eneo lililokumbwa na msiba wa asili, huenda mchango wako ukasaidia katika kazi ya kutoa msaada inayofanywa na Mashahidi wa Yehova. *

Unaweza kuwasaidia wenye uhitaji katika njia nyingine. Kwa mfano, ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, fikiria wale walio kwenye Jumba lenu la Ufalme. Je, kuna wazee au watu wengine wanaohitaji msaada? Unaweza kuwasaidia kufanya kazi mbalimbali? Mtume Paulo aliwaandikia hivi Waroma: “Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Waroma 12:10) Unapoona kwamba kuna uhitaji, uwe wa kwanza kutenda. Uwe tayari kufanya hata kazi za hali ya chini. Na ukumbuke kwamba kuwatumikia wengine kunahusiana kwa ukaribu na kumtumikia Mungu. Biblia inasema: “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, na Yeye atamlipa matendo yake.”—Methali 19:17.

Bila shaka, njia kuu zaidi ya kuwasaidia wengine ni kwa kuwaambia yale ambayo umejifunza kutoka katika Neno la Mungu, Biblia. Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Sasa kuliko wakati mwingine, watu wanahitaji kusikia kweli zenye kuokoa uhai za Biblia. Kwa hiyo, endelea kuhubiri kwa bidii na kwa ukawaida ukiwa na uhakika kwamba ‘kazi yako si ya bure.’—1 Wakorintho 15:58.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Michango inayotolewa kwa ajili ya msiba fulani hususa huthaminiwa sana. Hata hivyo, inapendekezwa kwamba michango hiyo iwekwe katika sanduku la michango ya kazi ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova kwa kuwa pesa hizo zinaweza kutumiwa kunapokuwa na uhitaji.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Unajua mtu yeyote anayehitaji msaada?

▪ Unaweza kumsaidia katika njia zipi?

[Blabu katika ukurasa wa 25]

“Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.”—Waebrania 13:16

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]

KWA NINI UJIZOEZE KUTOA?

“Kuona jinsi wazazi wangu walivyotumia wakati na nguvu zao kumtumikia Yehova na jirani zao kulinifanya nitake kutumia maisha yangu katika njia hiyo. Baba yangu aliniambia hivi: ‘Jambo lolote unalofanya kwa ajili ya Yehova, hata liwe dogo namna gani, hudumu milele. Yehova huishi milele, naye atalikumbuka milele. Lakini kuishi kwa ajili yako mwenyewe ni ubatili. Ukifa, kazi zako zitakoma pamoja nawe.’”—Kentaro, miaka 24, Japani.

“Kwa kweli, sikutaka kutumia wakati wangu Jumamosi alasiri kuwasaidia wazee kazi za nyumbani. Nilitaka tu kustarehe na rafiki zangu. Hata hivyo, nilipokaa na wazee hao, nilifurahia sana. Nilikuja kuelewa kwamba wao ni watu kama mimi, na wakati mmoja walikuwa vijana. Jambo hilo lilinichochea kuwasaidia.”—John, miaka 27, Uingereza.

“Nilipokuwa mchanga, nilishiriki katika utendaji mwingi kutia ndani kusafisha Jumba la Ufalme. Pia nilifurahia kufanya kazi ngumu kwa ajili ya wengine kutanikoni. Unapowasaidia wengine unaona shangwe wanayopata. Kwa mfano, wakati mmoja, mimi pamoja na ndugu wengine tulimbandikia dada mmoja mzee karatasi za ukutani katika nyumba yake. Alifurahi sana! Unapomfurahisha mtu, wewe pia unafurahi.”—Hermann, miaka 23, Ufaransa.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Wachanga wengi huchanga pesa za kusaidia watu waliokumbwa na msiba