Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Nitapanda Juu Kama Vile Paa Anavyofanya’

‘Nitapanda Juu Kama Vile Paa Anavyofanya’

‘Nitapanda Juu Kama Vile Paa Anavyofanya’

SIMULIZI LA FRANCESCO ABBATEMARCO

“Kwa nini Mungu aliruhusu jambo hili litukie? Kwa nini linipate mimi?” Nilijiuliza maswali hayo mara nyingi sana. Nisingevumilia wazo la kuishi nikitumia kiti cha magurudumu, bila uwezo wa kutumia mikono na miguu yangu.

MNAMO 1962, katika mji mmoja mdogo huko Basilicata, Italia, karibu nife nilipozaliwa. Mama yangu alikuwa na matatizo alipokuwa akijifungua, naye daktari akamdunga sindano ambazo zilitokeza madhara makubwa. Siku tatu baadaye, misuli ya mwili wangu mdogo ikanyauka. Mikono na miguu yangu ilipooza na viungo vyangu vya sauti vikaharibika.

Nilipokuwa mtu mzima, nilifadhaishwa kabisa na hali yangu. Nilikasirika-kasirika na mara nyingi niliwafokea watu waliokuwa karibu nami. Nilijihisi kuwa nimetengwa na ulimwengu wote, na maisha yangu hayakuwa na kusudi. Kufikia wakati nilipokuwa na umri wa miaka 25, singeweza kudhibiti hisia zangu. Sikuelewa sababu iliyofanya Mungu aniruhusu niteseke sana. Hivyo, niliona kuwa inafaa kuamini kwamba hakuna Mungu.

Mtazamo Tofauti

Asubuhi moja mwishoni mwa 1987, nilipokuwa nimeketi kwenye kiti cha magurudumu nje ya nyumba, vijana wawili waliovalia vizuri walinikaribia. Nilifikiri kwamba walitaka kuzungumza na kaka yangu kwa hiyo nikakaza sana viungo vyangu vya sauti na kuwaambia kwamba ndugu yangu hakuwa nyumbani. Lakini waliniambia: “Tunataka kuzungumza na wewe.” Hilo lilinishangaza kwani ni watu wachache sana waliopendezwa kuzungumza nami.

Waliniuliza, “Je, unaamini kwamba kuna Mungu?” Kwa njia isiyo ya kirafiki niliwajibu hivi, “Katika hali yangu, ninawezaje kumwamini?” Tulianza mazungumzo, nami nikagundua kwamba walikuwa Mashahidi wa Yehova. Walinitolea kitabu chenye kichwa Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? * nami nikakichukua shingo upande. Walisema kwamba wangerudi, nami nilitumaini kwamba hawangerudi.

Mashahidi hao wawili walirudi kama walivyokuwa wameahidi nasi tukaendelea na mazungumzo yetu. Ninakumbuka mistari ya Biblia ambayo walinisomea. Ilikuwa Isaya 35:5, 6: “Wakati huo macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Wakati huo kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha.” Maneno hayo yalipendeza sana lakini yalikuwa tofauti sana na maisha yangu. Singeweza hata kusimama, sembuse kupanda juu kama paa. Hata hivyo, nilikubali kujifunza Biblia pamoja nao lakini sikuamini kwamba Biblia ingenisaidia kukabiliana na matatizo yangu. Wazo la kwamba ulemavu wangu ungeisha siku moja lilionekana kuwa ndoto tu.

Baada ya muda, Mashahidi hao walinikaribisha kwenye mikutano yao katika Jumba la Ufalme. Siwezi kukumbuka hotuba ya Biblia iliyotolewa, lakini siwezi kusahau urafiki na upendo ambao Mashahidi walinionyesha. Badala ya kunihurumia, walinifanya nihisi nimekaribishwa kabisa. Jumapili hiyo nilijua kwamba ningeweza kujihisi huru kuwa kwenye Jumba la Ufalme, nami nikaanza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida.

Kizuizi Kikubwa

Kujifunza Neno la Mungu kulikuwa na matokeo makubwa katika moyo wangu. Ni kana kwamba mti ulionyauka ulianza kuwa tena na umajimaji ndani yake. Nilipata hisia ambazo nilifikiri zilikuwa zimekufa na kuzikwa. Ilipendeza kama nini kuwa hai tena! Nilitamani kuwaeleza wengine kuhusu tumaini zuri ajabu ambalo nilikuwa nimepokea. (Mathayo 24:14) Hata hivyo, ningewezaje kuanza kuhubiri? Nilisali kwa bidii kuhusu tamaa yangu na kumwomba Yehova anionyeshe njia ya kuhubiri.

Septemba 1991, painia (mweneza-injili wa wakati wote) alitumwa katika kutaniko langu. Siku moja nikiwa nyumbani kwake nilimweleza tamaa yangu ya kuhubiri. Singeweza kuongea vizuri, kwa hiyo tulizungumza kwa kutumia taipuraita kuandika herufi. Mikono yangu iliyokuwa imepooza ilikuwa kizuizi. Kwa msaada wa painia huyo tulijaribu mbinu mbalimbali. Nilijaribu kushika penseli kwa meno yangu na kupiga chapa. Kisha, nilijaribu kutumia kofia ngumu iliyounganishwa kijiti nami nikasogeza kichwa ili kupiga chapa. Ilionekana ni kama hakuna mbinu yoyote iliyofua dafu.

Baadaye tulipokuwa tukizungumzia tatizo hilo, painia huyohuyo alisema hivi kwa mzaha: “Una pua nzuri sana.” Mara moja nilijaribu kupiga chapa kwa kutumia pua yangu na nikafaulu. Mwishowe ningeweza kuandika. Hebu wazia jitihada iliyohitajika kutumia pua kusahihisha herufi kila mara nilipokosea! Niligundua kwamba ilikuwa rahisi zaidi kutumia kompyuta. Lakini ningepata wapi pesa za kuinunua? Nilingojea wakati unaofaa kisha nikazungumza na wazazi wangu. Punde si punde nilikuwa nikitumia kompyuta kuandika barua.

Tamaa Yangu Inatimizwa

Kwanza niliwaandikia barua marafiki na watu wa ukoo, kisha nikawaandikia watu walioishi katika mji wa kwetu na miji jirani. Muda si muda nilikuwa nikiwasiliana na watu kotekote nchini Italia. Ni vigumu kueleza shangwe niliyopata kila mara nilipopokea barua ya majibu. Desemba 1991, nilistahili kuwa mhubiri wa habari njema ambaye hajabatizwa. Pia nilijiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ambayo ni shule inayofanywa kila juma katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Nilipopokea mgawo wa kutoa hotuba, niliitayarisha kwa uangalifu nyumbani kwa kutumia kompyuta yangu. Kwenye mikutano, mmoja wa rafiki zangu angeenda jukwaani na kusoma habari niliyokuwa nimetayarisha.

Nikiwa na shukrani kwa upendo ambao Yehova alikuwa akinionyesha, nilijua kwamba hatua zilizofuata ili kufanya maendeleo zilikuwa kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa. Nilipata ujasiri na kuzungumza na wazazi wangu kuhusu uamuzi wangu. Hawakufurahi, lakini tamaa yangu ya kubatizwa ilizidi woga wangu. Kwa msaada wa Yehova na Mashahidi wenzangu, nilibatizwa Agosti 1992. Nilifurahi sana ndugu yangu na shemeji walipohudhuria ubatizo wangu!

Kubadili Mtazamo Wangu

Kanuni za Neno la Mungu zilipozidi kuwa wazi kwangu, niliona uhitaji wa kubadili tabia fulani zisizofaa. Nilitambua kwamba kwa sababu ya hali yangu ya kimwili, nilikuwa na ubinafsi. Nilijitahidi sana kuondoa kasoro hizo. Nilihitaji kuwa mnyenyekevu zaidi na kung’ang’ana na hisia za kukata tamaa zilizotokana na kulazimika kuwategemea wengine.

Pia nilijitahidi kuacha kujihurumia na kujiona kuwa hohehahe. Nilianza kuona ucheshi wa mambo fulani. Siku moja nilipokuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba msichana mdogo alifungua mlango. Mmoja wa Mashahidi niliokuwa nao akamwuliza ikiwa wazazi wake walikuwako. Msichana huyo mdogo alipaaza sauti, “Mama, kuna watu wawili na mgonjwa mmoja kwenye mlango.” Aliponiona, mama huyo aliaibika sana hivi kwamba hakujua aseme nini. Mmoja wa rafiki zangu akasema: “Kwa kweli, kuna watu wawili wagonjwa na mmoja mwenye afya nzuri.” Sote tulitabasamu kisha tukawa na mazungumzo mazuri.

Natamani Kutumikia Zaidi

Baada ya kubatizwa nilitumika nikiwa painia msaidizi kwa miezi tisa, nikitumia saa 60 kwa mwezi katika kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, nilitaka kufanya mengi zaidi. Nilianza utumishi wa upainia wa kawaida, nikitumia wakati mwingi zaidi katika kazi ya kuhubiri. Miezi ya kwanza ya utumishi wa painia ilikuwa migumu. Watu wengi walifikiri kwamba nilikuwa mlangoni kwao nikitaka kuomba pesa, na hilo liliniaibisha pamoja na Mashahidi walioandamana nami.

Isitoshe, ilikuwa vigumu kwa wengi katika kutaniko kuelewa maneno yangu nao hawakujua njia nzuri zaidi ya kunisaidia. Lakini kwa msaada wa Yehova na msaada usio na ubinafsi wa akina ndugu na dada zangu wa kiroho, hali yangu ilizidi kuwa bora. Sasa watu hawanioni tu kuwa mwanamume aliye katika kiti cha magurudumu bali kama Shahidi wa Yehova ambaye hujaribu kuwasaidia wengine wajue makusudi ya Mungu.

Katika Julai 1994, nilihudhuria shule ya pekee ya majuma mawili ya kuwazoeza mapainia. Huko tulijifunza kanuni za Maandiko ambazo huongoza kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Pia tulipokea mazoezi katika kazi ya kuhubiri. Nilihitaji kukabiliana na vizuizi ili nihudhurie, kwa kuwa shule hiyo ilifanyiwa kilometa 60 hivi kutoka mahali nilipoishi. Singeweza kulala mbali na nyumbani, hivyo Mashahidi walikuwa na zamu kunipeleka shuleni asubuhi na kunirudisha jioni. Wakati wa chakula cha mchana mmoja wao angenibeba hadi kwenye orofa ya pili, ambako sote tulikula pamoja.

Daraka Kubwa

Mnamo Machi 2003, niliwekwa rasmi kuwa mzee wa kutaniko. Mgawo huo umenilazimu kufanya kazi ngumu kwa ajili ya wengine. Sasa ninaelewa zaidi alichomaanisha Yesu aliposema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Ninatumika pamoja na baraza zuri la wazee, nao wamenisaidia kutimiza mgawo wangu. Mimi huhisi kwamba kutaniko lote hufurahi kuwa pamoja nami, hasa vijana, nao hunihusisha katika shughuli zao. Wao huona jinsi ambavyo nimekabiliana na vizuizi ili nimtumikie Yehova, na wengi wao huniomba msaada wanapokabili matatizo.

Nimejifunza kwamba furaha ya mtu haitokani na hali yake ya kimwili. Badala ya hivyo, jambo muhimu ni kuwa na kibali cha Yehova na kufanya mapenzi yake. Ninamshukuru zaidi kwa tumaini zuri ajabu la kuniondolea kiti changu cha magurudumu. Naam, ninatazamia wakati ambapo ‘nitapanda juu kama vile paa anavyofanya’ na kumtumikia Mungu wa kweli kwa umilele wote.—Isaya 35:5, 6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Sasa watu hawanioni tu kuwa mwanamume aliye katika kiti cha magurudumu bali kama Shahidi wa Yehova ambaye hujaribu kuwasaidia wengine wafahamu makusudi ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kujitayarisha kwa ajili ya mkutano wa kutaniko kwa kutumia pua yangu kupiga chapa