Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Alitumia Mageuzi Kuumba Uhai?

Je, Mungu Alitumia Mageuzi Kuumba Uhai?

Je, Mungu Alitumia Mageuzi Kuumba Uhai?

“Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.”—UFUNUO 4:11.

MUDA mfupi baada ya Charles Darwin kufanya nadharia ya mageuzi iwapendeze watu wengi, madhehebu mengi yanayodai kuwa ya Kikristo yalianza kutafuta njia ya kupatanisha imani kwamba kuna Mungu na nadharia ya mageuzi.

Leo, inaonekana vikundi vingi maarufu vya kidini vinavyodai kuwa vya Kikristo vinakubali kuwa Mungu alitumia mageuzi kwa njia fulani kuumba uhai. Wengine hufundisha kwamba Mungu aliutayarisha ulimwengu kwa njia ambayo uhai ungetokana na kemikali zisizo na uhai ambazo zingebadilika hatua kwa hatua na hatimaye kutokeza wanadamu. Wale wanaounga mkono fundisho hilo, hawahisi kwamba Mungu aliingilia kati baada ya mageuzi hayo kuanza. Wengine hufikiri kwamba kwa ujumla Mungu aliacha mageuzi yatokeze jamii nyingi za mimea na wanyama lakini mara kwa mara akaingilia mambo ili kuendeleza mageuzi hayo.

Je, Mafundisho Hayo Yanaweza Kupatanishwa?

Je, nadharia ya mageuzi inapatana na mafundisho ya Biblia? Ikiwa nadharia ya mageuzi ingekuwa kweli, basi simulizi la Biblia kuhusu uumbaji wa mtu wa kwanza, Adamu, lingekuwa tu hadithi iliyokusudiwa kufunza mambo fulani mazuri lakini haipaswi kuchukuliwa kihalisi. (Mwanzo 1:26, 27; 2:18-24) Je, Yesu aliona simulizi hilo la Biblia kuwa hadithi tu? “Je, hamkusoma,” Yesu akasema, “kwamba yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—Mathayo 19:4-6.

Yesu alikuwa akinukuu simulizi la uumbaji lililorekodiwa katika Mwanzo sura ya 2. Ikiwa Yesu aliamini kwamba ndoa hiyo ya kwanza ilikuwa hadithi ya kuwaziwa tu, je, angeirejelea ili kuthibitisha fundisho lake kuhusu utakatifu wa ndoa? Hapana. Yesu alitaja simulizi hilo la Mwanzo kwa sababu alijua lilikuwa ni jambo hakika.—Yohana 17:17.

Vilevile, wanafunzi wa Yesu waliamini kwamba simulizi la Mwanzo kuhusu uumbaji lilikuwa la kweli. Kwa mfano, injili ya Luka ina orodha ya ukoo wa Yesu inayorudi nyuma hadi kwa Adamu. (Luka 3:23-38) Ikiwa Adamu alikuwa mtu wa kuwaziwa tu, ni majina mangapi katika orodha hiyo yangekuwa ya watu halisi na mangapi ya watu wa kuwaziwa tu? Ikiwa mtu wa kwanza katika orodha hiyo ya ukoo angekuwa wa kuwaziwa tu, dai la Yesu kwamba alikuwa Mesiya aliyezaliwa katika ukoo wa Daudi lingekuwa thabiti kadiri gani? (Mathayo 1:1) Luka, mwandikaji wa Injili alisema kwamba alikuwa ‘amefuata kwa uangalifu mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi.’ Kwa wazi yeye aliamini simulizi la uumbaji katika kitabu cha Mwanzo.—Luka 1:3.

Imani ya mtume Paulo katika Yesu ilihusiana na imani yake katika simulizi la Mwanzo. Aliandika hivi: “Kwa kuwa kifo ni kupitia mwanadamu, ufufuo wa wafu pia ni kupitia mwanadamu. Kwa maana kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.” (1 Wakorintho 15:21, 22) Ikiwa kwa kweli Adamu hakuwa babu ya wanadamu wote, yule ambaye kupitia kwake “dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi,” kwa nini Yesu alilazimika kufa kutangua matokeo ya dhambi iliyorithiwa?—Waroma 5:12; 6:23.

Kudhoofisha imani katika simulizi la uumbaji katika kitabu cha Mwanzo ni kudhoofisha misingi ya imani ya Kikristo. Nadharia ya mageuzi na mafundisho ya Kristo hayapatani. Kujaribu kupatanisha mafundisho hayo mawili kunaweza tu kutokeza imani dhaifu ambayo inaweza ‘kurushwa huku na huku kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho.’—Waefeso 4:14.

Imani Juu ya Msingi Imara

Kwa karne nyingi, Biblia imechambuliwa na kushambuliwa. Lakini, tena na tena maandishi ya Biblia yamethibitishwa kuwa ya kweli. Inapozungumzia mambo ya historia, afya, na sayansi, masimulizi yake yamethibitika kuwa yenye kutegemeka. Mashauri yake kuhusu mahusiano ya watu ni yenye kutumainika na yanayoweza kutumika wakati wowote ule. Falsafa na nadharia za wanadamu ni kama majani mengi mabichi ambayo hukua na kukauka, lakini Neno la Mungu “litadumu mpaka wakati usio na kipimo.”—Isaya 40:8.

Nadharia ya mageuzi si fundisho la wanasayansi tu. Ni falsafa ya wanadamu ambayo ilianza na kusitawi kwa makumi ya miaka. Hata hivyo, katika miaka ya karibuni mafundisho ya awali ya Darwin yamebadilika hatua kwa hatua kadiri ambavyo watu wamejaribu kupatanisha nadharia hiyo na uthibitisho unaozidi kuongezeka wa kwamba vitu vya asili vimebuniwa. Tunakutia moyo uichunguze habari hiyo zaidi. Unaweza kufanya hivyo kwa kusoma makala nyingine zilizo katika gazeti hili. Isitoshe, unaweza kusoma vichapo vilivyoonyeshwa kwenye ukurasa huu na ukurasa wa 32.

Baada ya kuchunguza habari hiyo, inaelekea kwamba imani yako katika yale ambayo Biblia inasema kuhusu wakati uliopita itaimarishwa. La muhimu zaidi, imani yako katika ahadi za Biblia kuhusu wakati ujao itaimarishwa. (Waebrania 11:1) Huenda pia ukachochewa kumsifu Yehova, ‘Mtengenezaji wa mbingu na dunia.’—Zaburi 146:6.

UNAWEZA KUSOMA HABARI ZAIDI KATIKA

Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote Mifano hususa inayothibitisha usahihi wa maandishi ya Biblia inapatikana katika broshua hii

Je, Kuna Muumba Anayekujali? Chunguza uthibitisho zaidi wa kisayansi, na upate kujua sababu inayomfanya Mungu anayejali aruhusu watu wateseke sana

Biblia Inafundisha Nini Hasa? Jibu la swali “Mungu ana kusudi gani kwa dunia?” linapatikana katika sura ya 3 ya kitabu hiki

[Blabu katika ukurasa wa 10]

Yesu aliamini masimulizi ya uumbaji yaliyo katika kitabu cha Mwanzo. Je, alikosea?

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

MAGEUZI NI NINI?

Maana moja ya neno “mageuzi” ni: “Mabadiliko ya hatua kwa hatua.” Hata hivyo, neno hilo hutumiwa katika njia kadhaa. Kwa mfano, hutumiwa kurejelea mabadiliko makubwa ya vitu visivyo na uhai, yaani, jinsi ulimwengu ulivyotokea. Pia, hutumiwa kufafanua mabadiliko madogo ya vitu vilivyo hai, yaani, jinsi mimea na wanyama wanavyobadilika ili wapatane na mazingira yao. Hata hivyo, mara nyingi neno hilo hutumiwa kufafanua nadharia ya kwamba uhai ulitokana na kemikali zisizo na uhai ambazo zilijifanyiza kuwa chembe zinazogawanyika na kutokeza chembe mpya. Kisha chembe hizo zikasitawi polepole na kuwa vitu tata vyenye uhai, mwanadamu akiwa kitu tata zaidi kilichotokezwa na mageuzi hayo. Ufafanuzi huo wa tatu ndio unaowakilishwa na neno “mageuzi” katika makala hii.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]

Space photo: J. Hester and P. Scowen (AZ State Univ.), NASA