Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Sayansi Inapingana na Masimulizi ya Mwanzo?

Je, Sayansi Inapingana na Masimulizi ya Mwanzo?

Maoni ya Biblia

Je, Sayansi Inapingana na Masimulizi ya Mwanzo?

WATU wengi hudai kwamba sayansi inapinga masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji. Lakini, sayansi haipingani na Biblia bali inapingana na maoni ya Wakristo wenye imani kali. Baadhi ya Wakristo hao husisitiza kwa uwongo kwamba, kulingana na Biblia, vitu vyote vinavyoonekana viliumbwa katika kipindi cha siku sita zenye urefu wa saa 24 kila moja, yapata miaka 10,000 hivi iliyopita.

Hata hivyo, Biblia haiungi mkono fundisho hilo. Iwapo ingefanya hivyo, uvumbuzi mwingi wa kisayansi, ambao umefanywa katika muda wa miaka mia moja iliyopita, ungefanya Biblia itiliwe shaka. Kuchunguza Biblia kwa makini kumethibitisha kwamba mambo hakika ya sayansi hayapingani na Biblia. Kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova hawakubaliani na “Wakristo” wenye imani kali wala wanauumbaji, yaani, watu wanaodai kwamba vitu vyote vinavyoonekana viliumbwa katika kipindi cha siku sita zenye urefu wa saa 24 kila moja, yapata miaka 10,000 hivi iliyopita. Habari ifuatayo inaonyesha kile ambacho Biblia inafundisha hasa.

“Mwanzo” Ulikuwa Lini?

Masimulizi ya Mwanzo yanaanza kwa taarifa hii fupi yenye nguvu: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Wasomi wa Biblia wanakubali kwamba taarifa hiyo inafafanua jambo tofauti na matukio yaliyotendeka katika zile siku sita za uumbaji. Matukio hayo yanasimuliwa kuanzia mstari wa 3 na kuendelea. Hilo ni jambo muhimu sana. Kulingana na taarifa ya ufunguzi ya Biblia, ulimwengu wote, kutia ndani Dunia, ulikuwapo kwa kipindi kisichojulikana kabla ya zile siku sita za uumbaji.

Wanajiolojia wanakadiria kwamba dunia imekuwapo kwa miaka bilioni 4, nao wanaanga wanasema huenda ulimwengu umekuwapo kwa miaka bilioni 15. Je, kauli hizo, au marekebisho yoyote ya ufahamu wetu kuhusu muda ambao ulimwengu, kutia ndani dunia, umekuwapo, zinapingana na Mwanzo 1:1? La. Biblia haisemi chochote kuhusu muda ambao “mbingu na dunia” zimekuwapo. Sayansi haipingi masimulizi ya Biblia.

Siku za Uumbaji Zilikuwa na Urefu Gani?

Vipi zile siku za uumbaji? Je, zilikuwa siku halisi zenye urefu wa saa 24 kila moja? Watu fulani hudai kwamba kwa kuwa Musa—aliyeandika kitabu cha Mwanzo—alirejelea siku iliyofuata siku sita za uumbaji kuwa mfano wa Sabato ya kila juma, lazima kila mojawapo ya siku hizo za uumbaji iwe ilikuwa na urefu wa saa 24. (Kutoka 20:11) Je, maneno ya Mwanzo yanaunga mkono kauli hiyo?

La hasha. Ukweli ni kwamba, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “siku” halimaanishi tu kipindi cha saa 24, bali pia linamaanisha vipindi vya wakati vyenye urefu tofauti. Kwa mfano, akieleza kwa ufupi kazi ya Mungu ya uumbaji, Musa anarejelea kipindi hicho cha siku sita kuwa siku moja tu. (Mwanzo 2:4) Bila shaka, hatuna msingi wowote wa Kimaandiko wa kukata kauli kwamba kila mojawapo ya siku za uumbaji ilikuwa na urefu wa saa 24.

Hivyo basi, siku hizo zilikuwa na urefu gani? Maneno ya Mwanzo sura ya 1 na ya 2 yanaonyesha zilikuwa vipindi virefu sana vya wakati.

Viumbe Vyatokea Hatua kwa Hatua

Musa aliandika masimulizi yake katika Kiebrania, naye alisimulia mambo kama mtu ambaye yuko duniani. Mambo hayo mawili, kutia ndani uhakika wa kwamba ulimwengu wote ulikuwapo kabla ya zile “siku” za uumbaji, hujibu maswali mengi ambayo yamezushwa kuhusu masimulizi ya uumbaji. Jinsi gani?

Uchunguzi makini wa masimulizi ya Mwanzo unaonyesha kwamba matukio yanayoanza katika “siku” fulani yanaendelea kutukia siku moja au siku kadhaa zinazofuata. Kwa mfano, kabla ya “siku” ya kwanza, nuru ya jua, ambalo tayari lilikuwapo, ilizuiwa kwa njia fulani isiupige uso wa dunia. Labda ilikuwa ikizuiwa na mawingu mazito. (Ayubu 38:9) Kizuizi hicho kilianza kuondoka katika “siku” ya kwanza, na hivyo kuruhusu nuru ipenye kwenye anga la dunia. *

Katika “siku” ya pili, anga lilizidi kuwa wazi, na hivyo kukawa na nafasi kati ya mawingu mazito yaliyokuwa juu na bahari iliyokuwa chini. Katika “siku” ya nne, anga lilikuwa wazi kabisa hatua kwa hatua hivi kwamba jua na mwezi zilionekana “katika anga la mbingu.” (Mwanzo 1:14-16) Kwa maneno mengine, mtu aliye duniani angeweza kuona jua na mwezi. Yote hayo yalitukia hatua kwa hatua.

Masimulizi ya Mwanzo yanataja pia kwamba anga lilizidi kuwa wazi, kisha viumbe wanaoruka—kutia ndani wadudu na viumbe wengine wenye mabawa—wakaanza kutokea katika “siku” ya tano. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba katika “siku” ya sita, bado Mungu alikuwa “akifanya kutoka katika udongo kila mnyama wa mwituni na kila kiumbe kinachoruka cha mbinguni.”—Mwanzo 2:19.

Kwa wazi, maneno ya Biblia, yanaonyesha kwamba kuna uwezekano matukio fulani muhimu ya kila “siku” au kipindi cha uumbaji hayakutendeka mara moja bali yalitendeka hatua kwa hatua. Baadhi ya matukio hayo huenda hata yaliendelea hadi “siku” ya uumbaji iliyofuata.

Kulingana na Aina Yake

Je, uhakika wa kwamba mimea na wanyama walitokezwa hatua kwa hatua unamaanisha Mungu alitumia mageuzi kutokeza aina mbalimbali za vitu hai? La. Masimulizi hayo yanataja waziwazi kwamba Mungu aliumba “aina” zote za msingi za mimea na wanyama. (Mwanzo 1:11, 12, 20-25) Je, “aina” hizo za awali zilipewa uwezo wa kiasili wa kubadilika kulingana na mazingira? Kila “aina” ina mipaka gani ya kiasili? Biblia haisemi chochote kuhusu jambo hilo pia. Hata hivyo, inasema viumbe hai ‘walijaa kulingana na aina zake.’ (Mwanzo 1:21) Taarifa hiyo inamaanisha kwamba kulikuwa na mipaka ya kiasili iliyodhibiti tofauti za viumbe katika kila “aina.” Uchunguzi wa mabaki ya kale ya mimea na wanyama na pia utafiti wa karibuni, unaunga mkono kauli ya kwamba aina za msingi za mimea na wanyama zimebadilika kidogo katika kipindi kirefu sana cha wakati.

Kinyume na madai ya watu fulani, kitabu cha Mwanzo hakifundishi kwamba ulimwengu, kutia ndani dunia na viumbe hai vilivyomo, viliumbwa katika kipindi kifupi cha wakati, muda usio mrefu sana uliopita. Badala yake, masimulizi ya Mwanzo kuhusu kuumbwa kwa ulimwengu na vitu hai duniani yanapatana na uvumbuzi wa karibuni wa kisayansi.

Imani za kifalsafa za wanasayansi wengi huwafanya wapinge fundisho la Biblia kwamba Mungu aliumba vitu vyote. Hata hivyo, inapendeza kwamba, katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo kilichoandikwa zamani, Musa aliandika kuwa ulimwengu ulikuwa na mwanzo na uhai ulitokea hatua kwa hatua, katika vipindi vya wakati. Musa angewezaje kupata habari hizo zilizo sahihi kisayansi yapata miaka 3,500 hivi iliyopita? Kuna jibu moja tu linalopatana na akili. Yule aliye na nguvu na hekima ya kuumba mbingu na dunia angeweza kwa hakika kumpa Musa habari hizo zilizo sahihi kisayansi. Jibu hilo linaunga mkono dai la Biblia kwamba ‘imeongozwa na roho ya Mungu.’—2 Timotheo 3:16.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Mungu aliumba ulimwengu kitambo gani?—Mwanzo 1:1.

▪ Dunia iliumbwa katika kipindi cha siku sita zenye urefu wa saa 24 kila moja?—Mwanzo 2:4.

▪ Masimulizi ya Musa kuhusu mwanzo wa dunia yanawezaje kuwa sahihi kisayansi?—2 Timotheo 3:16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Katika masimulizi ya matukio ya “siku” ya kwanza, neno la Kiebrania linalotafsiriwa nuru ni ʼohr, lakini kuhusu “siku” ya nne, neno linalotumiwa ni ma·ʼohrʹ, linalomaanisha vyanzo vya nuru.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Kitabu cha Mwanzo hakifundishi kwamba ulimwengu uliumbwa katika kipindi kifupi cha wakati miaka kadhaa iliyopita

[Blabu katika ukurasa wa 20]

“Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.”—Mwanzo 1:1

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 18]

Universe: IAC/RGO/David Malin Images

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 20]

NASA photo