Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unayoamini Ni Muhimu?

Je, Unayoamini Ni Muhimu?

Je, Unayoamini Ni Muhimu?

JE, UNAFIKIRI uhai una kusudi? Ikiwa fundisho la mageuzi lingekuwa la kweli basi taarifa hii iliyonukuliwa katika jarida Scientific American ingekuwa sahihi: “Ufahamu wetu wa sasa kuhusu mageuzi unadokeza . . . kwamba uhai hauna kusudi halisi.”

Maneno hayo yanamaanisha nini? Ikiwa uhai hauna kusudi halisi, basi hauna kusudi lingine maishani ila tu kujaribu kutenda mema na, labda, kupitisha chembe zako za urithi kwa kizazi kinachofuata. Ukifa utakoma kuwako. Ubongo wako, pamoja na uwezo wake wa kuwaza, kufikiri, na kutafakari kuhusu kusudi la uhai ungekuwa tu umetokea bila mpango.

Lakini si hayo tu. Wengi wanaoamini mageuzi hudai kwamba hakuna Mungu au kwamba hataingilia mambo ya wanadamu. Vyovyote vile, wakati wetu ujao ungekuwa mikononi mwa wanasiasa, wasomi, na viongozi wa kidini. Matukio ya wakati uliopita yanaonyesha kwamba michafuko, mizozo, na ufisadi ambao umekithiri katika jamii ungeendelea. Ikiwa fundisho la mageuzi lingekuwa la kweli, yaelekea ingefaa kuishi kupatana na kauli hii ya watu wasiokuwa na tumaini: “Na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.”—1 Wakorintho 15:32.

Uwe na uhakika huu. Mashahidi wa Yehova hawakubaliani na maoni hayo yote. Wala hawakubaliani na fundisho la mageuzi ambalo ndilo msingi wa maoni hayo. Kinyume na hilo, Mashahidi wanaamini kwamba Biblia ni ya kweli. (Yohana 17:17) Kwa hiyo wanaamini kile ambacho Biblia inasema kuhusu wanadamu walivyotokea: “Kwako wewe iko chemchemi ya uzima.” (Zaburi 36:9) Maneno hayo yana maana kubwa.

Uhai una kusudi. Muumba wetu ana kusudi lenye upendo kuwaelekea watu wote wanaochagua kufanya mapenzi yake. (Mhubiri 12:13) Kusudi hilo linatia ndani ahadi ya kuishi katika ulimwengu usiokuwa na michafuko, mizozo, ufisadi, na hata kifo. (Isaya 2:4; 25:6-8) Mamilioni ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanaweza kuthibitisha kwamba kujifunza kumhusu Mungu na kufanya mapenzi yake humpa mtu kusudi maishani, kusudi ambalo hawezi kupata mahali pengine popote!—Yohana 17:3.

Kile unachoamini ni muhimu kwani kinaweza kuathiri furaha yako ya sasa na maisha yako ya wakati ujao. Chaguo ni lako. Je, utaamini nadharia ambayo imeshindwa kutupa sababu thabiti ya kupuuza uthibitisho mwingi uliopo kwamba ulimwengu ulibuniwa? Au utakubaliana na yale ambayo Biblia husema, yaani, ulimwengu na uhai ulitokezwa na Mbuni mwenye kustaajabisha, Yehova, Mungu ‘aliyeumba vitu vyote’?—Ufunuo 4:11.