Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kuiteteaje Imani Yangu Katika Uumbaji?

Ninaweza Kuiteteaje Imani Yangu Katika Uumbaji?

Vijana Huuliza . . .

Ninaweza Kuiteteaje Imani Yangu Katika Uumbaji?

“Suala la mageuzi lilipoanza kujadiliwa darasani lilikuwa tofauti na kila kitu nilichokuwa nimefundishwa. Lilifundishwa kama jambo hakika na hilo liliniogopesha.” —Ryan, 18.

“Nilikuwa na miaka 12 hivi, na mwalimu wangu alishikilia sana fundisho la mageuzi. Hata aliweka alama ya Darwin kwenye gari lake! Hilo lilinifanya nisite kuzungumza kwa uhuru kuhusu imani yangu katika uumbaji.”—Tyler, 19.

“Mwalimu wangu wa somo la elimu ya jamii aliposema kwamba tutazungumzia mageuzi katika somo ambalo lingefuata niliogopa sana. Nilijua kwamba itanibidi kuwaelezea wanafunzi wenzangu kuhusu msimamo wangu juu ya suala hilo lenye kubishaniwa.”—Raquel, 14.

LABDA kama vile Ryan, Tyler, na Raquel, wewe huingiwa na wasiwasi somo la mageuzi linapofundishwa darasani. Unaamini kwamba Mungu “aliumba vitu vyote.” (Ufunuo 4:11) Unaona uthibitisho wa kwamba vitu vyote viliumbwa na mbuni mwenye akili. Lakini vitabu vya mafunzo na vilevile walimu husema kwamba tulitokea kwa mageuzi. Wewe ni nani hata ushindane na “wataalamu”? Na wanafunzi wenzako watatendaje ukianza kuzungumza juu ya . . . Mungu?

Tulia, maswali kama hayo yasikubabaishe! Si wewe tu unayeamini uumbaji. Ukweli ni kwamba hata idadi kubwa ya wanasayansi hawakubaliani na nadharia ya mageuzi. Pia walimu wengi hawaiamini. Haidhuru vitabu vya mafunzo vinasema nini, wanafunzi 4 kati ya 5 huko Marekani wanaamini kwamba kuna Muumba!

Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Ninaweza kusema nini ili kutetea imani yangu katika uumbaji?’ Uwe na hakika kwamba ujapokuwa na woga, bado unaweza kueleza msimamo wako kwa uthabiti. Hata hivyo, utahitaji kujitayarisha.

Chunguza Yale Unayoamini!

Ikiwa umelelewa na wazazi Wakristo, huenda unaamini uumbaji kwa sababu tu umefundishwa hivyo. Lakini sasa una umri mkubwa na unataka kumwabudu Mungu kwa kutumia ‘nguvu zako za kufikiri,’ ukiwa na msingi thabiti wa yale unayoamini. (Waroma 12:1) Paulo aliwatia moyo Wakristo wa karne ya kwanza ‘wahakikishe mambo yote.’ (1 Wathesalonike 5:21) Unaweza kuthibitishaje imani yako katika uumbaji?

Kwanza ona kile ambacho Paulo aliandika kuhusu Mungu: “Sifa zake ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa.” (Waroma 1:20) Ukiwa na wazo hilo fikiria mwili wa binadamu, dunia, anga, na kina cha bahari. Chunguza ulimwengu wa ajabu wa wadudu, mimea, na wanyama au jambo lolote linalokuvutia. Halafu kwa kutumia “nguvu zako za kufikiri,” tafakari swali hili, ‘Ni nini kinachonithibitishia kwamba kuna Muumba?’

Ili kujibu swali hilo, Sam mwenye umri wa miaka 14 anatoa mfano wa mwili wa binadamu. Anasema kwamba mwili wa binadamu “umeumbwa vizuri na ni tata sana, sehemu zake zote zinafanya kazi pamoja vizuri. Mwili wa binadamu haungeweza kujitokeza kwa mageuzi!” Holly mwenye miaka 16, anakubaliana na hilo. Anasema, “tangu ilipogunduliwa kwamba nina kisukari, nimejifunza mengi kuhusu jinsi mwili unavyofanya kazi. Kwa mfano, inashangaza jinsi kongosho ambacho ni kiungo kidogo kinachopatikana sehemu ya nyuma ya tumbo kinavyofanya kazi kubwa ya kusaidia damu na viungo vingine kufanya kazi.”

Vijana wengine wana maoni tofauti kuhusu suala hilo. Jared mwenye miaka 19 anasema hivi, “kwangu uthibitisho wenye nguvu unahusiana na ukweli wa kwamba tuna hamu ya mambo ya kiroho, tunapendezwa na mambo yenye kuvutia na tuna tamaa ya kujifunza. Hatuhitaji sifa hizo ili tuendelee kuwa hai, kama wanamageuzi wanavyotaka tuamini. Ufafanuzi pekee ambao ninahisi unapatana na akili ni huu, kwamba tumewekwa hapa na mtu ambaye alitaka tufurahie uhai.” Tyler, aliyetajwa mwanzoni amekata kauli kama hiyo. “Ninapofikiria jinsi mimea inavyotegemeza uhai na pia jinsi ilivyoundwa kwa njia tata yenye kustaajabisha, ninasadikishwa kwamba kuna Muumba.”

Ni rahisi kutetea uumbaji ikiwa umetafakari fundisho hilo vizuri na kusadikishwa. Kwa hiyo, kama vile Sam, Holly, Jared, na Tyler, tumia wakati kufikiria vitu ambavyo Mungu ameumba. Kisha “sikiliza” yale ambayo vitu hivyo “vinakuambia.” Bila shaka utakata kauli ileile ambayo mtume Paulo aliikata, kwamba vitu hivyo vinathibitisha kuna Mungu na pia vinafunua sifa zake ambazo “zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa.” *

Fahamu Kile Ambacho Biblia Inafundisha Hasa

Ili utetee fundisho la uumbaji unapaswa kuchunguza vitu ambavyo Mungu ameumba na pia kufahamu kile ambacho Biblia inafundisha hasa kuhusiana na suala hilo. Hakuna sababu nzuri ya kubishana kuhusu mambo ambayo Biblia haitaji moja kwa moja. Fikiria mifano kadhaa.

Kitabu changu cha sayansi kinasema kwamba dunia na mfumo wa jua vimekuwapo kwa mabilioni ya miaka. Biblia haisemi chochote kuhusu muda ambao dunia au mfumo wa jua umekuwapo. Kwa hakika, kulingana na masimulizi ya Biblia huenda ulimwengu ulikuwapo mabilioni ya miaka kabla ya “siku” ya kwanza ya uumbaji kuanza.—Mwanzo 1:1, 2.

Mwalimu wangu anasema kwamba dunia haingeweza kuumbwa kwa siku sita tu. Biblia haisemi kwamba kila mojawapo ya “siku” sita za uumbaji ilikuwa na urefu wa saa 24. Kwa habari zaidi ona ukurasa wa 18-20 wa gazeti hili.

▪ Darasani tulizungumzia mifano kadhaa kuhusu jinsi wanyama na wanadamu wamebadilika kadiri ambavyo muda umepita. Biblia inasema kwamba Mungu aliumba kila kitu “kulingana na aina yake.” (Mwanzo 1:20, 21) Biblia haiungi mkono wazo la kwamba vitu hai vilitokana na vitu visivyo na uhai au kwamba Mungu alianzisha hatua za mageuzi kwa kuumba chembe moja tu. Hata hivyo, kila “aina” ina uwezo mkubwa wa kutokeza viumbe wenye sifa tofauti-tofauti. Hivyo masimulizi ya Biblia yanapatana na wazo la kwamba mabadiliko yanaweza kutokea katika kila “aina.”

Shikilia Imani Yako kwa Uhakika!

Huna sababu ya kuaibika kwa sababu unaamini uumbaji. Kwa kutegemea uthibitisho uliopo, ni jambo linalopatana kabisa na akili, naam la kisayansi, kusadiki kwamba tuliumbwa na mbuni mwenye akili. Kwa ujumla fundisho la mageuzi, wala si la uumbaji, ndilo linalomtaka mtu awe na imani kubwa isiyo na msingi na linalohitaji mtu aamini kwamba miujiza hutukia bila mfanya-miujiza. Bila shaka, baada ya kusoma makala mbalimbali za toleo hili la Amkeni! hapana shaka utasadikishwa kwamba uthibitisho unaunga mkono uumbaji. Na baada ya kufikiria jambo hilo kwa uzito ukitumia nguvu zako za kufikiri, utaweza kutetea imani yako kwa uhakika zaidi darasani.

Hilo ndilo jambo ambalo Raquel aliyetajwa mwanzoni aligundua. Anasema hivi: “Ilinichukua siku kadhaa kutambua kwamba ninapaswa kuwaeleza wengine mambo ninayoamini. Nilimpa mwalimu wangu kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? ambacho nilikuwa nimekiweka alama katika sehemu nilizotaka asome. Baadaye, aliniambia kwamba kitabu hicho kilimpa maoni mapya kabisa kuhusu mageuzi na kwamba wakati ujao atazingatia habari hiyo anapofundisha somo la mageuzi!”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Vijana wengi wamenufaika kwa kusoma habari iliyo katika vitabu kama vile Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? na Je, Kuna Muumba Anayekujali? Vitabu hivyo viwili vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Ni zipi baadhi ya njia rahisi unazoweza kueleza imani yako katika uumbaji unapokuwa shuleni?

▪ Unaweza kuonyeshaje uthamini wako kwa ajili ya Yule aliyeuumba vitu vyote?—Matendo 17:26, 27.

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

“KUNA UTHIBITISHO MWINGI SANA”

“Ungemwambia nini kijana aliyefundishwa tangu utotoni kwamba kuna Muumba lakini sasa anafundishwa mageuzi shuleni?” Mtaalamu wa mikrobiolojia ambaye ni Shahidi wa Yehova aliulizwa swali hilo. Alijibuje? “Unapaswa kuiona kuwa nafasi ya kujithibitishia kuwa kuna Mungu, si kwa sababu tu ulifundishwa hivyo na wazazi wako, bali kwa sababu umejichunguzia uthibitisho na kukata kauli yako mwenyewe. Nyakati nyingine walimu wanapoombwa ‘wathibitishe’ fundisho la mageuzi, wao hushindwa kufanya hivyo, nao hutambua kwamba wanaamini fundisho hilo kwa sababu tu wamefundishwa hivyo. Tunaweza kunaswa na mtego huohuo kuhusiana na imani ya kwamba kuna Muumba. Hiyo ndiyo sababu ni jambo muhimu sana ujithibitishie kwamba kweli kuna Mungu. Kuna uthibitisho mwingi sana. Si vigumu kuupata.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28]

NI NINI KINACHOKUSADIKISHA?

Andika hapa chini mambo matatu yanayokusadikishia kwamba kuna Muumba:

1. ․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

2. ․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

3. ․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․