Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unapaswa Kumwamini Nani?

Unapaswa Kumwamini Nani?

Unapaswa Kumwamini Nani?

“Bila shaka, kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.”—WAEBRANIA 3:4.

JE, UNAKUBALIANA na maneno hayo yanayopatana na akili ya mwandikaji wa Biblia? Mwanadamu amefanya maendeleo makubwa ya kisayansi katika muda wa miaka 2,000 hivi tangu maneno hayo yalipoandikwa. Je, bado kuna watu wanaofikiri kwamba ubuni unaoonekana katika vitu vya asili unapaswa kumchochea mtu kuamini kwamba kuna Mbuni, kuna Muumba, kuna Mungu?

Hata katika nchi zilizoendelea watu wengi wangesema ndiyo. Kwa mfano, huko Marekani, uchunguzi uliofanywa na Newsweek mnamo 2005 ulionyesha kwamba asilimia 80 ya watu “wanaamini kwamba Mungu aliumba ulimwengu.” Je, wana maoni hayo kwa kuwa hawana elimu? Kwa mfano, je, kuna wanasayansi wowote wanaoamini kwamba kuna Mungu? Katika mwaka wa 1997 jarida la kisayansi Nature liliripoti kwamba asilimia 40 kati ya wataalamu wa biolojia, fizikia, na hisabati walioombwa maoni, hawaamini tu kwamba kuna Mungu, bali pia Yeye husikiliza na kujibu sala.

Hata hivyo, wanasayansi wengine wanapinga kabisa imani hiyo. Hivi karibuni Dakt. Herbert A. Hauptman, mshindi wa Tuzo la Nobeli alisema katika warsha ya kisayansi kwamba kuamini nguvu zinazozidi zile za asili, hasa kuamini kuna Mungu hakupatani na mambo hakika ya kisayansi. Alisema kwamba “imani kama hiyo inaweza kuwadhuru wanadamu.” Hata wanasayansi wanaoamini kuna Mungu husita kufundisha kwamba ubuni unaoonekana katika mimea na wanyama ulitokezwa na Mbuni fulani. Kwa nini? Akitaja sababu moja, Douglas H. Erwin, mtaalamu wa biolojia ya mabaki ya kale ya wanyama na mimea katika Taasisi ya Smithsonia, alisema: “Kanuni moja ni kwamba sayansi haikubali eti miujiza hutokea.”

Je, ungependa kuwaacha wengine wakuambie kile utakachofikiri na kuamini? Au ungependa kujichunguzia baadhi ya uthibitisho na kukata kauli yako mwenyewe? Unaposoma habari kuhusu ugunduzi wa karibuni wa kisayansi katika kurasa zinazofuata, jiulize hivi, ‘Je, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba kuna Muumba?’

[Blabu katika ukurasa wa 3]

Jichunguzie uthibitisho

[Sanduku katika ukurasa wa 3]

Je, Mashahidi wa Yehova Ni Wanauumbaji?

Mashahidi wa Yehova wanaamini masimulizi ya uumbaji katika kitabu cha Mwanzo cha Biblia. Hata hivyo, imani ya Mashahidi wa Yehova kuhusu uumbaji inatofautiana na ya wale wanaoitwa eti wanauumbaji. Kwa nini? Wanauumbaji huamini kwamba vitu vyote viliumbwa katika kipindi cha siku sita zenye urefu wa saa 24 kila moja, miaka 10,000 hivi iliyopita. Hata hivyo, Biblia haifundishi hivyo. * Watu hao pia huamini mafundisho mengi yasiyoungwa mkono na Biblia. Mafundisho ya Mashahidi wa Yehova hutegemea tu Neno la Mungu.

Isitoshe, katika maeneo fulani, neno “wanauumbaji” huhusianishwa na vikundi ambavyo hushikilia pia imani nyingine kali za kidini na kujihusisha sana katika siasa. Vikundi hivyo hujaribu kuwashinikiza wanasiasa, mahakimu, na walimu wafuate sheria na mafundisho yanayopatana na imani yao kuhusu uumbaji.

Mashahidi wa Yehova hawajihusishi katika siasa. Wao hutambua kwamba serikali zina haki ya kutunga na kuhakikisha kwamba sheria zinafuatwa. (Waroma 13:1-7) Hata hivyo, wao huchukua kwa uzito maneno ya Yesu kwamba wao “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14-16) Wanapohubiri, wao huwatolea watu nafasi ya kujifunza manufaa ya kuishi kulingana na viwango vya Mungu. Lakini hawavunji msimamo wao wa Kikristo wa kutokuwamo kwa kuunga mkono jitihada za watu wenye imani kali za kidini ambao hujaribu kutunga sheria za kijamii za kuwalazimisha watu wafuate viwango vya Biblia.—Yohana 18:36.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Tafadhali ona makala “Maoni ya Biblia: Je, Sayansi Inapingana na Masimulizi ya Mwanzo?” iliyo kwenye ukurasa wa 18 wa gazeti hili.