Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Sawa Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa Ikiwa Mnapendana?

Je, Ni Sawa Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa Ikiwa Mnapendana?

Maoni ya Biblia

Je, Ni Sawa Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa Ikiwa Mnapendana?

KATIKA uchunguzi mmoja, asilimia 90 hivi ya matineja waliohojiwa hawakuona ubaya kufanya ngono kabla ya ndoa ikiwa watu wawili wanapendana. Maoni hayo mara nyingi huonekana na kuendelezwa katika vyombo vya habari. Kwa kawaida televisheni na sinema huonyesha ngono kuwa tokeo la kawaida la upendo wa kimahaba.

Bila shaka, wale wanaotaka kumpendeza Mungu hawatafuti mwongozo katika ulimwengu kwa kuwa wanatambua kwamba ulimwengu unadhihirisha kufikiri kwa mtawala wake, Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Pia wao hujihadhari wasiongozwe kikamili na hisia zao, kwa kuwa wanajua kwamba “moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yeremia 17:9) Badala ya hivyo, wenye hekima hutafuta mwongozo kutoka kwa Muumba na Neno lake lililoongozwa kwa roho.—Methali 3:5, 6; 2 Timotheo 3:16.

Ngono Ni Zawadi Kutoka kwa Mungu

“Kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu, kwa maana hushuka kutoka kwa Baba wa mianga ya mbinguni,” inasema Yakobo 1:17. Ngono katika mpango wa ndoa ni moja kati ya zawadi hizo zenye thamani. (Ruthu 1:9; 1 Wakorintho 7:2, 7) Tendo hilo huwawezesha wanadamu kuzaa, nalo huwezesha mume na mke kuwa na uhusiano wa karibu wa kimwili na kihisia katika njia nyororo na yenye kufurahisha. Mfalme Sulemani aliandika: ‘Shangilia pamoja na mke wa ujana wako, maziwa yake yakuleweshe nyakati zote.’—Methali 5:18, 19.

Ni wazi kwamba Yehova anataka tunufaike na kufurahia zawadi zake. Ili hilo liwezekane, ametupa sheria na kanuni bora zaidi zinazopaswa kutuongoza. (Zaburi 19:7, 8) Yehova ndiye “anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake.” (Isaya 48:17) Je, Baba yetu wa mbinguni, ambaye ndiye wonyesho halisi wa upendo, anaweza kutunyima kitu kizuri kwelikweli?—Zaburi 34:10; 37:4; 84:11; 1 Yohana 4:8.

Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa Si Upendo

Mwanamume na mwanamke wanapooana, wao huwa “mwili mmoja.” Watu wawili ambao hawajaoana wanapofanya ngono, ambao huitwa uasherati, wao pia huwa “mwili mmoja,” lakini huo ni mwili ambao Mungu huuona kuwa najisi. * Isitoshe, miungano kama hiyo si upendo. Kwa nini tunasema hivyo?—Marko 10:7-9; 1 Wakorintho 6:9, 10, 16.

Sababu moja ni kwamba uasherati ni ngono bila kuwajibika. Na licha ya kumfanya mtu asijiheshimu, uasherati unaweza kusababisha magonjwa, mimba isiyotakiwa, na maumivu ya kihisia. Zaidi ya yote, kufanya hivyo huvunja viwango vya uadilifu vya Mungu. Hivyo, uasherati unaonyesha kwamba mtu hajali sana au hajali kabisa hali njema na furaha ya sasa na ya wakati ujao ya mtu yule mwingine.

Kwa Mkristo, kufanya uasherati ni kuingilia haki za ndugu au dada yake wa kiroho. (1 Wathesalonike 4:3-6) Kwa mfano, watu wanaodai kuwa watumishi wa Mungu ambao hufanya ngono nje ya ndoa huingiza uchafu ndani ya kutaniko la Kikristo. (Waebrania 12:15, 16) Pia, wanamnyima yule wanayefanya ngono naye msimamo safi wa maadili, na ikiwa mtu yule mwingine ni mseja, wanamnyima uwezekano wa kuingia katika ndoa wakati ujao akiwa safi kiadili. Pia wanachafua sifa njema ya familia yao, na vilevile wanaikosea familia ya mtu wanayefanya ngono naye. Mwishowe, wanamdharau Mungu, ambaye wamemkosea kwa kuvunja sheria na viwango vyake vya uadilifu. (Zaburi 78:40, 41) Yehova ‘atalipiza adhabu’ kwa ajili ya matendo yote mabaya yanayofanywa na watu wasiotubu. (1 Wathesalonike 4:6) Basi, haishangazi kwamba Biblia inatuambia ‘tukimbie uasherati!’—1 Wakorintho 6:18.

Je, una mchumba na mnapanga kuoana? Basi kwa nini msitumie uchumba wenu kujenga msingi imara unaotegemea kuaminiana na kuheshimiana? Fikiria: Mwanamke anawezaje kumwamini mwanamume ambaye ameonyesha kwamba hawezi kujizuia? Na je, ni rahisi kwa mwanamume kuthamini na kuheshimu mwanamke ambaye hupuuza sheria ya Mungu ili kutosheleza hisia zake za kimahaba au kumpendeza mwanamume?

Pia, kumbuka kwamba wale ambao hukataa viwango vya Mungu vyenye upendo huvuna wanachopanda. (Wagalatia 6:7) Biblia inasema, “yeye aliye na mazoea ya kufanya uasherati anautendea dhambi mwili wake mwenyewe.” (1 Wakorintho 6:18; Methali 7:5-27) Ni kweli kwamba inawezekana kwa hisia mbaya kuondoka hatimaye kati ya wenzi wa ndoa ambao walifanya ngono kabla ya ndoa ikiwa wanatubu, wanajitahidi sana kurudisha uhusiano mzuri pamoja na Mungu, na kuimarisha uaminifu kati yao. Hata hivyo, mwenendo wao wa zamani huwaachia makovu. Wenzi fulani ambao sasa wameoana hujuta sana kwamba walifanya uasherati. Mara nyingine mume wake hujiuliza, ‘Je, matatizo yetu ya ndoa yanatokana na msingi mbaya wa ndoa yetu?’

Upendo wa Kweli Hauna Ubinafsi

Ingawa upendo wa kweli unaambatana na hisia za kimahaba, upendo wa kweli “haujiendeshi bila adabu,” wala “hautafuti faida zake wenyewe.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Badala yake, huangalia masilahi ya yule mtu mwingine na furaha yake ya milele. Upendo huo humchochea mwanamume na mwanamke waheshimiane, na kuishi kupatana na kanuni ya Mungu inayoruhusu ngono kati ya mume na mke tu.—Waebrania 13:4.

Hisia za kuaminiana na usalama ambazo hufanyiza ndoa iwe na furaha ya kweli ni muhimu hasa watoto wanapozaliwa kwani Mungu alikusudia kwamba watoto wakue katika mazingira yenye upendo, yasiyokuwa na vurugu, na yenye usalama. (Waefeso 6:1-4) Ni katika ndoa pekee ndiyo watu wanaweza kuwajibika kikweli kati yao. Mioyoni mwao na mara nyingi kupitia maneno, wao huapa kutunzana na kutegemezana kupitia hali nzuri na mbaya kwa muda wote wa maisha yao.—Waroma 7:2, 3.

Ngono kati ya mume na mke inaweza kuimarisha kifungo chao. Katika ndoa yenye furaha wenzi huona ngono kuwa yenye kufurahisha na yenye thamani zaidi, na bila kukifanya kifungo cha ndoa kuwa duni, kusumbua dhamiri, au kutomtii Muumba.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Mungu ana maoni gani kuhusu ngono kabla ya ndoa?—1 Wakorintho 6:9, 10.

▪ Kwa nini uasherati ni mbaya?—1 Wakorintho 6:18.

▪ Watu wawili wanaovutiana kimahaba wanawezaje kuonyeshana upendo wa kweli?—1 Wakorintho 13:4, 5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “uasherati” linahusisha mwenendo wowote wa kingono na mtu mwingine nje ya ndoa ambao unahusisha matumizi ya viungo vya uzazi, kutia ndani ngono ya kinywa.—Ona Amkeni! la Julai 22, 2004 (22/7/2004), ukurasa wa 12, na Mnara wa Mlinzi, la Februari 15, 2004 (15/2/2004), ukurasa wa 13, yaliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.