Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilikombolewa Kutokana na Taabu Zangu Zote

Nilikombolewa Kutokana na Taabu Zangu Zote

Nilikombolewa Kutokana na Taabu Zangu Zote

Simulizi la Jean-Claude François

Kwa sababu ya dhamiri yangu iliyozoezwa na Biblia, nilifungwa kwa miaka saba katika magereza zaidi ya kumi na mawili. licha ya kuteseka sana, ninaona kwamba nimebarikiwa. acheni nieleze.

NILIZALIWA Januari 9, 1937 (9/1/1937) huko Algiers, Algeria. Wakati huo Wafaransa walitawala Algeria na baba yangu alikuwa ofisa katika jeshi la Ufaransa. Kazi yake ilimpeleka Misri, Iraki, Lebanoni, na Siria na nyakati nyingine angeenda kwa miezi kadhaa na hivyo hakuwa na wakati wa kutosha kuwa na watoto wake watano.

Nilipenda shule na nilipata maksi za juu. Lakini nilihangaishwa na maswali kama vile, Kwa nini tunakufa, na kwa nini kuna uovu ikiwa Mungu ana nguvu zote naye ni mwema? Sikupata majibu yenye kuridhisha. Vilevile nilitamani kujua jinsi uhai ulivyotokea. Nadharia ya Darwin kuhusu mageuzi ndiyo maelezo yaliyoonekana kuwa yanapatana na akili, kwa hiyo baada ya muda nikaanza kuamini kwamba hakuna Mungu.

Mwishowe Napata Majibu!

Mnamo 1954 rafiki yangu anayeitwa Georges, ambaye alikuwa Shahidi wa Yehova, alinipa kijitabu Evolution Versus the New World. * Nilikisoma kwa hamu kubwa. Licha ya kufichua makosa katika nadharia ya mageuzi, kijitabu hicho kilifunua kwamba mabaki ya kale ya wanyama na mimea yanaunga mkono simulizi la Mwanzo, ambalo linasema kwamba Mungu aliumba kila kitu kilicho hai “kulingana na aina yake.” (Mwanzo 1:12, 25) Lakini swali langu kuhusu uovu liliendelea kunisumbua.

Georges alikuwa painia, au mtumishi wa wakati wote, na alitumia wakati wake mwingi kuwafundisha watu Biblia, kitabu ambacho sikuwa nimewahi kukisoma. Je, angejibu maswali yangu? Nilimtembelea kwenye nyumba yake ndogo ambako aliishi na mapainia wengine, na nikapata majibu ya kimaandiko ya mengi ya maswali yangu. Baada ya hapo niliendelea kujifunza Biblia kwa utaratibu huku nikiifurahia sana. Tangu wakati huo, sijachoka kuchimba ndani ya Neno la Mungu nikitafuta hazina zake zenye kuimarisha imani.—Methali 2:1-5.

Nilianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo iliyokuwa ikifanywa katika chumba cha chini ya ardhi kwenye hoteli iliyokuwa katikati ya jiji la Algiers. Mashahidi walinikaribisha kwa uchangamfu, na baada ya muda nikaanza kuhudhuria kwa kawaida. Tangazo lilipotolewa kuhusu mkutano ambao ungefanywa kwenye mtaa fulani, niliamua kwenda. Nilipofika, niligundua kwamba Mashahidi walikuwa wamekutana kwa ajili ya utumishi wa nyumba kwa nyumba. (Matendo 20:20) Hata hivyo, sikuondoka, na hivyo ndivyo nilivyoanza kuhubiri.

Mara ya tatu nilipoenda kuhubiri nilizungumza na wenye nyumba peke yangu. Kwenye nyumba moja sikuweza kupata andiko la Biblia ambalo nilikuwa nimenukuu. Mwenye nyumba aliniambia, “Kijana, wafundishe wengine utakapokuwa na uwezo wa kufanya hivyo.” Kisha akafunga mlango. Nikiwa nimevunjika moyo, niliketi kwenye benchi na kutafuta andiko hilo. Dakika chache baadaye nilipolipata, nilirudi na kumwonyesha.

Nilionyesha wakfu wangu kwa Mungu nilipobatizwa Machi 4, 1956 (4/3/1956). Miezi sita baadaye nilihitaji kufanya uamuzi mzito. Je, nifanye upainia wa kawaida, au nikubali kazi ya ualimu katika eneo la mashambani la Algeria na hivyo niwe na wakati mchache katika utumishi? Nilichagua upainia.

Baba yangu alighadhabishwa na uamuzi huo na akachukua kisu na kutisha kunidunga shingoni huku akiniamuru nirudi nyumbani kila jioni. Pia aliniambia kwamba nisitarajie tena kulishwa, hata ingawa nilikuwa nimeazimia kulipia gharama zangu zote. Hivyo, ningeondoka nyumbani asubuhi bila kula, nile pamoja na mapainia wengine wakati wa mchana, kisha nile tena jioni kabla ya kurudi nyumbani.

Kuepuka Mabomu na Kuhepa Risasi

Wakati huo, Algeria ilikuwa katikati ya vita vya kupigania uhuru kutoka kwa Ufaransa, na mabomu yalilipuliwa Algiers. Mwezi mmoja kulikuwa na milipuko zaidi ya 100. Mabomu yalitegwa ndani ya mabasi, vilabu vya pombe, na viwanja vya michezo. Kazi ya kuhubiri ilikuwa ngumu. Watu waliogopa kufungua milango, na mara nyingi kulikuwa na amri za kutotembea usiku, vitambulisho vilikaguliwa, na watu walipekuliwa.

Jumapili (Siku ya Yenga), Septemba 30, 1956 (30/9/1956), wakati mimi na mapainia wengine tulikuwa tukisafisha mahali petu pa mkutano, bomu lililipuka kwenye mkahawa uliokuwa juu yetu, nalo likaua na kuwalemaza watu wengi. Hakuna yeyote kati yetu tuliokuwa chumba cha chini aliyeumia. Mnamo Desemba (Mwezi wa 12) tulikuwa tukihubiri na dada mmoja kwenye barabara yenye shughuli nyingi wakati ambapo gari lilipita mbio likiwamiminia watu risasi kutoka kwenye madirisha yake yaliyokuwa wazi. Tulikimbia ndani ya mlango mmoja, nikamsukuma chini dada huyo kisha nikajitupa chini. Risasi ziliendelea kupita juu ya vichwa vyetu. Baada ya hilo, sote tulikuwa waangalifu zaidi tulipohubiri.

Nakataa Kubeba Silaha

Machi 1, 1957 (1/3/1957), niliitwa nitumikie jeshini. Kwa sababu dhamiri yangu haingeniruhusu kutumia silaha kupigana, nilisali ili nipate nguvu za kushughulika na wenye mamlaka. Pia nilisali kwamba niepuke mzozo na baba yangu. Nilitulia nilipoambiwa niripoti kwenye jiji la Lille, Ufaransa, mbali na nyumbani.

Siku sita baadaye nilifika kwenye Ngome ya Lille, iliyokuwa imejengwa katika karne ya 17 wakati wa Mfalme Louis wa 14. Kwa kutumia Biblia yangu, niliwaeleza maofisa wa jeshi msimamo wangu wa kutokuwamo, na wakanitupa gerezani. Asubuhi moja walinzi waliniburuta nje, wakanipekua, na kupata Biblia ndogo. Kisha walinifanya nilale kifudifudi kwenye barafu, wakatupa Biblia yangu kwenye barafu kando yangu, wakagandamiza upande wa nyuma wa bunduki kwenye kichwa changu, na kunifanya nilale hapo kwa nusu saa. Baadaye, nilifurahi walinzi hao waliponiachia Biblia, nayo ipo kwenye rafu yangu hadi leo. Hata hivyo, dhuluma niliyopata siku hiyo imenifanya niwe na matatizo ya tumbo kwa miaka mingi.

Siku kadhaa baadaye kamanda alinisomea barua aliyokuwa amepokea kutoka kwa baba yangu. Ilisema, “Mlazimisheni mpaka akubali. Ikiwezekana vunjeni ujasiri wake.” Kwa kuwa sikukubali, ofisa huyo alinitupa ndani ya seli yenye giza, ambako nililala kwenye ubao na kujifunika blanketi ndogo. Kwa kuwa hakukuwa na choo nilijisaidia kwenye kona moja ya seli hiyo. Singeweza kuoga, kupiga meno mswaki, au kusafisha chombo changu cha kulia. Majuma mawili baadaye nilipelekwa gereza la Fresne huko Paris.

Kwa miaka sita iliyofuata, nilifungwa mara nne katika magereza 14 tofauti. Wakati mmoja katika majira ya baridi kali, nilifungwa huko Fontevrault, makao ya watawa ya karne ya 12 katika Bonde la Loire, ambayo yalitumika kama gereza. Vitu vyangu vilitwaliwa nilipofika. Kwa kuwa nilisisitiza nirudishiwe Biblia yangu, walinzi walinitupa katika kifungo cha upweke kwa mwezi mzima. Nikiwa huko, nilipigwa na baridi kali hivi kwamba nikaanza kukohoa damu.

Nilihamishwa kwenye gereza la Château de Turquant, karibu na Saumur ambalo lilikuwa na hali nzuri zaidi. Huko wafungwa waliwafanyia mahakimu waliokuwa wamestaafu kazi za nyumbani. Ahmed Ben Bella, ambaye baadaye alikuja kuwa rais wa Jamhuri ya Algeria, alikuwa mmoja wa wafungwa. Kwa miezi kadhaa nilimhubiria. Wakati mmoja aliniambia hivi: “Wewe ni mwenyeji wa Algiers, nawe uko hapa kwa sababu ulikataa kuchukua silaha kupigana na Waalgeria.” Aliniheshimu kwa sababu ya msimamo wangu.

Naimarishwa Kupitia Majaribu Zaidi

Afya yangu ilizorota, nikaambiwa nina kifua kikuu na nikapelekwa kwenye hospitali ya wagonjwa wa muda mrefu kusini mwa Ufaransa, ambako nililazwa kwa miezi kadhaa. Daktari alipendekeza nifanyiwe upasuaji ili kuondoa pafu lililoathiriwa nami nikakubali, iwapo tu ‘ningejiepusha na damu.’ (Matendo 15:29) Akiwa amekasirika, daktari alikataa kunipasua. Kufikia kwa wakati huo, nilikuwa nimefungwa kwa miaka sita.

Nililazimika kutoka hospitali hiyo katikati ya majira ya baridi kali, bila kitu kingine isipokuwa nguo nilizokuwa nimevaa. Lakini kama vile Yehova alivyomtuma Onesiforo akamsaidie mtume Paulo, Yeye alinitumia msaidizi, Ndugu Adolphe Garatoni, ambaye aliniruhusu niishi naye na akawa “msaada wenye kunitia nguvu.” (Wakolosai 4:11; 2 Timotheo 1:16-18) Kwa msaada wake na ule wa daktari fulani kusini mwa Ufaransa, hatua kwa hatua afya yangu ikawa bora.

Wakati huo, nilihitaji pesa nyingi ili kulipia gharama zangu. Sikujua ningefanya nini. Kisha siku moja mgeni akaja. Akaniambia, “Mimi ni wakili. Rais wa Algeria, Bw. Ben Bella, amenituma nikupe hii.” Alinipa bahasha iliyokuwa na pesa nyingi kuliko zile nilizohitaji kulipia gharama zangu. Nilimshukuru Yehova, “Msikiaji wa sala,” kwa moyo wangu wote.—Zaburi 65:2.

Mapendeleo Mazuri na Mwenzi Mrembo

Niliachiliwa huru kutoka gerezani, nikaanza tena utumishi wa wakati wote. Katika kutaniko la Melun karibu Paris nilikutana na mjane mwenye miaka 35 anayeitwa Andrée Morel. Mume wake wa kwanza aliyekuwa shahidi alikufa kwa aksidenti ya gari. Tulifunga ndoa Septemba 26, 1964 (26/9/1964). Agosti 1, 1965 (1/8/1965) tulipata mgawo wa kuwa mapainia wa pekee. Ingawa Andrée hakuwa na afya nzuri, alifurahia utumishi wa wakati wote kwa miaka 28.

Mnamo 1967, niliwekwa kuwa mwangalizi wa mzunguko, mhudumu anayesafiri akitia moyo makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Tulitumikia eneo lililo kusini mwa Ufaransa kutoka Bordeaux hadi Monaco na pia Paris kwa mwaka mmoja. Kwa sababu ya afya yetu kazi ya kuzunguka haikuwa rahisi, lakini kwa msaada wa Yehova, tulitumikia ndugu zetu kwa miaka 20, hadi mwaka wa 1986, ambapo tena tulirudia upainia wa pekee.

Maisha Yangu Leo

Nina miaka 70 hivi na nimejifunza mara nyingi kwamba Yehova huwapa watumishi wake nguvu za kuvumilia majaribu kila mara. Bila shaka, baadhi ya nguvu hizo hutokana na kujifunza Neno lake ambalo mimi hujaribu kulisoma kila mwaka kutoka jalada hadi jalada.—Isaya 40:28-31; Waroma 15:4; 2 Timotheo 3:16.

Mimi na Andrée hutiwa moyo tunapoona watu wakiitikia habari njema na kujiweka wakfu kwa Yehova. Tumewaona wanafunzi wetu wa Biblia wakifanya hivyo na jambo hilo limetuletea furaha isiyo na kifani na yenye kudumu. Tukitafakari kuhusu maisha yetu tunahisi kana kwamba mtunga-zaburi alisema kwa niaba ya kila mmoja wetu: “Huyu mwenye kuteseka aliita, na Yehova mwenyewe akasikia. Na Yeye akamwokoa kutoka katika taabu zake zote.”—Zaburi 34:6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Katika gereza la Château de Turquant, karibu na Saumur

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na mke wangu 1967 na leo