Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza kushindaje zoea hili?

Ninaweza kushindaje zoea hili?

Vijana Huuliza . . .

Ninaweza kushindaje zoea hili?

“Nilianza kupiga punyeto nikiwa na umri wa miaka minane. Baadaye nilijifunza maoni ya Mungu kuhusu jambo hilo. Niliumia sana kila mara nilipopiga punyeto. ‘Mungu anawezaje kumpenda mtu kama mimi?’ Nilijiuliza. Nilikuwa na hakika kwamba sitaingia katika ulimwengu mpya wa Mungu.”—Luiz. *

HUENDA wewe ni mtumwa wa zoea la kupiga punyeto kama Luiz. Unajua Yehova atapendezwa nawe ukishinda zoea hilo na ukionyesha sifa ya kujiweza, ambayo ni tunda la roho takatifu ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23; 2 Petro 1:5, 6) Lakini mara kwa mara unashindwa kujizuia. Kila mara unaporudia tendo hilo, unakata kauli kwamba huwezi kamwe kubadilika wala kuishi kulingana na viwango vya uadilifu vya Mungu.

Hivyo hasa ndivyo kijana anayeitwa Pedro alivyojiona. “Niliporudia tendo hilo, nilijihisi vibaya sana,” anasema. “Nilihisi siwezi kamwe kulipia kosa langu. Ilikuwa vigumu kwangu kusali. Ningeanza sala kwa kusema: ‘Yehova, sijui kama utasikiliza sala hii, lakini . . .’” Kijana anayeitwa André alikuwa na mawazo hayohayo. “Nilijiona kuwa mnafiki sana,” anasema. “Ilinibidi kung’ang’ana kuamka asubuhi na kufanya shughuli zangu za kila siku. Ilikuwa vigumu kwangu kuhudhuria mikutano ya Kikristo au kuhubiri.”

Iwapo unahisi kama Luiz, Pedro, au André, jipe moyo. Wengine pia huhisi hivyo, na unaweza kupata msaada! Vijana wengi, na watu wazima pia, wamepambana sana na zoea la kupiga punyeto nao wamefaulu kulishinda. Wewe pia unaweza kufaulu. *

Kukabiliana na Hisia za Hatia

Kama ilivyotangulia kutajwa, wale walio na zoea la kupiga punyeto huhisi hatia. Bila shaka, ‘kuhuzunishwa kwa njia ya kimungu’ kunaweza kukuchochea ushinde zoea hilo. (2 Wakorintho 7:11) Lakini kulemewa na hisia za hatia kunaweza kuwa na matokeo mabaya. Kunaweza kukuvunja moyo sana kiasi cha kukata tamaa.—Methali 24:10.

Basi, jitahidi kuelewa vizuri jambo hilo. Kupiga punyeto ni mojawapo ya mambo machafu. Zoea hilo hukufanya uwe ‘mtumwa wa tamaa na raha za namna mbalimbali,’ na hukuchochea uwe na mtazamo unaoweza kufisidi akili yako. (Tito 3:3) Hata hivyo, kupiga punyeto si ukosefu mbaya wa maadili katika ngono kama uasherati. (Waefeso 4:19) Kwa hiyo, iwapo una zoea la kupiga punyeto, usikate kauli kwamba umefanya dhambi isiyosameheka. Ufunguo ni kupinga tamaa ya kufanya hivyo na kutokubali kamwe kushindwa!

Nyakati nyingine ni rahisi kushuka moyo unaporudia tena tendo hilo. Ukilirudia, zingatia moyoni maneno ya Methali 24:16: “Kwa maana huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, naye hakika atasimama; lakini waovu watakwazwa na msiba.” Kujikwaa hakumaanishi kwamba wewe ni mtu mwovu. Hivyo, usife moyo. Badala yake, chunguza mambo yaliyofanya urudie tendo hilo, kisha uyaepuke.

Badala ya kujilaumu kwa sababu ya zoea lako, tafakari upendo na rehema za Mungu. Mtunga-zaburi Daudi, ambaye pia alikumbwa na udhaifu, alisema hivi: “Kama vile baba anavyowaonyesha wanawe rehema, ndivyo ambavyo Yehova amewaonyesha rehema wale wanaomwogopa. Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:13, 14) Naam, Yehova hufikiria hali yetu ya kutokamilika naye yuko ‘tayari kutusamehe’ tunapokosea. (Zaburi 86:5) Kwa upande mwingine, yeye hutaka tujitahidi kufanya marekebisho.

Unaweza kuchukua hatua gani ili ushinde zoea hilo na usilirudie tena?

Faida ya Kumweleza Mwingine

Licha ya kwamba habari kuhusu ngono zinaenezwa waziwazi katika nchi kadhaa, ni vigumu kwa watu wengi kuongea kwa uzito na kwa heshima kuhusu ngono. Aibu inaweza kukuzuia usimtajie, hata mtu unayemwamini, kuhusu zoea lako. Mkristo mmoja aliyepambana na zoea la kupiga punyeto kwa miaka kadhaa alisema: “Laiti ningejipa ujasiri na kumweleza mtu fulani kuhusu jambo hilo nilipokuwa kijana! Hisia za hatia zilinilemea kwa miaka mingi, na hilo liliathiri sana uhusiano wangu na wengine, na hasa, pamoja na Yehova.”

Unaweza kuongea na nani? Mtu anayefaa zaidi ni yule aliyekomaa kiroho, hasa mzazi. Unaweza kuanza kwa kusema: “Ningependa kuzungumza nawe kuhusu tatizo linalonihangaisha sana?”

Mário aliamua kuongea na baba yake, aliyemwonyesha fadhili na kumwelewa sana. Hata alimweleza Mário kwamba yeye pia alipambana na zoea hilo alipokuwa kijana. “Unyoofu wa baba yangu ulinitia moyo sana,” Mário anasema. “Nilikata kauli kwamba ikiwa alishinda zoea hilo, mimi pia ninaweza kulishinda. Niliguswa sana na mtazamo wa baba yangu hivi kwamba nikalia machozi.”

André alijipa ujasiri na kuzungumza na mzee Mkristo, na anafurahi kuwa alifanya hivyo. * “Mzee huyo alipokuwa akinisikiliza, alilengwa-lengwa na machozi,” anasema André. “Nilipomaliza kumwelezea, alinihakikishia kwamba Yehova ananipenda. Aliniambia kwamba tatizo langu ni la kawaida. Aliahidi kufuatia maendeleo yangu na kuniletea habari zaidi kutoka katika vichapo vya kujifunzia Biblia. Baada ya kuzungumza naye, niliazimia kuendelea kupambana hata kama ningerudia tendo hilo tena.”

Kama Mário na André, wewe pia unaweza kupata msaada ili ushinde zoea la kupiga punyeto. Fuata ushauri ulio katika sanduku lenye kichwa, “Chukua hatua ya kupambana!” Naam, uwe na hakika kwamba unaweza kushinda zoea hilo!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 6 Ijapokuwa watu wanaotajwa katika makala hii ni wanaume, wanawake wengi wanapambana na zoea la kupiga punyeto. Hivyo, mashauri yanayotolewa hapa yanawahusu wanaume na wanawake. Pia, tambua kwamba makala hii inazungumzia zoea la kujipiga punyeto. Kumpiga punyeto mtu mwingine nje ya kifungo cha ndoa kunatiwa ndani ya kile ambacho Biblia inaita uasherati, ambayo ni dhambi nzito sana machoni pa Mungu.—Ona makala “Vijana Huuliza . . . Kuna Ubaya Gani Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa?” katika Amkeni! la Julai 22, 2004 (22/7/2004), ukurasa wa 12-14.

^ fu. 17 Huenda msichana akapendelea kuongea na mama yake au na dada aliye mkomavu kiroho kutanikoni.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Kwa nini ni muhimu kukumbuka kwamba Yehova yuko “tayari kusamehe”?—Zaburi 86:5.

▪ Utachukua hatua gani ili ushinde zoea la kupiga punyeto?

▪ Kwa nini hupaswi kuaibika kuomba msaada?

▪ Unaweza kuendeleaje kufikiria mambo yaliyo safi?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]

Kurudia Tendo Hilo Hakumaanishi Umeshindwa!

Jinsi ilivyo rahisi kuhisi hivi: ‘Nimeshindwa, hivyo afadhali niache kupambana.’ Pinga mtazamo huo. Hata kama umelirudia tendo hilo mara moja, au hata mara kadhaa, usikubali kushindwa.

Fikiria mfano huu: Tuseme unapanda ngazi, kisha uteleze na kurudi nyuma hatua moja au mbili, je,ungesema ‘itanibidi kushuka hadi chini na kuanza tena kupanda ngazi’? Bila shaka la! Mbona, basi, ukate kauli hiyo unapopambana na mazoea mabaya?

Kwa kawaida mtu huhisi hatia anaporudia zoea hilo. Huenda ukafanya hisia hizo zikulemee kwa kufikiri kwamba hufai, huna nguvu za kulishinda, na hustahili kutendewa jambo lolote jema. Usijiruhusu kuwa na hisia za hatia zinazopita kiasi kama hizo. Zitafyonza nguvu zako unazohitaji ili urudie tena pambano lako. Pia kumbuka hili: Mtu mkuu zaidi aliyetembea hapa duniani, yaani, Yesu Kristo, alikuja kuwakomboa watenda dhambi wala si watu wakamilifu. Hivyo, kwa sasa hakuna yeyote kati yetu anayeweza kutenda kwa ukamilifu.—Kutoka Amkeni! la Agosti 8, 1992 (8/8/1992), ukurasa wa 13.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]

Chukua Hatua ya Kupambana!

▪ Jilazimishe kufikiria mambo tofauti.—Wafilipi 4:8.

▪ Epuka kutazama mambo yanavyoweza kuchochea tamaa mbaya.—Zaburi 119:37.

▪ Omba “nguvu zinazopita zile za kawaida.”—2 Wakorintho 4:7.

▪ Uwe na mengi ya kufanya katika kazi za Kikristo.—1 Wakorintho 15:58.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]

Msaada Zaidi

Ukitaka kupata habari zaidi kuhusu jinsi ya kushinda zoea la kupiga punyeto, ona sura ya 25 na 26 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza . . . Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.