Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Pindi za Mlo Hutuwezesha Kukaribiana Zaidi”

“Pindi za Mlo Hutuwezesha Kukaribiana Zaidi”

“Pindi za Mlo Hutuwezesha Kukaribiana Zaidi”

JE, FAMILIA yenu hula pamoja angalau mara moja kwa siku? Inasikitisha kwamba, katika ulimwengu wa leo ulio na pilikapilika nyingi, watu katika familia nyingi hawali kwa mpango na kila mmoja hula peke yake. Hata hivyo, mbali na kutosheleza uhitaji wa kimwili, kula pamoja huwezesha familia kutosheleza mahitaji muhimu zaidi, yaani, kuwa na mawasiliano mazuri na uhusiano wa karibu zaidi.

Algirdas anaishi na mke wake anayeitwa Rima, na binti zao watatu huko Lithuania, kaskazini mwa Ulaya. “Ijapokuwa ninafanya kazi na binti zetu wanaenda shule,” anasema Algirdas, “sisi hupanga mambo ili tuweze kula chakula cha jioni pamoja. Tunapokuwa tukila, kila mmoja wetu huwa huru kuongea kuhusu jinsi siku ilivyokuwa na kueleza matatizo, mawazo, mipango, na mapendezi yake. Pia, sisi hutumia wakati huo kuzungumzia mambo ya kiroho. Bila shaka, pindi za mlo hutuwezesha kukaribiana zaidi.”

Rima anaongezea: “Kutayarisha chakula pamoja na binti zetu hutupa pia nafasi ya kuwa na mazungumzo ya ndani. Binti zetu hufurahia kufanya kazi pamoja jikoni na wakati huohuo wakijifunza kazi muhimu. Hivyo, tumefaulu kufanya kazi huku tukijifurahisha.”

Algirdas, Rima, na watoto wao wanapata manufaa tele kwa kuwa na pindi za kula pamoja. Ikiwa hufanyi hivyo, mbona usipange kula angalau mlo mmoja kila siku pamoja na familia yako, hata kama wewe ni mzazi usiye na mwenzi? Utapata thawabu nyingi sana ukijitahidi kufanya hivyo.