Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Alipenda Alichojifunza

Alipenda Alichojifunza

Alipenda Alichojifunza

MUDA mfupi uliopita barua fulani iliyokuwa imeandikwa na mwanamke mmoja kabla ya kifo chake ilipatikana. Alikufa mnamo Mei (Mwezi wa 5) 2004 kutokana na kansa. Hakuwa amemaliza kuandika barua hiyo, huenda kwa sababu ya kuzorota ghafula kwa afya yake. Hata hivyo, wale waliosoma barua hiyo ambayo haikuwa imetumwa waliguswa sana hivi kwamba wakalia, na imani yao katika Mungu ikaimarishwa.

Katika barua hiyo, mwandishi, anayeitwa Susan, alieleza kwamba alikuwa kijana alipompigia simu mzee Mkristo ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova huko Connecticut, Marekani. Alieleza hali aliyokabili alipokuwa kijana. Mwishoni mwa mwaka jana, mama ya Susan alipata barua hiyo yenye kugusa moyo sana na akatuma nakala moja kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko New York.

Susan aliandika kwamba alikuwa amepata namba ya simu ya mzee huyo aliyekuwa akiishi Connecticut katika kitabu cha simu mwaka wa 1973. Alieleza hivi: “Mwaka huo, nilipokuwa na umri wa miaka 14, ndipo nilipoamua kwamba huu ndio ukweli baada ya kusoma nakala za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kwa kuwa sikuwa nimewahi kukutana na Mashahidi wa Yehova, niliwatafuta katika kitabu cha simu na kuchagua namba ya eneo nilimokuwa nikiishi kati ya zile za Mashahidi wa Yehova. Ndugu Genrich alipojibu simu, alishangaa kusikia kwamba sijawahi kukutana na Mashahidi.” *

Tatizo Kubwa

Susan alieleza katika barua yake kwamba alipokuwa na miaka kumi, alipelekwa akaishi na dada ya mama yake huko Connecticut. Alipaswa kukaa huko kwa muda mfupi, lakini baada ya muda Susan akamwambia mama yake, aliyekuwa akiishi peke yake huko Florida, kwamba angependa kuendelea kukaa Connecticut. Katika barua yake Susan aliandika kwamba hali yake ilifanana na kile “kinachoitwa tabia isiyo ya kawaida ya Stockholm, yaani, mtu kufanya urafiki na watu wanaomnyanyasa.” * Aliteswa vibaya sana.

Susan aliandika hivi: “Shangazi yangu na mwenzi wake walinitesa sana. Isitoshe, ni watu wachache sana ambao waliwahi kututembelea. Niliporuhusiwa kwenda shuleni, sikupewa chakula cha mchana wala nguo nadhifu, hata ingawa Mama alikuwa akituma pesa nyingi za kunitunza. Nilikuwa tu na nguo moja ya ndani, ilhali binti wawili wa shangazi, waliokuwa na umri mdogo kuliko mimi, walikuwa na kila kitu.” Alieleza mambo hayo ili iwe wazi kwa nini alijua angepata matatizo iwapo shangazi yake angegundua kwamba alipendezwa kujifunza mengi kuhusu Biblia.

Jinsi Ujuzi wa Biblia wa Susan Ulivyoongezeka

Susan aliandika hivi: “Ndugu Genrich alinijulisha kwa Laura, dada Mkristo mkomavu, naye alitumia wakati mwingi kujibu maswali yangu mengi ya Biblia na mara nyingi tulikutana kwenye duka la kufulia nguo.” Susan anaeleza kwamba kufikia wakati huo hakuwa amefanya uamuzi wowote, lakini baada ya mazungumzo yake pamoja na Laura na kusoma vichapo vinavyotegemea Biblia kama vile kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, alifanya uamuzi.

Susan aliendelea kuandika hivi: “Ilikuwa Ijumaa usiku nilipomwambia shangazi kwamba nilikuwa nikizungumza na Mashahidi. Shangazi alinipa adhabu ya kusimama jikoni usiku kucha bila kulala. Hilo lilinifanya niazimie hata zaidi kuwa Shahidi.”

Kuanzia wakati huo, Ndugu Genrich alimpelekea Susan vichapo kwa kawaida ili kumsaidia kuielewa Biblia. Susan anaeleza, “Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1974 (cha Kiingereza) ndicho ninachokumbuka vizuri zaidi kwa sababu kilieleza jinsi ambavyo Mashahidi katika Ujerumani ya Nazi walivumilia mnyanyaso kabla na wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. . . . Wakati huo ndipo nilipomwomba mzee huyo anirekodie nyimbo za Ufalme ili nijifunze kuziimba. Baada ya mwaka mmoja nilikuwa naweza kuimba nyimbo zote 119 za kitabu cha nyimbo kilichotolewa mwaka wa 1966, ‘Kuimba na Kufuatana Wenyewe kwa Muziki Katika Mioyo Yenu.’”

“Wakati huohuo Ndugu Genrich alinipa kanda za hotuba za Biblia, drama, na programu za kusanyiko. Angeacha kanda hizo kwenye Barabara ya 10 karibu na mlingoti wa simu, na ningezichukua hapo. . . . Hali yangu ikaanza kunihuzunisha kwani nilikuwa nimefanya maendeleo makubwa bila kuhudhuria mkutano hata mmoja. Kwa hiyo nikaishiwa nguvu za kuendelea kuvumilia.”

Susan anasema kuwa miaka iliyofuata ilikuwa migumu sana. Alikuwa ameacha kuwasiliana na wale Mashahidi wawili tu aliokuwa anawajua. Hata hivyo, anasema kwamba “kujifunza nyimbo hizo zote kulikuwa kama ‘laana.’” Kwa nini? “Kwa kuwa ningekumbuka maneno ya wimbo fulani, kama vile, ‘Askari za Yah ni wa kujikaza.’ Nilijua kwamba maneno hayo yalikuwa yameandikwa na Shahidi fulani alipokuwa kwenye kambi ya mateso ya Wajerumani wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu na hilo lilinihuzunisha zaidi. Nilijiona kuwa mwoga na nilifikiri kuwa Yehova ameniacha.” *

Hatimaye Uhuru

“Mambo yalibadilika siku ambayo nilitimiza umri wa miaka 18. Hakuna Shahidi ambaye aligonga mlango wetu kwa miaka mingi kwa kuwa tulikuwa tumeorodheshwa miongoni mwa ‘nyumba ambazo hazipaswi kuhubiriwa.’ Lakini siku hiyo mtu kutoka kutaniko lingine alitembelea nyumba yetu nami nilizungumza naye kwani hakukuwa na mtu mwingine nyumbani. Ninafikiri hiyo ndiyo mara ya kwanza kuwa nyumbani peke yangu siku ya Jumamosi. Niliona hilo kuwa uthibitisho kwamba Yehova hakuwa ameniacha. Kwa hiyo, nilimpigia simu Ndugu Genrich ambaye nilikuwa nimezungumza naye hapo awali, nikamwambia kwamba niko tayari kuhama nyumba hiyo na nikamwuliza ikiwa alikuwa na mapendekezo yoyote. Mwishowe nilisaidiwa kuhama.”

Mnamo Aprili (Mwezi wa 4) 1977 Susan alihamia mahali pengine. Barua yake ilisema hivi: “Mwaka uliofuata nilihudhuria mikutano na makusanyiko yote na nikaanza kuhubiri. Niliwasiliana tena na mama yangu. Kwa miaka hiyo yote hakujua jinsi nilivyokuwa nimeteswa vibaya sana, kwa hiyo alishangaa sana. Mara moja akaanza kunisaidia na kuhakikisha kwamba nilikuwa na kila kitu ninachohitaji. Mama alikuwa amehamia Alaska miaka michache kabla ya hapo. Kwa kuwa alipendezwa sana na kujifunza Biblia nikajiunga naye huko Alaska mnamo 1978. Baadaye akawa Shahidi na amedumu akiwa mwaminifu hadi leo.

“Nilipoanza kuhudhuria mikutano, Ndugu Genrich alipanga kwamba kikundi fulani kitembelee makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, naye akanikaribisha niandamane na kikundi hicho. Hiyo ni moja kati ya zawadi bora ambazo nimewahi kupewa, kwa kuwa tangu wakati huo nimethamini sana tengenezo la Yehova. Acheni nimalizie hapo. Sikuandika mambo yote kwa kuwa nilitaka kumaliza barua hii kwa wakati.”

Tumenukuu maneno machache tu kutoka katika barua yenye kurasa sita na nusu. Karibu na mwisho wa barua yake, Susan aliandika hivi: “Mwezi uliopita nikiwa hospitalini nilizidiwa sana hivi kwamba nilifikiri nitakufa . . . Nilimwomba Yehova kwamba kama tu ningeishi kwa majuma mawili nikiwa na afya nzuri, ningekamilisha mambo fulani. . . . Sitazamii kwamba nitaendelea kuishi kwa muda mrefu zaidi lakini lazima niseme kwamba miaka hii ambayo nimekuwa katika kweli imekuwa yenye kupendeza sana. Nimepata maisha bora ambayo kila mtu angependa kuwa nayo.”

Hakuandika maneno ya kumalizia wala kutia sahihi, na barua yake haikuwahi kutumwa. Walioipata hawakujua ni nani aliyepaswa kutumiwa barua hiyo. Lakini, kama ilivyotajwa awali, mwishowe mama ya Susan alipewa barua hiyo.

Habari Zaidi Kuhusu Susan

Susan alipobatizwa Aprili 14, 1979 (14/4/1979), mama yake alirudi Florida. Susan alibaki Alaska kwa kuwa alikuwa na marafiki wa karibu katika Kutaniko la North Pole. Muda mfupi baada ya hapo akawa mtumishi wa wakati wote akitumikia kama painia. Mwishowe, alihamia Florida na mnamo 1991, akaolewa na mzee Mkristo ambaye pia alikuwa painia, lakini akafa muda mfupi baada ya Susan kufa.

Susan na mume wake walipendwa sana, nao walishiriki katika utumishi wa wakati wote pamoja hadi ugonjwa wake ulipowalazimu kuacha. Kwa ujumla alikuwa mtumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 20. Kutaniko la North Pole lilisikiliza hotuba ya mazishi yake kwa njia ya simu kutoka Florida.

Barua ya Susan inaweza kutusaidia tuthamini hata zaidi baraka za kiroho ambazo wale wanaomtumikia Yehova hufurahia na kutupa tumaini zuri la ufufuo. (Matendo 24:15) Simulizi hilo la maisha linaonyesha wazi kwamba Mungu yuko karibu na wote wanaomkaribia!—Yakobo 4:7, 8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ndugu Genrich na mke wake walikufa katika aksidenti mbaya mnamo 1993.

^ fu. 6 Ona Amkeni! la Desemba 22, 1999, ukurasa wa 7.

^ fu. 13 Wimbo Na. 29, “Haya Mbele, Enyi Mashahidi!” katika kitabu Mwimbieni Yehova Sifa.

[Blabu katika ukurasa wa 23]

“Miaka hii ambayo nimekuwa katika kweli imekuwa yenye kupendeza sana. Nimepata maisha bora ambayo kila mtu angependa kuwa nayo”

[Picha katika ukurasa wa 21]

Susan alipokuwa na umri wa miaka kumi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Susan akiwa na mume wake, James Seymour