Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Yesu Ni Mtu Muhimu Sana?

Kwa Nini Yesu Ni Mtu Muhimu Sana?

Kwa Nini Yesu Ni Mtu Muhimu Sana?

KWA miaka 2,000 sasa, watu wamekazia fikira kuzaliwa kwa Yesu. Kulingana na Luka, tabibu wa karne ya kwanza, bikira fulani kijana aliyeitwa Maria aliambiwa hivi na malaika: “Tazama! utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu.” Malaika huyo alisema nini kuhusu Yesu? “Huyo atakuwa mkuu naye ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi . . . Naye [Yesu] atatawala akiwa mfalme,” na “ufalme wake hautakuwa na mwisho.”—Luka 1:31-33.

Kwa kweli, hilo ndilo jambo ambalo wanadamu wanahitaji, mtawala wa ulimwengu mwenye uadilifu ambaye atasimamia mambo ya dunia kwa upendo! Muda mrefu kabla Yesu hajazaliwa, Biblia ilitabiri: “Kwetu mtoto amezaliwa, tumepewa mwana, na serikali itakuwa juu ya mabega yake. Naye ataitwa . . . Baba wa Milele, Mkuu wa Amani. Kuongezeka kwa serikali yake na amani hakutakuwa na mwisho.”—Isaya 9:6, 7, New International Version.

Serikali yenye uadilifu na amani—hayo ni mataraja mazuri kama nini! Lakini ona kwamba serikali hiyo ilitabiriwa kuwa juu ya mabega ya mwana wa mfalme—“Mkuu wa Amani”—ikionyesha kwamba Mfalme mkuu, yaani Mungu Mweza-Yote, anamkabidhi Mwana Wake ufalme huo. Kwa hiyo, tena na tena Yesu alisema serikali hiyo ambayo angetawala ingeitwa “ufalme wa Mungu.”—Luka 9:27, 60, 62.

Mapema katika huduma yake Yesu alisema: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Vilevile Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali Ufalme wa Mungu uje. (Mathayo 6:9, 10) Jarida Christianity and Crisis linasema kwamba “Ufalme ulikuwa jambo kuu la mafundisho ya [Yesu],” kisha linaongeza: “Hakuna habari nyingine ambayo alikazia fikira zaidi au iliyokuwa kiini cha ujumbe wake. Unatajwa zaidi ya mara 100 katika masimulizi ya Injili.”

Maswali ya Kufikiria

Wewe unamwonaje Yesu leo? Mara nyingi wakati huu wa mwaka, yeye huonyeshwa kuwa mtoto katika hori. Na ni kweli kwamba kwa muda alikuwa mtoto asiyejiweza. (Luka 2:15-20) Lakini je, hivyo ndivyo tunavyopaswa kumkumbuka? Fikiria, Kwa nini Yesu alizaliwa akiwa mwanadamu? Kwa kweli, alikuwa nani?

Kitabu Encarta Yearbook cha mwaka wa 1996 kiliuliza, “Je, Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, Masihi aliyeahidiwa katika Biblia ya Kiebrania? Au alikuwa mwanadamu tu wa ajabu?” Maswali kama hayo yanahitaji kufikiriwa kwa uzito. Kwa nini? Kwa kuwa maisha na furaha yetu yanategemea maoni yetu kumhusu Yesu na jinsi tunavyotenda kumwelekea. “Yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele,” Biblia inasema, lakini “yule asiyemtii Mwana hataona uzima.”—Yohana 3:36.

Hakuwa Mtu wa Kawaida

Baada ya kufafanua mambo ambayo Yesu alifanya alipokuwa katika hekalu la Yerusalemu akiwa na umri wa miaka 12, Biblia inasema kwamba alirudi nyumbani na Maria na mume wake, Yosefu, “naye [Yesu] akaendelea kujitiisha kwao.” (Luka 2:51, 52) Lakini Yesu alipokua, ilidhihirika kwamba hakuwa mtu wa kawaida.

Yesu alipotuliza bahari iliyochafuliwa na dhoruba, rafiki yake mmoja aliyekuwa ameshikwa na woga alisema: “Kwa kweli huyu ni nani?” (Marko 4:41) Mwishowe, Yesu alipelekwa kwa Gavana Mroma Pontio Pilato kwa mashtaka ya uwongo. Akiwa na uhakika kwamba Yesu hakuwa na hatia na akiwa amevutiwa na hadhi ya Yesu alipotendwa kwa ukatili na isivyo haki, Pilato alimleta mbele ya umati, akisema hivi kwa mshangao: “Tazameni! Mwanamume!” Lakini Wayahudi walijibu: “Sisi tuna sheria, na kulingana na sheria anapaswa kufa, kwa sababu alijifanya mwenyewe kuwa mwana wa Mungu.”—Yohana 19:4-7.

Aliposikia Yesu akiitwa “mwana wa Mungu,” Pilato aliogopa. Mapema alikuwa amesikia ndoto ya mke wake kumhusu Yesu, ambaye mke wake alimwita “mtu huyo mwadilifu.” (Mathayo 27:19) Kwa hiyo, Pilato alijiuliza Yesu alikuwa nani kwa kweli! Ingawa alijua kwamba Yesu alitoka Galilaya, Pilato aliuliza: “Wewe ni mtu wa kutoka wapi?” Yesu alipokataa kujibu, mazungumzo yakaishia hapo.—Yohana 19:9, 10.

Ni wazi kwamba Yesu alikuwa mwanadamu, lakini hakuwa kama wanadamu wengine kwani hapo zamani alikuwa mtu wa kiroho, aliyejulikana mbinguni kama Neno. Kisha, kwa muujiza, uhai wake ukahamishwa hadi kwenye tumbo la uzazi la Maria. Mtume Yohana aliandika: “Neno akawa mwili, akakaa katikati yetu.”—Yohana 1:1, 2, 14, 18; Ufunuo 3:14.

Kwa Nini Ilikuwa Muhimu Mungu Amtume Mwana Wake?

Kabla hajapata watoto mwanadamu wa kwanza, Adamu, alifanya dhambi. Malaika mwasi ambaye alikuja kuitwa Ibilisi na Shetani alifaulu kumfanya asimtii Mungu. Basi Adamu hakuwa tena mwana wa Mungu kama vile Mungu alivyosema ingetukia iwapo angekosa kumtii. Hivyo Adamu akapatwa na matokeo ya dhambi yake. Alipoteza ukamilifu, akazeeka, na mwishowe akafa.—Mwanzo 2:15-17; 3:17-19; Ufunuo 12:9.

Ikifafanua matokeo ambayo sisi sote tulio wazao wake hupata kutokana na kutotii kwa Adamu, Biblia inaeleza hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Kwa kusikitisha sisi sote tulirithi dhambi kutoka kwa babu yetu Adamu, pamoja na madhara yanayotokana nayo, yaani, kuzeeka na kufa.—Ayubu 14:4; Waroma 3:23.

Madhara hayo yangeweza kuondolewa tu ikiwa tungekuwa na baba mkamilifu, ambaye hakuwa amerithi dhambi wala madhara yake yenye kuogofya. Fikiria jinsi ambavyo baba huyo mpya anayelingana na Adamu mkamilifu alivyoandaliwa.

Aliyehitajika Aandaliwa

Kama unavyokumbuka, “Mkuu wa Amani” aliyeahidiwa pia anaitwa “Baba wa Milele.” (NIV) Kuzaliwa kwake akiwa mwanadamu kulitabiriwa hivi: “Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto mwanamume.” (Isaya 7:14; Mathayo 1:20-23, Union Version) Yesu hakuwa na baba wa kibinadamu kama tu Adamu yule mwanadamu wa kwanza. Akifuatilia ukoo wa Yesu kwa kurudi nyuma hadi mwanzo wa historia ya wanadamu, mwanahistoria wa Biblia, Luka, anaonyesha kwamba Adamu aliumbwa akiwa “mwana wa Mungu.” (Luka 3:38) Lakini kama tulivyoona, Adamu alipoteza uhusiano wa kuwa mwana wa Mungu kwa ajili yake na wazao wake wote. Kwa hiyo, sote tunahitaji baba mkamilifu kama Adamu alivyokuwa alipoumbwa.

Mungu alimtuma Mwana wake kutoka mbinguni ili awe Adamu mpya badala ya yule wa kwanza. Biblia inasema hivi: “‘Mtu wa kwanza Adamu akawa nafsi hai.’ Adamu wa mwisho akawa roho inayotoa uhai. Mtu wa kwanza ni wa kutoka duniani na amefanywa kwa mavumbi; mtu wa pili ni wa kutoka mbinguni.” (1 Wakorintho 15:45, 47) Yesu, “Adamu wa mwisho,” ni kama “mtu wa kwanza Adamu” katika maana ya kwamba Yeye alikuwa mkamilifu, akiwa na uwezo wa kuzaa watoto wakamilifu, ambao wangeweza kuishi duniani milele wakiwa wakamilifu.—Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4.

Yesu, ambaye hakuzaa watoto, alidumisha uaminifu kwa Mungu licha ya mashambulio mbalimbali kutoka kwa Shetani. Uhai mkamilifu wa kibinadamu ambao Yesu alitoa baada ya kudumisha utimilifu uliitwa fidia. Biblia inaeleza hivi: “Kwa njia yake tuna kuachiliwa huru [kutoka kwa dhambi na kifo tuliyorithi kutoka kwa Adamu] kwa njia ya fidia kupitia damu ya [Yesu].” Pia inasema hivi: “Kama vile kupitia kutotii kwa [Adamu] wengi walifanywa watenda-dhambi, vivyo hivyo pia kupitia kutii kwa [Yesu] wengi watafanywa kuwa waadilifu.”—Waefeso 1:7; Waroma 5:18, 19; Mathayo 20:28.

Tukimwamini Yesu atakuwa kwetu “Baba wa Milele” na “Mwokozi.” Atatawala akiwa mkuu kwa njia nzuri ajabu akitumika kama Mtawala wa Ufalme wa Baba yake. Acheni tuchunguze jinsi maisha yatakavyokuwa chini ya utawala huo na wakati ambapo tutafurahia baraka hizo nzuri.—Luka 2:8-11.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Unamwonaje Yesu leo?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Kwa nini Yesu anaitwa “Adamu wa mwisho”?