Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maisha Anayotuwezesha Kupata

Maisha Anayotuwezesha Kupata

Maisha Anayotuwezesha Kupata

“TAZAMA! Mfalme atatawala kwa ajili ya uadilifu.” Biblia ina ahadi nyingi kama hiyo zenye kutia moyo kuhusu utawala wa Yesu. Ahadi nyingine kama hiyo inasema: “Atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini. . . . Damu yao itakuwa na thamani machoni pake.”—Isaya 32:1; Zaburi 72:12-14.

Je, mtu yeyote anaweza kukataa kwamba wanadamu ulimwenguni pote wanahitaji utawala kama huo wenye uadilifu? Yesu aliwahimiza wafuasi wake wazingatie Ufalme wa Mungu. Aliwafundisha kusali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.

Uthibitisho Kwamba Ufalme wa Mungu Umekaribia

Tunaweza kujuaje wakati ambapo Ufalme huo utakuja ili kujibu sala hiyo? Wafuasi wa mapema wa Yesu walitaka kujua jambo hilo, kwa hiyo wakauliza: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako [kama Mfalme anayetawala] na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Yesu alijibu hivi: “Taifa litasimama kupigana na taifa . . . , kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya nchi mahali pamoja baada ya pengine. Mambo yote hayo ni mwanzo wa maumivu ya taabu.” Pia akaonya: “Kwa sababu ya kuongezeka kwa uasi-sheria upendo wa walio wengi zaidi utapoa.”—Mathayo 24:3-12.

Unabii mwingine wa Biblia unasema kwamba “katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake.”—2 Timotheo 3:1-5.

Huenda ukakubali kwamba ufafanuzi huo kuhusu “siku za mwisho” unalingana kabisa na siku zetu. Kuna uthibitisho mwingi kwamba sasa ndio wakati wa kutimia kwa unabii huu wa Biblia: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Danieli 2:44.

Kupitia Ufalme huo “Mkuu wa Amani” ataondoa kila kitu kitakachoharibu amani ya wale watakaokuwa wameokoka mwisho wa ulimwengu huu. (Isaya 9:6) Unabii wa Biblia unaahidi hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17) Mwisho wa ulimwengu huu utawapa wale wanaofanya mapenzi ya Mungu nafasi ya kufurahia kile ambacho wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walipotezea familia ya kibinadamu walipomwasi Mungu.

Maisha Tunayotazamia Karibuni

Yesu alieleza hivi: ‘Katika uumbaji-mpya Mwana wa binadamu ataketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu.’ (Mathayo 19:28) Huo “uumbaji-mpya” ni nini? Tafsiri nyingine inasema “mambo yote yanapofanywa upya.” (New International Version) Simulizi la Biblia linalopatana na hilo linauita “mfumo wa mambo unaokuja.” (Luka 18:30) Wakati huo Yesu atatumia mamlaka aliyopewa na Mungu akiwa Mkuu wa Amani kuwapa uzima wa milele wote wanaoamini dhabihu yake ya fidia.—Yohana 5:21.

Katika mfumo mpya wa Mungu, watu watafurahia maisha ambayo Mungu aliwapa Adamu na Hawa alipowaweka katika Paradiso duniani. Kumbuka kwamba Mungu alikuwa amewaagiza wazae watoto, naam, ‘waijaze dunia na kuitiisha.’ Mgawo wao ulikuwa kupanua Paradiso ya Edeni ienee duniani pote! (Mwanzo 1:28) Vilevile, katika uumbaji-mpya dunia itajawa na wale watakaookoka mwisho wa ulimwengu huu, watoto wao, na wale ambao wamekufa na kufufuliwa. Mgawo wao utakuwa kushiriki kuifanya dunia iwe paradiso, kama Mungu alivyokusudia mwanzoni.

Fikiria baraka fulani ambazo Biblia inaonyesha watu katika ulimwengu huo mpya wenye uadilifu watafurahia.—2 Petro 3:13.

Huenda ahadi zinazoelezwa katika kurasa hizi zikaonekana kuwa ndoto tu, lakini kwa hakika zitatimizwa katika “mfumo wa mambo unaokuja.” Alipokuwa akisali kwa Mungu, Yesu alieleza kinachohitajika ili kufurahia baraka hizo aliposema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Na uwe miongoni mwa wale wanaotafuta kwa unyenyekevu ujuzi huo unaoongoza kwenye uzima.

[Blabu katika ukurasa wa 7]

“Ataitwa jina . . . Mkuu wa Amani. Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani.”—Isaya 9:6, 7

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Makao na Kazi kwa Ajili ya Kila Mtu

“Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake . . . Hawatapanda na mtu mwingine ale.”—Isaya 65:21, 22.

Chakula Kingi kwa Ajili ya Wote

“Hakika dunia itatoa mazao yake.” “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani.” —Zaburi 67:6; 72:16.

Wanyama Watafurahia Amani Ulimwenguni

“Mbwa-mwitu kwa kweli atakaa pamoja na mwana-kondoo kwa muda fulani, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi, . . . na mvulana mdogo atakuwa kiongozi juu yao.” —Isaya 11:6.

Vita Vimekomeshwa, Amani Milele

“Taifa halitainua upanga juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.” “Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani.”—Isaya 2:4; 9:7.

Wapendwa Waliokufa Wafufuliwa

“Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake [Yesu] na kutoka.” —Yohana 5:28, 29.

Hakuna Tena Magonjwa Wala Kifo

“Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” “Kifo hakitakuwapo tena . . . Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” —Isaya 33:24; Ufunuo 21:3, 4.