Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilikuwa Mwana Mpotevu

Nilikuwa Mwana Mpotevu

Nilikuwa Mwana Mpotevu

SIMULIZI LA MEROS WILLIAM SUNDAY

Tangu utotoni nilifunzwa kumpenda Mungu; lakini nilipokuwa na umri wa miaka 18, niliasi na kuondoka nyumbani. Kwa miaka 13 niliishi kama yule mwana mpotevu katika mfano wa Yesu. (Luka 15:11-24) Nilikuwa mlanguzi wa dawa za kulevya na karibu niharibu maisha yangu. Hebu niwaeleze kilichonifanya nibadili maisha yangu na jinsi nilivyorudi.

NILIZALIWA mnamo 1956 na wazazi Wakristo, nikiwa wa pili kati ya watoto tisa. Tuliishi Ilesha, mji ulio kusini-magharibi mwa Nigeria. Baba yangu alikuwa amelelewa na wazazi Wakatoliki, lakini mnamo 1945 mjomba wake akampa kitabu The Harp of God. * Baada ya kukisoma, Baba aliwatafuta Mashahidi wa Yehova. Mnamo 1946 alibatizwa, naye Mama akabatizwa muda mfupi baadaye.

Bado ninakumbuka jinsi Yehova alivyokuwa halisi kwangu nilipokuwa mvulana na jinsi nilivyoshiriki kwa bidii katika kuhubiri pamoja na wazazi wangu. Baba alijifunza Biblia pamoja nami. Mara kwa mara, Alice Obarah, ambaye mume wake alikuwa mwangalizi asafiriye katika eneo letu, alijifunza pamoja nami vilevile. Wazazi wangu walitaka niwe mtumishi wa wakati wote. Hata hivyo, Mama alipendekeza kwamba nipate elimu ya sekondari kwanza.

Punde tu baada ya kuanza, ingawa nilikuwa na umri wa miaka 16, nilifanya urafiki na wanafunzi ambao hawakuheshimu kanuni za Biblia. Hilo lilikuwa kosa la kijinga kama nini! Nilianza kuvuta sigara na kujihusisha katika upotovu wa maadili. Nilitambua kwamba maisha yangu mapya hayakupatana na maagizo niliyokuwa nikipata kwenye mikutano ya Kikristo, hivyo nikaacha kuhudhuria mikutano na kuhubiri nyumba kwa nyumba. Wazazi wangu walihuzunika sana, lakini sikujali tena jinsi wengine walivyohisi.

Naondoka Nyumbani

Baada ya kuwa katika shule ya sekondari kwa miaka miwili tu, niliondoka nyumbani na kwenda kuishi na marafiki katika ujirani. Nyakati nyingine nilirudi nyumbani bila kuonekana na kunyakua chakula ambacho ningepata na kukimbia. Akiwa amehuzunika, Baba aliacha kunilipia karo, akitumaini kwamba nitabadilika.

Hata hivyo, karibu na wakati huo, nilipata mtu wa kulipia masomo yangu. Mdhamini wangu alinitumia karo ya shule kutoka Scotland na nyakati nyingine pia alinipa zawadi, kutia ndani pesa. Pindi hiyo, ndugu zangu wawili waliacha kushirikiana na Mashahidi wa Yehova, na hilo lilizidisha huzuni ya wazazi wangu. Mara kadhaa Mama alinisihi akilia. Ingawa jambo hilo lilinifanya nihisi vibaya, sikubadili mwenendo wangu.

Maisha Katika Majiji Makubwa

Nilipomaliza shule mnamo 1977, nilienda Lagos na kupata kazi. Muda mfupi baada ya hapo, nilipata pesa kwa njia isiyo halali na kununua teksi. Nikiwa na pesa nyingi, nilianza kutumia dawa za kulevya na kuponda wakati katika vilabu vya usiku na madanguro. Maisha ya Lagos yalinichosha, na mnamo 1981 nikahamia London. Kutoka hapo nilienda Ubelgiji, ambako nilianza kujifunza Kifaransa na kufanya kazi ya muda katika hoteli. Hata hivyo, nilitumia wakati wangu mwingi kusafirisha magari na vifaa vya elektroniki hadi Nigeria.

Baba aliandikia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Ubelgiji na kuwaomba wawasiliane nami na kujaribu kujifunza nami Biblia. Lakini kila mara Mashahidi wa Yehova walipokuja nyumbani niliwafukuza. Nilianza kwenda kanisani ambako tungekula, kunywa, na kucheza baada ya ibada.

Maisha Yangu Nikiwa Mlanguzi wa Dawa za Kulevya

Mnamo 1982, nilisafirisha gari la kifahari hadi Nigeria na nikaenda bandarini ili kulitoa. Idara ya Forodha ya Nigeria iligundua kwamba hati ya kodi ya forodha ilikuwa bandia, kwa hiyo nikatiwa kizuizini kwa siku 40 hivi. Baba yangu alinitoa kwa dhamana. Kwa kuwa nilihitaji pesa za kukamilisha kesi hiyo, nilirudi Ubelgiji nikiwa na bidhaa fulani, kutia ndani kilo kadhaa za bangi. Baada ya kuondolewa shtaka la kuwa na hati hiyo bandia, nilijiimarisha katika biashara ya dawa za kulevya.

Safari moja nilikamatwa huko Uholanzi. Maofisa wa idara ya uhamiaji waliniingiza kwenye ndege na kunirudisha Nigeria. Nikiwa njiani nilikutana na walanguzi wengine wa dawa za kulevya, nasi tukaunda ushirika wa kuuza dawa za kulevya. Januari (Mwezi wa 1) 1984, nilihamia nchi nyingine ya Afrika. Kwa kuwa nilijua Kifaransa, lugha inayotumiwa huko, nilifanya urafiki na polisi, askari-jeshi, na maofisa wa idara ya uhamiaji. Hilo lilituwezesha kuingiza maelfu ya kilo za bangi nchini humo.

Nakamatwa na Kufungwa

Kisha nikajiingiza katika matatizo tena. Nilikuwa nimepanga na kapteni wa jeshi ambaye angenisaidia kupitisha bidhaa zangu kwenye uwanja wa ndege nchini humo. Lakini akachelewa, nami nikakamatwa. Polisi walinipiga na kunitesa sana hivi kwamba nikapoteza fahamu. Walinipeleka hospitali na kuniacha huko, wakitarajia nitakufa. Lakini sikufa na baadaye nilishtakiwa, nikahukumiwa, na kufungwa.

Nilipotoka jela, rafiki ambaye nilimwachia nyumba yangu alikuwa ameuza vitu vyangu vyote na kutoweka. Ili nijipatie riziki nilianza tena kuuza bangi. Hata hivyo, siku kumi baadaye nilikamatwa tena na kufungwa kwa miezi mitatu. Kufikia wakati ambapo nilifunguliwa, nilikuwa mgonjwa sana karibu tena nife. Lakini kwa njia fulani, nilifaulu kurudi Lagos.

Narudia “Biashara”

Huko Lagos nilikutana na baadhi ya washirika wangu, nasi tukaenda India ambako tulinunua heroini ya dola 600,000 hivi. Kutoka Bombay (ambayo sasa ni Mumbai) tulienda Uswisi, kisha Ureno, na mwishowe tukaenda Hispania. Tulipata faida kubwa, na kila mtu akarudi Lagos kwa njia tofauti. Mwishoni mwa mwaka wa 1984, niliuza shehena nyingine ya dawa za kulevya. Ndoto yangu ilikuwa kupata dola milioni moja kisha niishi Marekani.

Mnamo 1986, nilichukua pesa zote nilizokuwa nazo na kununua heroini ya hali ya juu sana huko Lagos. Niliipeleka katika nchi nyingine, lakini huko iliingia mikononi mwa mlanguzi mwenye pupa ambaye hakunilipa. Kwa kuhofia maisha yangu, nilirudi Lagos bila kusema chochote kuhusu masaibu yangu. Nilikuwa nimepoteza pesa zangu zote na nilikuwa nimevunjika moyo. Kwa mara ya kwanza niliketi na kufikiria kuhusu kusudi la maisha yangu. ‘Kwa nini ninapatwa na shida zote hizi?’ Nilijiuliza.

Kumrudia Mungu

Usiku mmoja baadaye, nilisali Yehova anisaidie. Asubuhi iliyofuata, mwanamume mzee na mkewe walibisha mlango wangu. Walikuwa Mashahidi wa Yehova. Niliwasikiliza kwa utulivu na kuchukua gazeti. “Wazazi wangu ni Mashahidi wa Yehova,” niliwaeleza. “Nilikuwa nikijifunza Biblia na Alice Obarah.”

Huyo mzee, P. K. Ogbanefe, akanijibu: “Tunawafahamu akina Obarah vizuri sana. Sasa wanatumika katika ofisi ya tawi ya Nigeria jijini Lagos.” Walinihimiza niwatembelee. Kukutana na akina Obarah kulinitia moyo sana. Baada ya hapo, Ndugu Ogbanefe alianza kunifunza Biblia, nami nikaanza kufanya mabadiliko katika maisha yangu mapotovu. Kwa sababu nilikuwa nimetumia dawa za kulevya kwa muda mrefu ilikuwa vigumu kufanya mabadiliko. Lakini nilikuwa nimeazimia kusafisha maisha yangu.

Licha ya hayo, bado kulikuwa na vishawishi na mikazo mingi! Waliodai kuwa marafiki wangu wangekuja nyumbani na kunitamanisha kwa mipango ya kupata pesa. Kwa muda fulani nilianza tena kuvuta sigara na kujihusisha na mwenendo mpotovu. Nilimimina moyo wangu kwa Mungu katika sala. Nilijua kwamba kwa kuwa marafiki wa ulimwengu walikuwa wamenipotosha, hawangenisaidia sasa. Pia nilitambua kuwa ili nifanye maendeleo ya kiroho, ilikuwa lazima niondoke Lagos. Lakini niliaibika kurudi nyumbani huko Ilesha. Mwishowe, nilimwandikia baba yangu na ndugu yangu mkubwa na kuwaomba nirudi nyumbani.

Baba alinihakikishia kwamba nilikaribishwa kurudi, naye ndugu yangu akasema atanisaidia kifedha. Kwa hiyo, miaka kumi baada ya kuwaacha wazazi wangu, nilirudi tena nyumbani. Nilipokewa kwa shangwe. “Asante Yehova!” Mama akasema. Baba aliporudi jioni, aliniambia, “Yehova atakusaidia.” Familia yote ikiwa pamoja, Baba alisali kwa Yehova na kumwomba anisaidie kwa kuwa sasa nilikuwa nimerudi kufanya mapenzi Yake.

Kulipia Muda Niliopoteza

Nilianza tena kujifunza Biblia na nikafanya maendeleo haraka; nilibatizwa Aprili 24, 1988 (24/4/1988). Mara moja nikawa mwenye bidii katika huduma. Novemba 1, 1989 (1/11/1989), nikaanza kutumika kama painia, yaani, mhubiri wa wakati wote. Mnamo 1995, nilikaribishwa kuhudhuria darasa la kumi la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma huko Nigeria. Kisha, mnamo Julai (Mwezi wa 7) 1998, nikawekwa kuwa mwangalizi anayesafiri, nikitembelea makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Mwaka mmoja baadaye, nilibarikiwa kumpata Ruth, ambaye alikuwa mke wangu na mwandamani wangu katika kazi ya kusafiri.

Washiriki wengine wa familia wamefanya maendeleo ya kiroho pia. Ndugu yangu mmoja, ambaye alikuwa ameacha kumtumikia Yehova, alianza tena kushiriki katika ibada ya kweli na akabatizwa. Ninafurahi kwamba Baba alituona tukirudi. Alikuwa mtumishi wa huduma kutanikoni hadi kifo chake mnamo 1993 akiwa na umri wa miaka 75. Bado Mama anaendelea kumtumikia Yehova kwa bidii huko Ilesha.

Nilisafiri katika nchi 16 za Ulaya, Asia, na Afrika nikitafuta utajiri. Kwa sababu hiyo nilijichoma mwenyewe kila mahali kwa maumivu mengi. (1 Timotheo 6:9, 10) Ninapotazama nyuma, ninasikitika sana kwamba nilipoteza maisha yangu ya ujana kwa sababu ya dawa za kulevya na mwenendo mpotovu. Ninajuta kwa kumhuzunisha sana Yehova Mungu na familia yangu. Hata hivyo, ninashukuru kwamba nimeishi muda mrefu ili niweze kubadili maisha yangu. Nimeazimia kudumu nikiwa mwaminifu kwa Yehova na kumtumikia milele.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Nikiwa kijana mwasi

[Picha katika ukurasa wa 15]

Siku ya ubatizo wangu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiwa na mke wangu, Ruth