Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ukristo Umeshindwa?

Je, Ukristo Umeshindwa?

Maoni ya Biblia

Je, Ukristo Umeshindwa?

ASILIMIA 33 hivi ya idadi ya watu duniani wanadai kuwa Wakristo. Hata hivyo, ulimwengu unazidi kugawanyika kisiasa na kuwa wenye jeuri hata zaidi. Je, hilo linamaanisha kwamba Ukristo ambao Yesu alifundisha una makosa? Au kosa linatokea kwa sababu ya njia ambayo watu wengi wanafuata mafundisho ya Kristo?

Makala hii itachunguza kile ambacho Kristo alifundisha na mfano alioachia wafuasi wake. Pia itaonyesha maoni ya kawaida miongoni mwa Wakristo, ambayo yanapingana na maana halisi ya Ukristo.

Aina ya Ukristo Uliopotoshwa

Mamia ya miaka baada ya kifo cha Kristo, aina fulani ya Ukristo uliopotoshwa ulichaguliwa kuwa dini iliyopendwa na Milki ya Roma. Badala ya kuonwa tena kama watu waliotengwa, kikundi hiki cha waliodai kuwa Wakristo kilijikuta kikiwa sehemu muhimu sana katika masuala ya kisiasa na kijamii huko Roma. Viongozi wa kidini, kama vile Augustine, walisema kuwa badiliko hilo linaonyesha kwamba Ufalme wa Mungu ambao watu walikuwa wakingojea ulikuwa umekuja. Viongozi kama hao walifundisha kuwa uvutano huo mpya wa kisiasa na kidini ungekuwa njia ya kufanya mapenzi ya Mungu duniani. Hivyo, umuhimu wa jitihada za wanadamu za kuongoza mambo duniani ulikaziwa.

Jambo hilo limefanya wengi waamini kuwa Mkristo ana jukumu la kujihusisha katika siasa za jamii. Ili hilo liwezekane, wengine wanaamini kuwa lazima Mkristo akose kutimiza sehemu fulani ya imani yake ili afanye mapenzi ya jamii anayoishi. Kwa mfano, watu huzungumza kuhusu mafundisho ya Kristo ya upendo na amani, huku wakichochea vita. Kwa sababu hiyohiyo, makanisa yanawatia moyo wafuasi wao wasali kuhusu Ufalme wa Mungu lakini wakati uleule yanategemeza viongozi wanaowanyanyasa watu.

Yesu hakuanzisha Ukristo huo usio wa kweli. Badala ya hivyo, huo ni Ukristo uliobuniwa na wanadamu na unafuatwa na wengi wanaodai kuwa Wakristo leo. Ukristo huo usio wa kweli umeshindwa, kama kuenea kwa kutojali kanuni za Biblia katika makanisa yote ya Jumuiya ya Wakristo leo kunavyoonyesha.

Yesu Alifundisha Nini Hasa?

Wengine wanaweza kushangaa wakisikia kwamba Yesu alisema kuwa wafuasi wake hawapaswi kuwa “sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo [yeye hakuwa] sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:15, 16) Kwa nini Yesu aliwatia moyo wanafunzi wake wachukue msimamo huo? Mtume Yohana, mwanafunzi mpendwa wa Yesu, anatupa jibu. Aliandika hivi: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.”—1 Yohana 5:19.

Kwa hiyo, mafundisho ya Kristo hayaelekezi watu kwa mashirika ya kibinadamu, bali kwa Ufalme wa Mungu, kwani huo ndio utakaoleta ulimwengu wenye haki na uadilifu. (Mathayo 6:10) Yesu mwenyewe hakujiingiza katika masuala ya kijamii ya wakati wake. Alikataa cheo cha kisiasa. (Yohana 6:15) Pia alikataa jeuri kuwa njia ya kusuluhisha ugomvi. (Mathayo 26:50-53; Yohana 18:36) Yesu hakutunga sheria za kuongoza nchi au zinazohusu raia wa kawaida. Hakuchukua msimamo wa kisiasa kwa masuala ya wakati wake. Kwa mfano, hakupigania haki za watumwa, au kujiingiza katika mgogoro uliokuwepo kati ya Wayahudi na Waroma.

Hilo halimaanishi kwamba Yesu hakujali watu au matatizo yao. Yesu alifundisha mambo mengi kuhusu jukumu la kila mmoja kwa mwanadamu mwenzake. Alitia moyo watu wawe wanyoofu katika kulipa kodi na pia alisisitiza umuhimu wa kujinyenyekeza kwa mamlaka iliyo halali. (Mathayo 22:17-21) Alifundisha jinsi ambavyo tunaweza kuonyesha kwamba tunajali masilahi ya wenye uhitaji. Pia alifundisha jinsi tunavyoweza kuwaonyesha wengine heshima na jinsi ya kuwa na hisia-mwenzi, kusamehe, na kuonyesha rehema. (Mathayo, sura ya 5-7) Inajulikana kwamba mafundisho ya Kristo yalikazia hasa upendo kwa Mungu na kwa jirani.—Marko 12:30, 31.

Ukristo wa Kweli Leo

Kwa hiyo, mfuasi wa kweli wa Kristo anapaswa kujiendeshaje? Atafanya kama vile Yesu alivyofanya. Ingawa atatii sheria za nchi, atadumisha msimamo wa kutokuwamo katika mambo ya kisiasa. (Yohana 12:47, 48) Hatavunja kanuni za Kikristo hata kuwe na mkazo mkubwa kiasi gani. (1 Petro 2:21-23) Kwa wakati uleule hatakuwa tu mtazamaji asiyejali. Mkristo wa kweli angejali sana masilahi ya walio karibu naye, kama Yesu alivyofanya. (Marko 6:34) Pia angejitolea mhanga kuwasaidia wengine kuishi maisha yenye furaha zaidi kwa kuwafanya waelewe na kuishi kulingana na mafundisho ya Kristo.—Yohana 13:17.

Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova leo wanajaribu kumwiga Kristo katika uhusiano wao na ulimwengu unaowazunguka. Ingawa wao ni raia wanaopenda amani na kutii sheria, wao si sehemu ya ulimwengu. Kama Yesu alivyofanya, wao pia wanakataa kushiriki katika jeuri na mizozo ya kisiasa ambayo ni ya kawaida wakati huu. Tumaini lao ni kwamba Ufalme wa Mungu utasuluhisha matatizo yanayokumba ulimwengu. Ukristo wa kweli unatokeza maisha yenye furaha na umoja zaidi kati ya wafuasi wake. (Yohana 13:34, 35) Kwa kweli, Ukristo wa kweli haujashindwa.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Je, Wakristo wanapaswa kujiingiza katika siasa?Yohana 6:15.

▪ Je, Kristo alipendekeza jeuri kuwa njia ya kusuluhisha ugomvi?Mathayo 26:50-53.

▪ Ni nini kinachowatambulisha Wakristo wa kweli?Yohana 13:34, 35.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 18]

EL COMERCIO, Quito, Ecuador