Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mfalme Atafuta Hekima

Mfalme Atafuta Hekima

Mfalme Atafuta Hekima

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI HISPANIA

KARNE ya 13 ilikuwa ni wakati wa ubaguzi na jeuri iliyopita kiasi. Bara la Ulaya lilikuwa na Vita vya Kidini na Baraza la Kuhukumu Wazushi. Hata hivyo, kwenye enzi hiyo yenye umwagaji mwingi wa damu mfalme wa Hispania alikuwa akijaribu kuleta mambo tofauti. Anaitwa Alfonso wa Kumi, ambaye pia anaitwa Alfonso mwenye Hekima.

Mfalme huyo anakumbukwa kwa kuchochea upendezi katika utamaduni ambao nyakati nyingine huitwa kipindi cha mwamko cha karne ya 13. Aliingiza huko Hispania elimu mpya kutoka nchi za mbali. Alipendezwa hasa na sanaa, historia, sheria, na sayansi. Kufanya hivyo kulikuwa na uvutano mkubwa katika kusitawi kwa utamaduni wa Hispania na bara lote la Ulaya. Lakini jambo muhimu zaidi ni kwamba jitihada zake zilichochea watu wapendezwe na Neno la Mungu, Biblia Takatifu.

Alfonso alikuwa mwanzilishi wa chuo ambacho Wayahudi, Waislamu, na “Wakristo” wasomi wangeshirikiana. Ili kurahisisha kazi yao, mfalme alianzisha na kutegemeza kifedha moja kati ya maktaba ya kwanza ulimwenguni iliyomilikiwa na Serikali.

Alfonso pia alishiriki sana katika kuandika na kukusanya maandishi mbalimbali ya kisheria, sayansi, na historia. Alichochea kusitawi kwa fasihi na ushairi, nyanja ambazo yeye mwenyewe alikuwa bingwa kama inavyoonyeshwa na cantigas zake maarufu. * Aliziandika katika lugha ya Gallego (Kigalisiani), lugha iliyotumiwa wakati huo kutunga na kuandika mashairi.

Chuo cha Watafsiri

Alfonso alikuwa mdhamini wa Chuo cha Watafsiri huko Toledo. “Kazi ya mfalme ilikuwa kuchagua watafsiri pamoja na maandishi yaliyopaswa kutafsiriwa,” kinaeleza kitabu La Escuela de Traductores de Toledo (Chuo cha Watafsiri huko Toledo). “Alipitia tafsiri hizo na kutia moyo kuwe na mijadala ya kisomi, na akadhamini utunzi mpya.”

Wasomi wa Toledo walianza kwa kutafsiri maandishi mengi ya Kiarabu. Wasomi Waislamu tayari walikuwa wametafsiri maandishi muhimu zaidi ya Kigiriki, Kihindi, Kiashuru, na Kisiria katika Kiarabu. Ujuzi uliotokana na kazi yote hiyo ulikuwa muhimu kwa wasomi Waislamu katika kuendeleza ukuzi wa hesabu, elimu ya nyota, historia, na jiografia. Nao watafsiri wa chuo cha Toledo wakatumia ujuzi huo mwingi. Jinsi gani? Kwa kutafsiri maandishi muhimu ya Kiarabu katika Kilatini na Kihispania.

Habari kuhusu kazi ambayo wasomi wa Toledo walifanya zilisambaa katika nchi nyingine. Wasomi kutoka vyuo vikuu vya Ulaya kaskazini walimiminika huko Toledo. Matukio yote hayo yalichangia sana maendeleo ya sayansi na fasihi katika nchi za Magharibi. Kwa kweli, kazi hiyo kubwa ya kutafsiri iliathiri sana ukuzi wa Kipindi cha Mwamko.

Jitihada za watafsiri wa Toledo ziliwawezesha madaktari kusoma vitabu vya kitiba vilivyoandikwa na Galen, Hippocrates, na Avicenna, ambavyo vilikusanywa katika kitabu kimoja kilichoitwa Canon of Medicine ambacho kilitumiwa kama kitabu cha mafunzo ya kitiba katika vyuo vikuu vya nchi za Magharibi hadi karne ya 17. Wataalamu wa elimu ya nyota waliweza kusoma maandishi ya Tolemi na kunufaika na elimu ya hesabu ya maumbo na chati zenye habari kuhusu nyota zilizoandikwa na al-Khwārizmī. *

Alfonso alitaka watu kwa ujumla wazielewe tafsiri hizo. Jitihada hiyo ilifanya Kihispania kiwe njia ya kuwasiliana kuhusu mambo ya kisayansi na fasihi. Kazi ambayo Alfonso alianzisha ilisaidia kubadili maoni ya wengi kwamba Kilatini ndiyo lugha pekee ya kisayansi na kitamaduni.

Biblia Alfonsina

Ujuzi ambao wasomi hao wa Toledo walipata kwa kutafsiri vichapo vingi uliwasaidia Alfonso alipowaamuru watafsiri sehemu za Biblia kwa Kihispania. Kulingana na mwanahistoria Mhispania, Juan de Mariana, mfalme alitoa pesa ili Biblia hiyo itafsiriwe akitumaini kuwa kufanya hivyo kutaboresha lugha ya Kihispania. Bila shaka, tafsiri hizo za awali za Biblia zilichangia kuendeleza lugha ya Kihispania.

Mfalme aliiona Biblia kuwa yenye thamani kwa ajili ya kuwafundisha wanadamu. Aliandika hivi katika utangulizi wa kitabu Crónica de España: “Tukichunguza manufaa yanayotokana na Maandiko Matakatifu, tunaona kuwa kuna mafundisho tunayopata kuhusu kuumbwa kwa ulimwengu, kuja kwa baba wa ukoo, . . . kuja kulikoahidiwa kwa Bwana wetu Yesu Kristo, kuteswa, kufufuliwa, na kupaa kwake mbinguni.”

Pia alikagua matayarisho ya vichapo vya fasihi alivyoiita General Estoria. Vilitia ndani kutafsiriwa kwa sehemu fulani za Maandiko ya Kiebrania katika Kihispania. (Sehemu fulani za Maandiko ya Kigiriki zilitafsiriwa baadaye.) Biblia hiyo ya kupendeza, inayojulikana kama Biblia Alfonsina, ndiyo iliyokuwa kubwa zaidi kutokezwa katika Enzi za Kati. Ilinakiliwa mara nyingi na sehemu fulani zilitafsiriwa katika Kireno na sehemu nyingine kwa Kikatalani.

Urithi wa Alfonso

Hati za wakati wa Alfonso zilifanya watu wapate ujuzi wa Maandiko katika enzi za giza la kiroho. Kupitia tafsiri hizi upendezi uliamshwa kwa Biblia za lugha ya asili. Kwa karne mbili zilizofuata, tafsiri nyingine za Biblia za Kihispania zilitokezwa.

Kubuniwa kwa mashine ya kuchapisha na kazi ngumu ya watafsiri wa karne ya 16 huko Hispania na kwingineko Ulaya kuliendeleza kazi ambayo Alfonso na wengine wa wakati uleule walianzisha. Watu kutoka sehemu zote za Ulaya mwishowe wangepata nakala ya Biblia kwa lugha yao wenyewe. Ingawa utawala wa Alfonso wa Kumi ulikumbwa na vita na uasi, kutafuta ujuzi kulifanya hekima ya kimungu iweze kufikiwa na kila mtu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Cantigas ni mashairi yaliyoimbwa enzi za kati na waimbaji wasafiri.

^ fu. 11 Al-Khwārizmī alikuwa mwanahisabati maarufu Mwashuru wa karne ya tisa ambaye aliboresha hesabu za aljebra na akaanzisha dhana za hesabu za Kihindi, kama vile matumizi ya namba za Kiarabu kutia ndani dhana ya sufuri na mambo ya msingi ya hesabu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 14]

TAFSIRI ZA MAPEMA ZA BIBLIA ZA KIHISPANIA

Alfonso wa Kumi hakuwa wa kwanza kutafsiri sehemu fulani za Maandiko katika Kihispania. Miaka michache kabla yake, Hermannus Alemannus, mmoja wa watafsiri ambao walifanya kazi katika chuo cha Toledo, alikuwa ametafsiri kitabu cha Zaburi moja kwa moja kutoka Kiebrania hadi Kihispania. Pia, mapema katika karne ya 13, Biblia inayoitwa Biblia medieval romanceada Prealfonsina (Biblia ya Enzi za Kati ya Kabla ya Alfonso) ilitafsiriwa. (Ona picha kushoto.) Tafsiri hiyo ndiyo inayosemekana kuwa Biblia kamili ya Kihispania ya zamani zaidi. Bila shaka tafsiri hiyo ilisaidia katika kutafsiri Biblia ya Alfonso wa Kumi miaka michache baadaye.

Msomi Thomas Montgomery alisema hivi kuhusu tafsiri hiyo ya Biblia iliyofanywa kabla ile ya Alfonso: “Mtafsiri wa Biblia hii alitokeza tafsiri sahihi na yenye lugha inayopendeza. Tafsiri hiyo hufuata kwa makini Biblia ya Kilatini inayoitwa Vulgate bila kutumia maneno mengi ya Kilatini. Lugha iliyotumiwa katika tafsiri hiyo ni rahisi na inayoeleweka, kama ilivyohitajika kwa Biblia iliyotafsiriwa kwa ajili ya watu wasiojua Kilatini.”

[Hisani]

Bible: Patrimonio Nacional. Real Biblioteca de El Escorial

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Sanamu ya Alfonso wa Kumi katika sehemu ya kuingilia ya Maktaba ya Kitaifa ya Hispania, Madrid

[Picha katika ukurasa wa 13]

Mfalme akiwa pamoja na watafsiri kutoka Toledo (juu); akiwa na wachoraji (chini); Injili ya Luka katika “Biblia Alfonsina” (chini kabisa)

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 13]

All photos except statue of Alfonso X: Oronoz