Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakati magonjwa hayatakuwapo tena!

Wakati magonjwa hayatakuwapo tena!

Wakati magonjwa hayatakuwapo tena!

WATU wengi hutumaini kwamba watapata kitulizo huko mbinguni kutokana na maumivu na magonjwa baada ya kufa. Hata hivyo, tofauti na wengi wanavyoamini, tumaini ambalo Biblia inatoa kwa wanadamu wote kwa ujumla ni kuishi katika paradiso duniani. (Zaburi 37:11; 115:16) Ahadi hizo za wakati ujao zinatia ndani afya bora, furaha, na uzima wa milele.

Kwa nini tunakuwa wagonjwa na kufa? Ulimwengu usiokuwa na magonjwa utatokeaje? Biblia inajibu maswali hayo.

Kinachosababisha magonjwa Adamu na Hawa, wazazi wetu wa kwanza, waliumbwa wakiwa na miili yenye afya kamilifu. (Mwanzo 1:31; Kumbukumbu la Torati 32:4) Waliumbwa waishi duniani milele. Walipomwasi Mungu kimakusudi ndipo miili yao ilianza kuathiriwa na magonjwa. (Mwanzo 3:17-19) Kwa kukataa mamlaka ya Mungu walivunja uhusiano pamoja na Muumba, ambaye ni Chanzo cha uhai wao mkamilifu. Wakawa na kasoro. Kwa sababu hiyo, wakawa wagonjwa na kufa, kama vile Mungu alivyokuwa amewaonya.—Mwanzo 2:16, 17; 5:5.

Baada ya kuasi, Adamu na Hawa wangeweza tu kupitishia watoto wao uhai usio mkamilifu. (Waroma 5:12) Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, leo wanasayansi wanatambua kwamba kuna kasoro fulani zilizorithiwa ambazo zinachangia kuwa na magonjwa na kifo. Hivi karibuni kikundi cha wanasayansi kilisema hivi baada ya uchunguzi wa muda mrefu: “Ni jambo lisiloepukika la kibiolojia kwamba mara tu baada ya uhai wetu kuanza, mwili wetu huchukua mkondo wa kujiharibu.”

Si kwa jitihada za wanadamu Sayansi inapata mafanikio makubwa katika kupigana na magonjwa. Lakini wanasayansi wameshindwa kumaliza kisababishi cha magonjwa. Jambo hilo haliwashangazi wanafunzi wa Biblia ambao wanafahamu maneno haya yaliyoongozwa kwa roho: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote.”—Zaburi 146:3.

Hata hivyo, kama vile Biblia inavyosema, “mambo yasiyowezekana kwa wanadamu yanawezekana kwa Mungu.” (Luka 18:27) Yehova anaweza kumaliza kisababishi cha magonjwa. Ataponya magonjwa yetu yote. (Zaburi 103:3) Neno lake lililoongozwa kwa roho linaahidi hivi: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4.

Unachohitaji kufanya Yesu Kristo alieleza waziwazi kile tunachopaswa kufanya ili kufurahia ulimwengu ambao hautakuwa na magonjwa. Alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Ujuzi juu ya Mungu na mafundisho ya Mwana wake Yesu yanapatikana katika Biblia. Ujuzi huo unatia ndani mashauri ambayo yanaweza kuboresha maisha yako sasa. Zaidi ya hayo, Mungu anaahidi ulimwengu usio na maumivu kwa waabudu wake waaminifu. Naam, Mungu anaahidi wakati ujao ambao “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

Maoni Yaliyosawazika Kuhusu Afya

Biblia hutia watu moyo waheshimu uhai. Kila mmoja kati ya Mashahidi wa Yehova huonyesha heshima hiyo kwa kutunza afya yake. Wao huepuka mazoea mabaya kama kutumia dawa za kulevya na tumbaku. Mungu hutazamia watumishi wake wawe na kiasi wanapokula na kunywa. (Methali 23:20; Tito 2:2, 3) Hatua hizo muhimu pamoja na kupumzika na kufanya mazoezi ya kutosha kunaweza kuzuia matatizo mengi ya afya. Huenda wale ambao ni wagonjwa wakahitaji kutafuta msaada kutoka kwa madaktari wanaoaminika.

Biblia inapendekeza tuwe na usawaziko na “utimamu wa akili.” (Tito 2:12; Wafilipi 4:5) Wengi leo wanakosa usawaziko na kuhangaikia sana kutafuta matibabu, hivi kwamba wanapuuza hali yao ya kiroho. Wengine wanageukia mbinu za matibabu zinazoweza kuwadhuru. Nao wengine wanapoteza pesa na muda kwa ajili ya matibabu yasiyofaa au yenye kudhuru.

Ukweli ni kwamba kwa sasa afya kamilifu haijapatikana. Unapongojea wakati ujao ambapo magonjwa hayatakuwapo tena, hekima na usawaziko ambao unapatikana katika Biblia unaweza kukusaidia kubaki ukiwa mwenye usawaziko unapotafuta afya nzuri.