Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Tumaini Gani kwa Ukristo?

Kuna Tumaini Gani kwa Ukristo?

Kuna Tumaini Gani kwa Ukristo?

JE, WATU wote duniani watageuzwa kuwa Wakristo, au Ukristo utatokomea? Je, Ukristo ulibaki ukiwa nuru nyangavu katika ulimwengu wenye giza, au ulipotoshwa? Hayo ni maswali yanayotusumbua hadi leo.

Akitumia mfano unaoeleweka kwa urahisi, Yesu alionyesha kwamba mara tu baada ya yeye kupanda mbegu za Ukristo, adui, Shetani angeharibu mambo. (Mathayo 13:24, 25) Hivyo si mwelekeo wa kijamii uliofanya Ukristo ubadilike katika karne za mapema baada ya huduma ya Yesu, bali ni kitendo kiovu cha adui Shetani. Leo makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yanaendeleza makosa yaliyofanywa zamani na yanavuna matokeo yake.—2 Wakorintho 11:14, 15; Yakobo 4:4.

Ukristo Washambuliwa kwa Hila

Yesu alitabiri kwamba mafundisho yake yangepotoshwa. Alisema: “Ufalme wa mbinguni umekuwa kama mtu aliyepanda mbegu nzuri katika shamba lake. Watu wakiwa wamelala usingizi, adui yake alikuja na kupanda magugu katikati ya ngano, naye akaondoka.” Kwa kushangaza watumishi walipomweleza kuhusu tendo hilo ovu na kuomba ruhusa wakusanye magugu, mtu huyo aliwaambia hivi: “Hapana; ili, mnapoyakusanya magugu, msije mkang’oa ngano pamoja nayo. Acheni zikue pamoja mpaka wakati wa mavuno; na katika majira ya mavuno nitawaambia wavunaji, Kwanza kusanyeni magugu na kuyafunga matita-matita ili kuyateketeza motoni, ndipo nendeni mkusanye ngano ghalani mwangu.”—Mathayo 13:24-30.

Kama Yesu mwenyewe alivyofafanua kwenye mfano wake, mtu aliyepanda ngano katika shamba anawakilisha Yesu, na mbegu alizopanda zinawakilisha Wakristo wa kweli. Adui aliyepanda magugu miongoni mwa ngano anawakilisha “Ibilisi.” Magugu yanawakilisha waasi-sheria na waasi-imani ambao walidai kuwa watumishi wa Mungu. (Mathayo 13:36-42) Mtume Paulo aliendelea kueleza kile ambacho kingetokea. Alisema hivi: “Ninajua kwamba baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wenye kukandamiza wataingia katikati yenu nao hawatalitendea kundi kwa wororo, na kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.”—Matendo 20:29, 30.

Ukristo Wapotoshwa

Je, mfano ambao Yesu alitoa na yale ambayo Paulo alitabiri yalitimia? Ndiyo yalitimia. Wanaume wenye kujitakia makuu walilitumia kutaniko ambalo Yesu alianzisha kwa faida yao wenyewe. Yesu alikuwa amewaambia wafuasi wake hivi: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19) Hata hivyo, watu wenye pupa ya mamlaka walifanya mapatano na viongozi wa serikali na makanisa yao yaliyoungwa mkono na Serikali yakajikusanyia mamlaka makubwa na utajiri mwingi. Makanisa hayo yalifundisha “mambo yaliyopotoka.” Kwa mfano, yalifundisha watu kuabudu Serikali na kudhabihu maisha yao vitani. Wale waliojiita Wakristo walijihusisha katika Vita Vitakatifu na kuwaua watu waliowaona kuwa si waamini. Pia walipigana vitani na kuwaua “ndugu” zao, yaani, waumini wenzao. Kwa kweli, hawakuwapenda jirani zao wala kudumisha msimamo wa kutounga mkono siasa.—Mathayo 22:37-39; Yohana 15:19; 2 Wakorintho 10:3-5; 1 Yohana 4:8, 11.

Kwa wazi, makanisa ambayo kwa karne nyingi yamejiita ya Kikristo yanawakilisha Ukristo bandia. Kama tulivyoona katika makala zilizotangulia, hiyo ndiyo sababu kumekuwa na mwelekeo wa makanisa kugawanyika na kuwa madhehebu, kujihusisha katika siasa, na kupuuza sheria za Mungu. Matunda hayo mabaya hayakutokezwa na Ukristo wa kweli bali ni matokeo ya Ukristo bandia ambao Ibilisi alipanda. Dini hiyo ya uwongo inaelekea wapi? Kama Yesu alivyoonyesha katika mfano wake, dini hiyo haitatokomea tu kwa kukosa waumini. Itahukumiwa na kuharibiwa.

Wakristo wa Kweli Wanaangaza Gizani

Hata hivyo, kabla ya “magugu” ya Ukristo wa uwongo kukusanywa na kuharibiwa, mfano wa Yesu unaonyesha kwamba jambo fulani lazima litendeke. Kwa karne nyingi, “magugu” ya Wakristo wa uwongo yalikua na kusambaa haraka sana hivi kwamba yalifunika “ngano” ya Ukristo wa kweli. Lakini Yesu alisema kwamba ngano ingetenganishwa na magugu wakati wa “mavuno,” ambao uliwakilisha “umalizio wa mfumo wa mambo.” Alisema pia: “Wakati huo waadilifu watang’aa kwa uangavu kama jua.” (Mathayo 13:39-43) Uthibitisho unaonyesha kwamba tumekuwa tukiishi katika umalizio wa mfumo wa mambo tangu Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, ambavyo vilitokea zaidi ya miaka 90 iliyopita. (Mathayo 24:3, 7-12) Je, sehemu hiyo ya mfano wa Yesu wa kinabii imetimia pia?

Wakristo wa kweli wametenganishwa na “magugu” ya Jumuiya ya Wakristo. Mashahidi wa Yehova ‘wanang’aa kwa uangavu kama jua,’ wakiwasaidia wengine kumjua Mungu wa kweli, Yehova. Mashahidi hawashushi viwango vyake. Badala yake, watu ambao wanakuwa Mashahidi lazima wafanye mabadiliko makubwa katika maisha yao ili kutii kanuni za Kikristo zinazopatikana katika Biblia.

Mashahidi wa Yehova hawaandai burudani katika mikutano yao, badala yake, wao hujitolea kuwafunza watu Biblia bila malipo. Wao pia huonyesha upendo na urafiki, sifa ambazo wanajifunza kutoka kwenye Biblia. Wanaamini kwamba Mungu ataigeuza dunia iwe paradiso na kuifanya ikaliwe na watu wapole kama alivyokusudia mwanzoni. Lakini kwanza, lazima uvutano mbaya wa dini ya uwongo inayoitwa katika Biblia Babiloni Mkubwa, uondolewe ulimwenguni. Kulingana na unabii wa Biblia, Yehova ataleta mabadiliko hayo makubwa hivi karibuni.—Mathayo 5:5; Ufunuo 18:9-10, 21.

Baada ya wanadamu watiifu kuwekwa huru kutokana na mazoea yenye kupotosha ya dini ya uwongo, Ukristo wa kweli utawaunganisha katika ibada wanadamu wote wanaoishi duniani. Ukristo wa kweli ambao Yesu aliupanda utakuwa na wakati ujao mzuri sana! Dunia yenye amani itakuwa tena kama Paradiso ya Edeni ambako hakutakuwa tena na dini zenye kuleta migawanyiko na kusababisha mvurugo.

[Picha katika ukurasa wa 7]

“Adui yake alikuja na kupanda magugu.”—Mathayo 13:25

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Unakaribishwa kwa mikono miwili kwenye Jumba lolote la Ufalme la Mashahidi wa Yehova ambako watu hufundishwa Biblia bila malipo

[Picha katika ukurasa wa 9]

“Nendeni mkusanye ngano ghalani mwangu.”—Mathayo 13:30