Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza kuepukaje ngono kati ya watu wa jinsia moja?

Ninaweza kuepukaje ngono kati ya watu wa jinsia moja?

Vijana Huuliza . . .

Ninaweza kuepukaje ngono kati ya watu wa jinsia moja?

“Nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilivutiwa na msichana mwenzangu shuleni. Nilichanganyikiwa na kuhofia kwamba huenda nikawa ninavutiwa kingono na watu wa jinsia yangu.”—Anna. *

“Nilipokuwa kijana, nilipambana na hisia za kuvutiwa kingono na wanaume wengine. Moyoni, nilijua kwamba hisia hizo si za kawaida.”—Olef.

“Mimi na rafiki yangu tulipigana busu mara moja au mbili. Kwa kuwa bado nilikuwa ninapendezwa na wavulana, nilijiuliza ikiwa mimi ni mtu anayevutiwa kingono na watu wa jinsia zote mbili.”—Sarah.

MTAZAMO wa siku hizi wa kuachilia mambo umewachochea vijana wengi wa jinsia moja kuwa na mahusiano ya kingono. “Wasichana wengi katika shule yangu wanadai kuwa wao wanavutiwa kingono na wasichana wenzao, wengine hudai kwamba wao huvutiwa kingono na watu wa jinsia zote mbili, na wengine hujihusisha katika mahusiano hayo kwa sababu ya udadisi,” anasema Becky mwenye umri wa miaka 15. Naye Christa, mwenye umri wa miaka 18, anasema anakumbana na hali hiyohiyo shuleni kwao. Anasema hivi: “Tayari wasichana wawili katika darasa langu wamenishawishi kufanya ngono nao. Mmoja wao aliniandikia barua na kuniuliza ikiwa ningetaka kuona inakuwaje msichana anapofanya ngono na msichana mwenzake.”

Wakati huu ambapo ngono kati ya watu wa jinsia moja inaonyeshwa waziwazi, huenda ukajiuliza: ‘Je, kweli ni dhambi kuwa na uhusiano wa kingono na mtu wa jinsia yako? Namna gani ikiwa ninavutiwa na mtu wa jinsia yangu? Je, hilo linamaanisha kwamba mimi nitakuwa shoga?’ *

Maoni ya Mungu Kuhusu Ngono Kati ya Watu wa Jinsia Moja

Leo, watu wengi kutia ndani viongozi fulani wa dini hawashutumu ngono kati ya watu wa jinsia moja. Hata hivyo, Biblia iko wazi kuhusu jambo hilo. Inatuambia Yehova Mungu aliumba mwanamume na mwanamke na kwamba alikusudia ngono ifanywe kati ya mume na mke tu. (Mwanzo 1:27, 28; 2:24) Hivyo, haishangazi kwamba Biblia inashutumu ngono kati ya watu wa jinsia moja.—Waroma 1:26, 27.

Bila shaka, huenda watu wengi wakasema kwamba Biblia imepitwa na wakati. Kwa mfano, Megan mwenye umri wa miaka 14 anasema: “Baadhi ya mambo yanayozungumziwa katika Biblia hayana maana leo.” Kwa nini wengi huwa na maoni kama hayo? Mara nyingi ni kwa sababu maoni ya Biblia yanapingana na maoni yao. Wanakataa Neno la Mungu kwa sababu linafundisha jambo tofauti na lile wanalotaka kuamini. Lakini maoni hayo yamepotoka, na Biblia inatuhimiza tusijiruhusu kuathiriwa na maoni hayo yasiyopatana na akili! Isitoshe, katika Neno lake, Yehova Mungu anatuambia kwamba amri zake ni kwa faida yetu. (Isaya 48:17, 18) Hilo linapatana na akili, kwa kuwa hakuna mtu anayetujua vizuri kuliko Muumba wetu.

Ukiwa kijana, huenda ukawa unakabili hisia mbalimbali. Vipi ikiwa unavutiwa kingono na mtu wa jinsia yako? Je, hilo linaonyesha wazi kwamba utakuwa shoga? Hapana. Kumbuka, uko katika “upeo wa ujana,” kipindi ambacho unasisimuka kingono bila kutaka. (1 Wakorintho 7:36) Kwa muda fulani huenda ukavutiwa kingono na mtu wa jinsia yako. Lakini kuwa na hisia hizo hakumaanishi kwamba utakuwa shoga. Takwimu zinaonyesha kwamba kwa kawaida hisia hizo hutoweka baada ya muda. Lakini huenda bado unajiuliza, ‘Chanzo cha hisia hizo ni nini?’

Watu wengine wanasema kwamba ushoga upo kwenye chembe za urithi. Wengine wanasema kwamba mtu hujifunza zoea hilo. Si kusudi la makala hii kujadili ikiwa zoea hilo ni la kurithiwa au ni la kujifunza. Kwa wazi, kusema kwamba ushoga unasababishwa na jambo fulani hususa haingekuwa kweli. Inaonekana kwamba kama ilivyo kwa mazoea mengine, ni vigumu kufahamu chanzo cha zoea hilo.

Hata chanzo kiwe nini, jambo muhimu ni kutambua kwamba Biblia inashutumu ngono kati ya watu wa jinsia moja. Hivyo, mtu anayevutiwa kingono na mtu wa jinsia yake anaweza kushinda tatizo hilo kwa kutotenda kulingana na tamaa hizo. Kwa mfano: Mtu anaweza kuwa na “mwelekeo wa ghadhabu.” (Methali 29:22) Huenda zamani alizoea kulipuka kwa hasira. Lakini baada ya kujifunza Biblia, anaona uhitaji wa kujizuia. Je, hilo linamaanisha kwamba hatawahi tena kupandwa na hasira? Hapana. Hata hivyo, kwa kuwa anajua yale ambayo Biblia inasema kuhusu hasira isiyodhibitiwa, hatendi kulingana na hisia zake. Hivyo ndivyo ilivyo kwa mtu anayevutiwa na mtu wa jinsia yake, lakini sasa amejifunza maoni ya Biblia kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja. Mara kwa mara, anaweza kurudiwa na tamaa hizo zisizofaa. Hata hivyo, kwa kutii shauri la Biblia, mtu anaweza kukataa kutenda kulingana na tamaa hizo.

Ni kweli kwamba huenda tamaa ya kufanya ngono na mtu wa jinsia yako ikawa imekita mizizi. Uwe na hakika, kwamba hata tamaa hiyo iwe imekita mizizi namna gani, unaweza kuishinda. (1 Wakorintho 9:27; Waefeso 4:22-24) Kwa vyovyote vile, wewe ndiye utakayeamua jinsi utakavyoishi. (Mathayo 7:13, 14; Waroma 12:1, 2) Na licha ya madai ya wengi, unaweza kujifunza kuthibiti tamaa zako na hata kuamua kutotenda kulingana na tamaa hizo—au hata kujifunza kuzidhibiti.

Kataa Mazoea Mabaya

Unaweza kuepukaje kujihusisha na ngono ya watu wa jinsia moja?

Kwanza Mtupie Yehova mahangaiko yako yote kupitia sala, ukiwa na uhakika kwamba ‘anakujali wewe.’ (1 Petro 5:7; Zaburi 55:22) Yehova anaweza kukuimarisha kwa kukupa amani “yenye ubora unaozidi fikira zote.” Amani hiyo ‘itaulinda moyo wako na nguvu zako za akili’ na kukupa “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili usitende kulingana na tamaa zisizofaa. (Wafilipi 4:7; 2 Wakorintho 4:7) Sarah, ambaye alihofia kwamba anavutiwa na watu wa jinsia zote mbili, anasema: “Kila wakati ninapopatwa na hisia hizo, mimi husali; na Yehova hunitegemeza. Nisingeweza kukabiliana na tatizo hilo bila msaada wake. Sala ndiyo msaada wangu mkubwa!”—Zaburi 94:18, 19; Waefeso 3:20.

Pili Jaza akili yako mambo ya kiroho yenye kujenga. (Wafilipi 4:8) Soma Biblia kila siku. Usidharau uwezo wake wa kuongoza akili na moyo wako daima. (Waebrania 4:12) Kijana mmoja anayeitwa Jason anasema: “Biblia—kutia ndani maandiko kama vile 1 Wakorintho 6:9, 10; na Waefeso 5:3—imenisaidia sana. Mimi husoma maandiko haya kila wakati tamaa mbaya zinaponijia.”

Tatu Epuka ponografia, yaani picha au habari za kingono na propaganda za ngono kati ya watu wa jinsia moja ambazo zinaweza kuchochea mawazo yasiyofaa. * (Zaburi 119:37; Wakolosai 3:5, 6) Sinema na vipindi fulani vya televisheni pia huendeleza wazo la kwamba ngono kati ya watu wa jinsia moja ni mtindo mwingine tu wa maisha. “Maoni yaliyopotoka ya ulimwengu yaliathiri sana akili yangu, na kufanya nichanganyikiwe kuhusu hisia za kuvutiwa na watu wa jinsia yangu,” anasema Anna. “Sasa mimi huepuka kabisa kitu chochote au mtu yeyote ambaye anaunga mkono ngono kati ya watu wa jinsia moja.”—Methali 13:20.

Nne Zungumza na mtu unayemwamini kuhusu hisia zako. (Methali 23:26; 31:26; 2 Timotheo 1:1, 2; 3:10) Olef, ambaye alitafuta msaada kutoka kwa mzee Mkristo anasema hivi: “Shauri lake lilinisaidia sana. Laiti ningeongea naye mapema.”

Usikate Tamaa!

Bila shaka, huenda wengine wakasema kwamba hakuna haja ya kuchukua hatua hizo zote, kwamba unapaswa kufuatia tamaa zako na kukubali jinsi ulivyo. Lakini, Biblia inasema kwamba unaweza kufanya mabadiliko! Kwa mfano, Biblia inatuambia kwamba baadhi ya Wakristo wa karne ya kwanza ambao walikuwa na zoea la kulala na watu wa jinsia yao walibadilika. (1 Wakorintho 6:9-11) Wewe pia unaweza kukabiliana na tatizo hilo—hata ingawa kwa sasa liko moyoni mwako tu.

Hata tamaa hizo zikiendelea, usivunjike moyo na kufikiria kwamba huwezi kubadilika. (Waebrania 12:12, 13) Sisi sote hushikwa na tamaa mbaya nyakati nyingine. (Waroma 3:23; 7:21-23) Ukikataa kutenda kulingana na tamaa hizo zisizofaa, baada ya muda fulani zitapungua. (Wakolosai 3:5-8) Zaidi ya yote, mtegemee Yehova akusaidie. Anakupenda na anajua kile ambacho kitakuletea furaha. (Isaya 41:10) Naam, “mtegemee Yehova na ufanye mema . . . , naye atakupa maombi ya moyo wako.” —Zaburi 37:3, 4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 7 Ingawa neno hili shoga linatumiwa hasa kuwahusu wanaume wanaolala na wanaume wenzao, katika makala hii linatumiwa pia kuhusu wanawake wanaolala na wanawake.

^ fu. 19 Mtindo ambao sasa unapendwa sana katika majiji mengi ni ule wa wanaume kuhangaikia sana sura yao hivi kwamba huwezi kutofautisha kati ya mwanamume wa kawaida na shoga. Kulingana na ripoti moja, mwanamume anayejiremba ‘anaweza kuwa mtu anayejulikana kuwa shoga, mwanamume wa kawaida, au anayevutiwa na jinsia zote mbili. Lakini hilo si muhimu kwani anajikazia fikira na kujihusisha na ngono yoyote inayomfurahisha.’ Ensaiklopedia moja inasema kwamba mtindo huo ulianza kuwa maarufu “baada ya mashoga kukubaliwa na jamii. Pia, jamii imeacha kuona mashoga na mtindo wa wanaume kujiremba kuwa mwiko.”

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Kwa nini Mungu hushutumu ngono kati ya watu wa jinsia moja?

▪ Utafanya nini ikiwa unakabiliana na hisia za kuvutiwa kingono na mtu wa jinsia yako?

▪ Unaweza kuongea na nani ikiwa unahangaishwa na hisia za kufanya ngono na mtu wa jinsia yako?

[Picha katika ukurasa wa 30]

Tafuta msaada kutoka kwa Mkristo mkomavu