Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanyeje nikiombwa nifanye ngono?

Nifanyeje nikiombwa nifanye ngono?

Vijana Huuliza

Nifanyeje nikiombwa nifanye ngono?

“Vijana huanzisha urafiki ili waone ikiwa wanaweza kufanya ngono na pia ili waone wanaweza kufanya ngono na watu wangapi.”—Penny. *

“Wavulana huzungumza waziwazi kuhusu jambo hilo. Wao hujigamba kwamba ingawa wana mpenzi wa kike bado wanaweza kufanya ngono na wasichana wengine wengi.”—Edward.

“Wale walioniomba kufanya ngono hawakuona haya. Hata nilipokataa bado waliendelea tu kuniomba!”—Ida.

KATIKA nchi nyingi watu hutumia maneno mbalimbali wanaporejelea tendo la kuanzisha urafiki kwa kusudi tu la kufanya ngono bila kuwajibika. Kwa mfano, msichana mmoja anayeitwa Akiko anasema kwamba nchini Japani watu huita tendo hilo, kupelekwa nje. “Pia wao hutumia neno sefre, linalomaanisha ‘rafiki wa kufanya naye ngono,’” anasema Akiko. “Sababu tu ya urafiki wao ni kufanya ngono.”

Haidhuru ni maneno gani yanayotumiwa, yote yanamaanisha jambo lilelile, yaani, kufanya ngono bila kuwajibika kokote. * Hata vijana fulani hujigamba kuwa na wale wanaowaita “washikaji,” yaani, marafiki ambao hawaleti “matatizo” ya kutaka kuanzisha uhusiano wa karibu wenye kuendelea. “Marafiki wa kufanya ngono tu hutosheleza hamu ya wakati huo,” anasema msichana mmoja. “Unapewa unachotaka na kuondoka.”

Ukiwa Mkristo, unapaswa ‘kuukimbia uasherati.’ * (1 Wakorintho 6:18) Ukitambua hilo, bila shaka wewe hujitahidi kuepuka hali ambazo zinaweza kukuingiza katika kishawishi. Hata hivyo, huenda vishawishi vikakupata. “Wavulana wengi sana shuleni wameniomba nifanye ngono nao,” anasema Cindy. Jambo kama hilo linaweza kutendeka kazini. “Meneja wangu aliniomba nifanye ngono naye,” anasema Margaret. “Alisisitiza sana jambo hilo hadi ikanibidi niache kazi!”

Kwa upande mwingine, usishangae ukianza kuvutiwa kufanya ngono. Biblia inasema: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yeremia 17:9) Msichana anayeitwa Lourdes aliona kwamba hilo linawezekana. Anakiri hivi: “Nilivutiwa na jamaa fulani aliyeniomba nifanye ngono naye.” Jane alikuwa na hisia kama hizo. Anasema, “Hisia zangu ziliguswa sana. Ilikuwa vigumu sana kwangu kukataa.” Edward aliyetajwa awali, anakubali kwamba si rahisi kudumisha usafi wa maadili. “Wasichana wengi wameniomba tufanye ngono, na kukataa kumekuwa jambo gumu zaidi nikiwa Mkristo,” anasema. “Ni vigumu sana kukataa!”

Ikiwa umewahi kuhisi kama Lourdes, Jane, na Edward lakini ukafanya lililo sawa machoni pa Yehova Mungu, unapaswa kupongezwa. Unaweza kufarijika kujua kwamba mtume Paulo pia alipigana vita vyenye kuendelea dhidi ya mielekeo isiyofaa.—Waroma 7:21-24.

Ni kanuni gani za Biblia unazopaswa kukumbuka unapoombwa ufanye ngono bila kuwajibika?

Tambua kwa Nini Ni Vibaya Kufanya Ngono Bila Kuwajibika

Biblia inashutumu kufanya ngono nje ya ndoa. Kwa kweli, uasherati ni dhambi nzito na waasherati “hawataurithi ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:9, 10) Ili upinge tamaa ya kufanya ngono bila kuwajibika, unapaswa kuona zoea hilo kama Yehova alionavyo. Kudumisha usafi wa maadili kunapaswa kuwa lengo lako.

“Ninaamini kwa uthabiti kwamba njia ya Yehova ndiyo njia bora zaidi ya maisha.”—Karen, Kanada.

“Mtu anaweza kupoteza vitu vingi anapopuuza sheria za maadili za Yehova kwa muda mfupi tu ili kuponda raha.”—Vivian, Mexico.

“Kumbuka kwamba wewe ni mtoto wa mtu fulani, una marafiki wengi, nawe ni mshiriki wa kutaniko fulani. Utawaumiza watu hao wote ukikubali kushawishiwa!”—Peter, Uingereza.

Mtume Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana.” (Waefeso 5:10) Unapokuwa na maoni ya Yehova kuhusu uasherati, utaweza ‘kuchukia yaliyo mabaya,’ hata ingawa huenda mwili wako usio mkamilifu ukavutiwa na mambo hayo.—Zaburi 97:10.

Tunapendekeza usome: Mwanzo 39:7-9. Ona msimamo wenye ujasiri wa Yosefu dhidi ya kishawishi cha kufanya ngono na kile kilichomsaidia kupinga kishawishi hicho.

Jivunie Imani Yako

Si ajabu kwa vijana kuchukua msimamo thabiti na kutetea jambo wanaloamini. Ukiwa Mkristo, una pendeleo la kutetea jina la Mungu kwa mwenendo wako mzuri. Usiaibikie msimamo wako wa kukataa katakata kufanya ngono kabla ya ndoa.

“Tangu mwanzo onyesha wazi kwamba una kanuni za juu za maadili.”—Allen, Ujerumani.

“Hakuna sababu ya kuaibikia mambo unayoamini.”—Esther, Nigeria.

“Vijana wenzako hawawezi kuheshimu msimamo wako kuhusu kutofanya ngono ukiwaambia, ‘Wazazi wangu hawawezi kuniruhusu niwe na rafiki wa karibu.’ Lazima uwaonyeshe vijana kwamba wewe hutaki kuwa na urafiki wa karibu nao.”—Janet, Afrika Kusini.

“Wavulana nilioenda nao shule ya sekondari walijua mimi ni nani, nao walijua kwamba wangekuwa wakipoteza muda wao ikiwa wangejaribu kunishawishi.”—Vicky, Marekani.

Kuchukua msimamo thabiti kwa ajili ya imani yako ni ishara ya kwamba unaendelea kuwa Mkristo mkomavu.—1 Wakorintho 14:20.

Tunapendekeza usome: Methali 27:11. Ona jinsi matendo yako yanavyoweza kutetea jambo muhimu zaidi ulimwenguni, yaani, kutakaswa kwa jina la Yehova!

Uwe Thabiti!

Ni muhimu kukataa. Lakini huenda wengine wasikuelewe na wakadhani kwamba unajifanya tu eti hupendezwi na ngono.

“Huenda kukataa kukaonekana ni kama unamjaribu anayekuomba ufanye naye ngono, kana kwamba umemwekea kizuizi anachopaswa kushinda, na hivyo unamchochea aongeze bidii.”—Lauren, Kanada.

“Kila jambo unalofanya, kutia ndani mavazi yako, jinsi unavyoongea, watu unaozungumza nao, na jinsi unavyoingiliana na watu, linapaswa kuonyesha kwamba hukubali maombi yao.”—Joy, Nigeria.

“Unapokataa ombi hilo unapaswa kuwa thabiti na useme kwa mkazo.”—Daniel, Australia.

“Uwe imara! Kijana mmoja alipojaribu kunishawishi, nilimwambia, ‘Ondoa mkono wako juu ya bega langu!’ kisha nikaondoka nikiwa na uso usiotaka mchezo.”—Ellen, Uingereza.

“Lazima useme mambo wazi na kuwaambia hutaki wala hutabadili nia. Huo si wakati wa kuwa mpole!”—Jean, Scotland.

“Mvulana mmoja aliendelea kunisumbua kwa kunishawishi na kuniambia maneno ya kejeli. Lakini nilipokuwa thabiti kabisa aliacha kunisumbua.”—Juanita, Mexico.

“Lazima useme waziwazi kwamba hutawahi kufanya ngono nao. Usikubali zawadi kutoka kwa wavulana wanaotaka kufanya ngono nawe. Wanaweza kutumia zawadi hizo kama kisingizio.”—Lara, Uingereza.

Yehova atakusaidia ukiwa thabiti. Kwa kutegemea mambo aliyojionea, mtunga-zaburi Daudi angeweza kumwambia Yehova: “Kwa mtu mshikamanifu utatenda kwa ushikamanifu.”—Zaburi 18:25.

Tunapendekeza usome: 2 Mambo ya Nyakati 16:9. Ona jinsi Yehova anavyotaka sana kuwasaidia wale ambao mioyo yao ni kamili kumwelekea.

Tazama Mbele

Biblia inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” (Methali 22:3) Unaweza kufuataje shauri hilo? Kwa kutazama mbele!

“Jiepushe kabisa na watu ambao huzungumza kuhusu mambo hayo.”—Naomi, Japani.

“Epuka ushirika na hali ambazo zinaweza kuwa hatari. Kwa mfano, ninajua watu fulani ambao walikubali kushawishiwa walipokuwa wametumia kileo.”—Isha, Brazili.

“Usiwaambie watu habari za kibinafsi kama vile, mahali unapoishi au namba yako ya simu.”—Diana, Uingereza.

“Usiwakumbatie ovyoovyo wanafunzi wenzako.”—Esther, Nigeria.

“Chunguza mavazi yako. Usivalie mavazi yanayoamsha nyege.”—Heidi, Ujerumani.

“Kuwa na uhusiano mzuri na wazazi wako na kuzungumzia mambo kama hayo ni ulinzi thabiti.”—Akiko, Japani.

Chunguza usemi, mwenendo, marafiki, na mahali ambapo wewe hupenda kwenda. Kisha jiulize, ‘Je, ninajitia katika hali au kutoa ishara ambazo zitawafanya wengine waniombe nifanye ngono nao?’

Tunapendekeza usome: Mwanzo 34:1, 2. Ona jinsi ambavyo kuwa mahali pasipofaa kulimletea madhara msichana anayeitwa Dina.

Kumbuka, kufanya ngono bila kuwajibika ni jambo zito sana machoni pa Yehova; nawe unapaswa kuwa na maoni kama hayo. Biblia inasema: “Hakuna mwasherati au mtu asiye safi . . . aliye na urithi wowote katika ufalme wa Kristo na wa Mungu.” (Waefeso 5:5) Kwa kuchukua msimamo kwa ajili ya lililo sawa, unaweza kudumisha dhamiri safi na kujiheshimu. Kama tu msichana anayeitwa Carly anavyosema, “Kwa nini umruhusu mtu mwingine ‘akutumie’ kutosheleza hamu yake ya muda tu? Tunza msimamo safi mbele za Yehova ambao umejitahidi kuudumisha kwa muda mrefu!”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 7 Maneno hayo yanaweza pia kutia ndani mwenendo unaohusisha mambo kama vile kupapasana na kubusiana kwa njia yenye kuamsha nyege.

^ fu. 8 Uasherati unatia ndani mambo kama vile ngono kati ya watu ambao hawajafunga ndoa, ngono ya mdomo na ya mkundu, vitendo vya ngono kati ya watu wa jinsia moja, kumpiga mtu mwingine punyeto, na vitendo vingine vinavyohusisha matumizi yasiyofaa ya viungo vya uzazi kati ya watu wawili ambao hawajaoana.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Ingawa huenda mwili wako usio mkamilifu ukavutiwa kufanya ngono haramu, kwa nini si sawa?

▪ Utafanya nini ikiwa mtu fulani anakuomba ufanye ngono naye bila kuwajibika?

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

▪ Biblia inasema kwamba mtu anayefanya uasherati “anautendea dhambi mwili wake mwenyewe.” (1 Wakorintho 6:18) Je, Biblia inasema kweli? Hebu fikiria sababu kadhaa, na uziandike hapa chini.

․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

Pendekezo: Ili kukusaidia kujibu swali lililo hapa juu, ona kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, ukurasa wa 333, na Insight on the Scriptures, Buku la 1, ukurasa wa 863. Vitabu vyote viwili vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

TAARIFA KWA WAZAZI

“Mwanafunzi mwenzangu alinitongoza shuleni. Sikuelewa mara moja kile alichokuwa akiniambia. Nilikuwa na umri wa miaka 11 tu.”—Leah.

Watoto wenye umri mdogo sana wanaambiwa kuhusu ngono. Zamani sana Biblia ilitabiri kwamba katika “siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” kwani watu watakuwa “wasiojizuia” na “wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:1, 3, 4) Tabia ya kufanya ngono bila kuwajibika, iliyozungumziwa katika makala hii kwa ajili ya vijana, ni jambo moja linaloonyesha kwamba unabii huo umetimia.

Ulimwengu wa leo ni tofauti sana na ule ambao wewe ulilelewa. Hata hivyo, katika njia fulani matatizo ni yaleyale. Kwa hiyo, usishangazwe wala kuogopeshwa na uvutano mbaya unaowazunguka watoto wako. Badala ya hivyo, azimia kuwasaidia kufanya kama mtume Paulo alivyowasihi Wakristo miaka 2,000 hivi iliyopita: “Vaeni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili mweze kusimama imara kupinga hila za Ibilisi.” (Waefeso 6:11) Ukweli ni kwamba, vijana wengi Wakristo wanajitahidi sana kufanya yaliyo sawa licha ya uvutano usiofaa unaowazunguka. Unaweza kuwasaidiaje watoto wako wafanye hivyo pia?

Njia moja ni kwa kuzungumza waziwazi na mwana au binti yako ukitumia habari hii. Sehemu za “tunapendekeza usome” zina marejeo ya maandiko yanayomchochea mtu afikiri. Maandiko fulani yaliyorejelewa yanazungumzia mifano ya watu halisi ambao walichukua msimamo kwa ajili ya lililo sawa na baraka walizopata, na pia watu waliopuuza sheria za Mungu na kupatwa na madhara. Maandiko mengine katika sehemu ya “tunapendekeza usome” yana kanuni zinazoweza kuwasaidia watoto wako kutambua kwamba ni pendeleo kubwa kwako na kwao kuishi kulingana na sheria za Mungu. Kwa nini usipitie habari hiyo pamoja nao sasa?

Sikuzote kuishi kulingana na viwango vya Mungu hutunufaisha. (Isaya 48:17, 18) Sikuzote kupuuza viwango hivyo hutokeza madhara. Wachapishaji wa Amkeni! wanakutakia baraka za Yehova unapojitahidi kukazia sheria na kanuni za Mungu katika mioyo ya watoto wako.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Lazima useme waziwazi kwamba hutawahi kufanya ngono nao