Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza kujifunza lugha nyingine!

Unaweza kujifunza lugha nyingine!

Unaweza kujifunza lugha nyingine!

“Siwezi kulinganisha jambo hilo na kitu kingine chochote,” anasema Mike. Phelps anaongeza hivi: “Ni mojawapo ya maamuzi bora niliyofanya maishani mwangu.” Wote wanazungumza kuhusu msisimuko wa kujifunza lugha nyingine.

KATIKA nchi nyingi duniani, watu wengi wanajifunza lugha nyingine kwa sababu mbalimbali. Wengine wanajifunza kwa sababu za kibinafsi, wengine kwa sababu za kiuchumi, na wengine kwa sababu za kidini. Mwandishi wa Amkeni! aliwahoji watu kadhaa ambao wanajifunza lugha nyingine. Haya ni baadhi ya maswali waliyoulizwa, Ni matatizo gani ambayo mtu hukabili anapojifunza lugha mpya akiwa mtu mzima na ni nini kinachoweza kumsaidia? Makala hii itazungumzia maoni yao. Huenda ukajifunza jambo fulani kutokana na maelezo yao au ukatiwa moyo hasa ikiwa unajifunza lugha mpya au unafikiria kufanya hivyo. Kwa mfano, fikiria baadhi ya sifa ambazo wale waliohojiwa walisema ni muhimu ili kujifunza lugha nyingine.

Subira, Unyenyekevu, na Kubadilikana

Ni rahisi kwa watoto kujifunza lugha mbili au zaidi kwa wakati uleule, mara nyingi kwa kusikia tu lugha hizo zikizungumzwa. Lakini ni vigumu sana kwa watu wazima kujifunza lugha nyingine. Sababu moja ni kwamba wanapaswa kuwa na subira kwa kuwa kujifunza lugha mpya kunaweza kuchukua muda mrefu sana. Na kwa sababu wana shughuli nyingi sana, mara nyingi hilo humaanisha waahirishe kufanya mambo fulani.

“Unyenyekevu ni muhimu,” anasema George. “Unapoanza kujifunza lugha nyingine, unapaswa kuwa tayari kuzungumza na hata nyakati nyingine, kutendewa kama mtoto.” Kitabu How to Learn a Foreign Language kinaeleza hivi: “Usijione kuwa bora na usihangaikie jinsi watu wanavyokuona ikiwa unataka kufanya maendeleo.” Kwa hiyo, usiaibike unapokosea. “Ikiwa hufanyi makosa yoyote, basi hutumii lugha hiyo vya kutosha,” anasema Ben.

Usihisi vibaya wengine wakikucheka unapokosea, badala yake cheka pamoja nao! Huenda siku moja utasimulia mambo yenye kuchekesha ambayo uliwahi kusema. Na usiogope kuuliza maswali. Kuelewa sababu inayowafanya watu wazungumze kwa njia fulani kutakusaidia kukumbuka.

Kwa kuwa mara nyingi kujifunza lugha mpya humaanisha kujifunza utamaduni mpya, itafaa ubadilikane na hali, kuwa tayari kukubali maoni mapya. “Kujifunza lugha nyingine kumenisaidia kutambua kwamba kuna njia nyingi za kuona na kufanya mambo,” anasema Julie. “Si lazima njia moja iwe bora kuliko njia nyingine, zinatofautiana tu.” Jay anapendekeza, “Jitahidi kufanya urafiki na watu wanaozungumza lugha hiyo na ufurahie kuwa pamoja nao.” Bila shaka, Wakristo watahakikisha kwamba marafiki hao ni watu wazuri wanaotumia lugha inayofaa. (1 Wakorintho 15:33; Waefeso 5:3, 4) Jay anaongezea hivi, “Watu watavutiwa nawe wakiona kwamba unapendezwa nao, na chakula chao, muziki wao, na mambo mengine.”

Kadiri unavyotumia wakati mwingi kujifunza na kutumia lugha hiyo, ndivyo utakavyofanya maendeleo haraka. “Mtu hujifunza kutumia lugha sawa na jinsi kuku hudonoa chakula, punje moja baada ya nyingine,” anasema George. “Ingawa hadonoi punje nyingi kwa wakati mmoja, punje hizo huongezeka kadiri anavyokula.” Bill, ambaye amejifunza lugha kadhaa akiwa mmishonari, anasema, “Kila mahali nilipoenda, nilibeba orodha ya maneno na kuisoma nilipopata nafasi.” Wengi wameona kwamba ni afadhali kujifunza kwa kawaida kwa muda mfupi, badala ya kutumia wakati mwingi kujifunza mara mojamoja tu.

Kuna vifaa vingi mbalimbali vya kuwasaidia watu kujifunza lugha, kutia ndani vitabu, rekodi, kadi za kujifunzia, na kadhalika. Hata hivyo, licha ya kuwa na vifaa vyote hivyo watu wengi huona kwamba wanajifunza kwa urahisi wanapokuwa darasani. Tumia njia yoyote inayokufaa. Hata hivyo, kumbuka kwamba hakuna njia ya mkato. Lazima ujifunze kwa bidii bila kuacha. Lakini kuna njia za kufanya kujifunza kuwe rahisi na kufurahishe zaidi. Njia moja ni kuchangamana sana na watu wanaozungumza lugha hiyo na kujifunza utamaduni wao.

“Baada ya kujifunza mambo ya msingi kuhusu lugha hiyo,” anasema George, “huenda ikafaa kukaa kwa muda fulani katika nchi ambayo lugha hiyo huzungumzwa.” Barb anakubaliana naye, anasema hivi: “Kutembelea nchi hiyo kunaweza kukusaidia kupata ladha ya lugha unayojifunza.” Jambo muhimu zaidi ni kwamba kuwa katika mazingira hayo hukusaidia kufikiri katika lugha hiyo mpya. Ni kweli kwamba huenda watu wengi wasiweze kwenda katika nchi nyingine. Lakini kunaweza kuwa na nafasi za kuchangamana na watu wanaotumia lugha hiyo na kuona utamaduni wao. Kwa mfano, huenda kukawa na vichapo au programu za redio au za televisheni katika lugha unayojifunza ambazo zinafaa. Tafuta watu katika eneo la kwenu ambao wanaijua lugha hiyo vizuri na uwe ukizungumza nao. Kitabu How to Learn a Foreign Language kinasema: “Ili ufanye maendeleo, ni lazima ufanye mazoezi.” *

Unapofanya Maendeleo Kidogo

Unapoendelea kujifunza lugha huenda nyakati nyingine ukahisi kwamba hufanyi maendeleo yoyote. Unaweza kufanya nini? Kwanza, fikiria sababu zilizokufanya utake kujifunza lugha hiyo. Wengi wa Mashahidi wa Yehova wameanza kujifunza lugha mpya ili kuwasaidia wengine wajifunze Biblia. Ukikazia fikira miradi au kusudi lako la kujifunza lugha hiyo utaimarisha azimio lako.

Pili, usitarajie mengi kupita kiasi. “Huwezi kuongea lugha hiyo kama mwenyeji,” kinasema kitabu How to Learn a Foreign Language. “Hilo si kusudi lako. Kusudi lako ni watu waweze kukuelewa.” Kwa hiyo, badala ya kulalamika kwamba huzungumzi lugha hiyo kwa mtiririko kama lugha yako ya asili, jitahidi kuzungumza kwa njia inayoeleweka, ukitumia yale uliyojifunza.

Tatu, jaribu kupima maendeleo yako kupitia mambo muhimu ambayo umetimiza. Kujifunza lugha ni kama kuangalia nyasi zikikua. Huwezi kuona ukuzi wenyewe lakini siku kwa siku nyasi hizo hurefuka. Vivyo hivyo, ukilinganisha mahali ulipoanzia na mahali ambapo umefika sasa, bila shaka utaona kwamba umefanya maendeleo. Epuka kupima maendeleo yako kwa kujilinganisha na wengine. Kanuni nzuri ya kufuata inapatikana katika Biblia kwenye Wagalatia 6:4. Andiko hilo linasema: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.”

Nne, ona kujifunza lugha mpya kuwa jambo litakalochukua muda mrefu na jitihada, lakini litaleta faida. Hebu fikiria, mtoto mwenye umri wa miaka mitatu au minne anaweza kuzungumza kwa ustadi kadiri gani? Je, yeye anatumia misamiati migumu na miundo tata ya kisarufi? La! Hata hivyo, anaweza kuwasiliana kwa njia rahisi. Kwa kweli, hata mtoto anahitaji miaka kadhaa ili ajifunze lugha.

Tano, tumia lugha hiyo mpya mara nyingi iwezekanavyo. “Nilishindwa kufanya maendeleo wakati ambapo sikutumia lugha hiyo kwa kawaida,” anasema Ben. Kwa hiyo endelea kuitumia. Zungumza, zungumza, zungumza! Bila shaka, inafadhaisha unapojaribu kuwasiliana katika lugha ambayo unajua maneno machache tu kama mtoto. “Jambo gumu zaidi kwangu ni kushindwa kusema jambo ninalotaka kusema wakati ninapotaka kulisema,” anasema Mileivi. Lakini mfadhaiko huo unaweza kukusukuma kuvumilia. “Nilichukizwa sana wakati ambapo sikuelewa hadithi au vichekesho,” anakumbuka Mike. “Nafikiri kwamba jambo hilo lilinichochea kufanya maendeleo.”

Jinsi Wengine Wanavyoweza Kusaidia

Wale ambao tayari wanajua lugha hiyo wanaweza kumsaidiaje mtu anayejifunza? Bill, aliyenukuliwa mapema anashauri hivi: “Zungumza polepole lakini kwa usahihi na usizungumze kama mtoto.” Julie anasema hivi: “Uwe na subira na umruhusu yule anayejifunza akamilishe sentensi yake.” Tony anakumbuka hivi: “Watu wanaojua lugha zaidi ya moja walikuwa wakizungumza nami wakitumia lugha yangu ya asili. Lakini kufanya hivyo kulinizuia kufanya maendeleo haraka.” Kwa hiyo, watu fulani wanaojifunza lugha mpya wamewaomba rafiki zao wazungumze nao katika lugha hiyo nyakati fulani na wawatajie mambo hususa ambayo wanapaswa kuyafanyia kazi. Pia wale wanaojifunza lugha mpya hufurahi wanapopongezwa kwa sababu ya jitihada zao. Kama George anavyosema, “Nisingeweza kufaulu bila upendo na kutiwa moyo na rafiki zangu.”

Kwa hiyo, je, kuna faida zozote za kujifunza lugha nyingine? “Bila shaka ziko!” anajibu Bill, ambaye, kama ilivyotajwa awali, anaweza kuzungumza lugha nyingi. “Kufanya hivyo kumepanua mtazamo wangu kuhusu maisha na kunisaidia kuona mambo kwa njia tofauti. Ninapofaulu kujifunza Biblia na watu wanaozungumza lugha hizo na kuwaona wakifanya maendeleo ya kiroho, mimi husahau matatizo niliyokabili nilipokuwa nikijifunza lugha hizo. Kwa kweli, mwanamume mmoja anayezungumza lugha 12 aliniambia hivi pindi moja: ‘Nakuonea wivu. Mimi hujifunza lugha ili kujifurahisha tu; lakini wewe unajifunza ili kuwasaidia watu.’”

[Maelezo ya Chini]

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Tamaa ya kuwasaidia wengine ni kichocheo chenye nguvu cha kujifunza lugha mpya