Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Wanatumia Intaneti!

Vijana Wanatumia Intaneti!

Vijana Wanatumia Intaneti!

Hebu wazia mtoto wako akizurura mitaani usiku akiwa peke yake.

Hebu wazia kijana wako akifanya karamu ndani ya nyumba yako bila wewe kuwa na habari.

Hebu wazia mwana au binti yako akitoa nakala ya funguo za nyumba yako na kuwapa watu usiowajua hata kidogo.

IKIWA mtoto wako anatumia Intaneti, basi mambo yaliyotajwa hapo juu hayapaswi kukushangaza. Gazeti Science News linasema: “Sasa kuliko wakati mwingine wowote, Intaneti inaandaa sehemu mbalimbali ambazo watu wanaweza kukutana, kama vile katika vituo vya kutoa maoni kuhusu mambo mbalimbali, vituo vya kutuma ujumbe haraka, na hata vituo vya kuwasiliana na wengine.”

Vijana wamejifunza haraka kutumia Intaneti. Mnamo 2004, karibu vijana 9 kati ya 10 huko Marekani walio na umri wa miaka 12 hadi 17, walitumia Intaneti ambayo inapatikana karibu kila mahali ulimwenguni.

Watu wengi wanakubali kwamba Intaneti ni muhimu. Lakini hatupaswi kupuuza hatari zake. Kwa mfano, vijana wengi wanatumia Intaneti bila usimamizi wa wazazi, na wengine wanaanzisha mawasiliano na watu ambao wewe, au mtoto wako, hamwezi kuwakaribisha nyumbani.

Vijana fulani wasio na uzoefu huweka habari zao za kibinafsi, maoni, na picha kwenye Intaneti. Profesa Zheng Yan wa Chuo Kikuu cha Serikali cha New York anasema kwamba ‘mara nyingi vijana hawatambui ni watu wangapi wanaoweza kupata habari hizo. Hata watu wanaowavizia watoto kwenye Intaneti ili wafanye nao ngono wanaweza kuzipata habari hizo.’

Na tuchunguze kwa uangalifu yale ambayo vijana wanafanya kwenye Intaneti. Hilo linaweza kutusaidia kuona matatizo yanayoweza kutokea, kutambua watoto wetu wanatafuta nini hasa, na kuona jinsi tunavyoweza kuwasaidia kutosheleza mahitaji yao yanayofaa. Uchunguzi huo pia utawasaidia vijana Wakristo wabaki wakiwa waaminifu kwa Mungu katika nyakati hizi ngumu.—2 Timotheo 3:1-5.