Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Inamaanisha Nini Kuwa Mkristo?

Inamaanisha Nini Kuwa Mkristo?

Maoni ya Biblia

Inamaanisha Nini Kuwa Mkristo?

“NCHINI kwetu, kuwa Mkristo kunamaanisha kwenda kanisani mara moja kwa juma,” anasema Kingsley kutoka nchi moja ya Afrika. Raad kutoka Mashariki ya Kati anaeleza hivi: “Katika jamii yetu, Wakristo huonwa kuwa kikundi cha watu kinachofuata desturi na utamaduni wa Ulaya na Marekani kwa sababu ya mavazi yao, sherehe, na jinsi wanavyowatendea wanawake.”

Lakini je, kuwa Mkristo kunamaanisha kwamba mtu huenda kanisani mara moja kwa juma na kufuata desturi na utamaduni fulani? Je, neno “Mkristo” halipaswi kumaanisha njia ya maisha inayoonyesha mtazamo, viwango, na mwenendo ambao Kristo alihubiri na kuishi kulingana nao? * Wakristo wa mapema walijiendeshaje?

Ukristo wa Mapema—Njia ya Maisha

Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Ninyi ni rafiki zangu ikiwa mnafanya ninalowaamuru ninyi.” (Yohana 15:14) Mwanzoni wanafunzi wa Yesu waliita dini yao “Ile Njia” kwa kuwa mafundisho ya Yesu yalihusu kila sehemu ya maisha yao. (Matendo 9:2) Muda mfupi baada ya hapo, “kwa uongozi wa kimungu waliitwa Wakristo.” (Matendo 11:26) Jina hilo jipya lilimaanisha waliamini kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, ambaye aliwafunulia wanadamu mapenzi ya Baba yake wa mbinguni. Imani hiyo iliwafanya wafuate njia ya maisha ambayo ilitofautiana na ulimwengu uliowazunguka.

Mafundisho ya Kristo yaliwafanya wafuasi wake wafuate mafundisho ya Biblia, na hilo lilimaanisha kuepuka “uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu, ibada ya sanamu, mazoea ya kuwasiliana na pepo, uadui, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, magomvi . . . vipindi vya kulewa, karamu za kupindukia, na mambo kama hayo.” (Wagalatia 5:19-21; Waefeso 4:17-24) Mtume Paulo aliwakumbusha Wakristo Wakorintho kwamba wakati mmoja wengine kati yao walikuwa wamezoea kufanya mambo hayo. Kisha akaongeza: “Lakini mmeoshwa mkawa safi, lakini mmetakaswa, lakini mmetangazwa kuwa waadilifu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo.”—1 Wakorintho 6:9-11.

E. W. Barnes anaeleza hivi katika kitabu chake (The Rise of Christianity) kinachozungumzia kusitawi kwa Ukristo: “Maandishi ya mapema kuhusu Ukristo yanaufafanua kuwa wenye kufuata maadili na sheria. Washiriki wake walijitahidi kuwa raia wazuri na waaminifu. Waliepuka upotovu uliokuwepo katika dini za kipagani. Katika maisha ya kibinafsi walijaribu kuwa majirani wenye amani na marafiki wanaoaminika. Walifundishwa kuwa watu wanaochukua mambo kwa uzito kwa kadiri inayofaa, kuwa wenye bidii na kuishi maisha manyoofu. Ingawa waliishi wakati kulipokuwa na ufisadi mwingi na uasi-sheria, Wakristo waliofuata kanuni walizofundishwa walikuwa wanyoofu na wenye kusema kweli. Viwango vyao kuhusu ngono vilikuwa vya juu: kifungo cha ndoa kiliheshimiwa na maisha ya familia yalikuwa safi.” Hayo ndiyo mambo yaliyowatambulisha Wakristo katika nyakati za mapema.

Alama nyingine iliyowatambulisha Wakristo wa mapema ni bidii yao katika kazi ya kuhubiri. Kristo aliwaamuru wafuasi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mathayo 28:19, 20) Jean Bernardi, profesa katika Chuo Kikuu cha Sorbonne huko Paris, Ufaransa, alisema hivi: “[Wakristo] walipaswa kwenda na kuzungumza na kila mtu kila mahali. Kwenye barabara kuu na katika majiji, kwenye viwanja vya watu wote na ndani ya nyumba. Wakaribishwe au wasikaribishwe. Kwa maskini, na kwa matajiri waliokuwa na mali nyingi. . . . Walihitaji kusafiri kwenye barabara, kwenye meli ili kwenda kwenye miisho ya dunia.”

Ukristo wa Kweli Leo

Wakristo wa kweli leo wanapaswa kuwa tofauti katika njia yao ya maisha, kama tu wenzao walivyokuwa katika karne ya kwanza. Kupatana na hilo, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuishi kulingana na kanuni zilizowekwa na Wakristo wa mapema. Watu wengine huona jitihada zao za kuishi kulingana na mafundisho ya Biblia.

Kwa mfano, kitabu New Catholic Encyclopedia kinasema wazi kwamba Mashahidi wa Yehova wanajulikana kuwa “moja kati ya vikundi vyenye mwenendo bora zaidi ulimwenguni.” Gazeti Deseret News la Salt Lake City, huko Utah, lilisema kwamba Mashahidi wa Yehova “huwa na familia zenye umoja na hutokeza raia wenye bidii na wanyoofu.” Gazeti hilo liliongeza hivi: “Washiriki wake hufuata sheria thabiti ya maadili. Wao wanaamini kwamba kuvuta sigara, kunywa kupita kiasi, kutumia dawa za kulevya, kucheza kamari, ukosefu wa adili katika ngono, na kufanya ngono na watu wa jinsia moja ni mazoea yanayoharibu hali ya kiroho. Wao huwafundisha watu kuwa wanyoofu na kufanya kazi kwa bidii.”

Pia Mashahidi hutambua kwamba wana daraka la kuhubiri kwa bidii. Likizungumza kuhusu jambo hilo kitabu New Catholic Encyclopedia kinasema: “Jukumu la msingi la kila mshiriki . . . ni kutoa ushahidi kumhusu Yehova kwa kutangaza kuhusu Ufalme Wake unaokaribia. . . . Ili kuwa Shahidi wa kweli lazima mtu ahubiri kwa matokeo kwa njia moja au nyingine.”

Kwa wazi, kuwa Mkristo wa kweli kunahusisha mengi zaidi ya kuwa mshiriki wa dini moja kati ya dini nyingi za Jumuiya ya Wakristo. Yesu mwenyewe alitabiri kwamba Wakristo wa uwongo wangetokea. (Mathayo 7:22, 23) Mashahidi wa Yehova wanakukaribisha ujifunze mambo ambayo Yesu alifundisha na kuyafuata. Hilo ndilo linalomaanishwa na kuwa Mkristo. Yesu alisema: “Ikiwa mnajua mambo haya, wenye furaha ni ninyi ikiwa mnayatenda.”—Yohana 13:17.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Yesu alisema rafiki zake ni nani?Yohana 15:14.

▪ Wakristo wanapaswa kuepuka mwenendo gani?Wagalatia 5:19-21.

▪ Wakristo wanapaswa kushiriki katika kazi gani?Mathayo 28:19, 20.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kamusi moja inamfafanua Mkristo kuwa mtu anayemwamini Yesu kuwa Kristo au anayefuata dini inayotegemea maisha na mafundisho ya Kristo.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Wakristo wa kweli huhubiri kwa bidii, kama Wakristo wa karne nyingi zilizopita walivyofanya