Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitu Ambacho Kinadumu Kuliko Sanaa

Kitu Ambacho Kinadumu Kuliko Sanaa

Kitu Ambacho Kinadumu Kuliko Sanaa

Simulizi la Rakel Koivisto

Pendekezo nililotoa mwaka wa 1950 kwa ajili ya kujengwa kwa mnara wa kuwakumbuka waliokufa katika Vita vya Pili vya Ulimwengu lilishinda mashindano ya kitaifa. Lakini sikuwapo mwaka mmoja baadaye katika sherehe ya kuuzindua rasmi mnara huo mkubwa wa mawe ya matale huko Tuusula, Finland. Acha nieleze sababu.

NILIZALIWA mnamo 1917, nikiwa kitindamimba katika familia ya watoto nane, nasi tuliishi katika kijiji cha mashambani kusini mwa Finland. Ingawa tulikuwa maskini, nilijihisi nikiwa salama na mwenye furaha. Wazazi wangu walikuwa wenye kutegemeka na wacha Mungu, nao walitufundisha kuthamini mambo ya kiroho. Biblia ambayo baba alikuwa amenunua ilithaminiwa sana nyumbani kwetu.

Nilipokuwa mtoto, nilichonga vinyago vya mbao. Watu wa ukoo waliona vinyago hivyo kuwa vya pekee, hivyo walinitia moyo nijifunze sanaa. Baada ya muda, maombi yangu ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Sanaa ya Viwanda huko Helsinki yalikubaliwa. Shule hiyo ya watu wenye vipaji iliyo kitovu cha sanaa ya Finland, ilikuwa yenye kuvutia sana kwa msichana aliyetoka vijijini, nami nikajihusisha sana na masomo. Nilipohitimu mnamo 1947, nilifikiri kwamba ningeweza kutengeneza kitu fulani cha kudumu ulimwenguni.

Mambo Yabadilika

Kisha miradi yangu ikabadilika ghafula. Siku moja, dada yangu Aune alinijia na kuniambia hivi kwa msisimko, “Nimeipata kweli!” Alikuwa amepata kitabu “Mungu na Awe wa Kweli,” kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Jambo hilo halikunisisimua. Muda mfupi baadaye, niligundua kwamba mwanafunzi mwenzangu alikuwa na kitabu hichohicho. Nilipokifanyia mzaha, msichana huyo alisema hivi kwa ukali: “Acha kucheka! Kitabu hiki kitakusaidia kuielewa Biblia.” Nilichukua kitabu hicho na kukisoma chote mara moja. Sikukicheka tena; kwa kweli, nilisadikishwa kwamba Mashahidi wana ukweli. Pia nilitambua kwamba Yehova Mungu alikuwa akinipa kitu ambacho sanaa haingeweza kunipa, yaani, uzima wa milele.

Nilipofahamiana na Mashahidi, hawakunialika kwenye mikutano yao. Hivyo, nikafikiri kwamba ilihudhuriwa tu na washiriki. Kwa hiyo, nikaamua kuuliza ikiwa ningeweza kuhudhuria mikutano hiyo. Nilifurahi kujua kwamba mtu yeyote anaweza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Kuhudhuria mikutano kuliimarisha imani yangu, nami nikaamua kujiweka wakfu kwa Yehova. Nilionyesha wakfu wangu hadharani mnamo Novemba 19, 1950 (19/11/1950), siku ambayo mimi na dada yangu tulibatizwa. Tulifurahi zaidi wakati dada zetu wengine wanne na wazazi wetu wapendwa walipokuwa Mashahidi.

Nichague Kazi Gani?

Nilipokuwa nikijifunza Biblia na Mashahidi, bado nilikuwa ninaendelea na usanii. Nilipohitimu kutoka shule ya sanaa, nilifanya kazi nikiwa msaidizi wa profesa wa sanaa za kuchongwa. Kisha, kama ilivyotajwa mwanzoni mwa makala hii, pendekezo langu kwa ajili ya mnara wa kuwakumbuka waliokufa katika Vita vya Pili vya Ulimwengu lilishinda katika mashindano ya kitaifa. Kichwa nilichopendekeza, “Hawatarudi Tena” kilionyesha maoni yangu yaliyobadilika kuhusu vita. (Isaya 2:4; Mathayo 26:52) Sikuwapo wakati wa kuzinduliwa kwa mnara huo ulio na urefu wa zaidi ya mita 5 kwa kuwa sherehe hiyo ilikuwa ya kizalendo na ilipingana na imani yangu inayotegemea Biblia.

Sifa yangu kama msanii ilipoendelea kukua nami nilijulikana sana, na watu walitaka kunipa kazi nzuri. Hata hivyo, nilichunguza mambo ninayotanguliza maishani. Ingawa nilipenda kazi yangu, tamaa yangu ya kuwasaidia wengine kiroho ilikuwa yenye nguvu zaidi. Hiyo ndiyo sababu mnamo 1953, nilianza kutumika nikiwa painia, kama wanavyoitwa wahubiri wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova.

Wakati mwingine niliambiwa kwamba ninapoteza kipawa changu. Lakini nilitambua kwamba mafanikio yoyote ya kibinafsi ambayo ningepata nikiwa kama msanii yangekuwa ya muda tu. Hata minara iliyochongwa kwa mawe ya matale hatimaye huvunjika. Hata hivyo, nikiwa painia ningeweza kutumia muda wangu mwingi kuwasaidia wengine wapate tumaini la uzima wa milele! (Yohana 17:3) Lakini, sikuacha usanii. Mara kwa mara niliendelea kuchonga vinyago vidogo ili kujifurahisha na pia kujiruzuku.

Nahamia Vijijini

Mnamo 1957, baada ya kufanya upainia kwa miaka minne huko Helsinki, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Finland iliniomba nitumike huko Jalasjärvi, eneo la vijijini lililoko katika eneo la Kusini la Ostrobothnia. Nilipaswa kujiunga na Anja Keto, ambaye nimemzidi umri kwa miaka 17. Ingawa sikumjua Anja, nilikubali mgawo huo na tukaanza kuishi pamoja. Mimi na yeye ndio tuliokuwa Mashahidi pekee katika eneo hilo, kwa hiyo karibu kila wakati tulihubiri pamoja. Muda si muda, tukawa marafiki wa chanda na pete.

Kuhamia huko Jalasjärvi kulimaanisha kwamba nijifunze tena kuishi maisha ya vijijini kama nilivyokuwa nimezoea kabla ya kuanza kusomea usanii kwenye jiji kuu miaka 20 iliyotangulia. Hali ilikuwa ngumu sana wakati wa majira ya baridi kali, na nyakati nyingine tulihitaji kutembea kwenye theluji iliyofika hadi kwenye mapaja yetu. Tuliishi katika nyumba ndogo ya mbao ambayo haikuwa nzuri sana. Tulichota maji kutoka kwenye chemchemi iliyokuwa karibu, na mara kwa mara maji tuliyoteka na kuweka ndani ya nyumba yetu yaliganda usiku. Lakini tulikuwa na kila kitu tulichohitaji. (1 Timotheo 6:8) Hizo zilikuwa siku zenye furaha sana zilizokuwa na shughuli nyingi.

Mengi ya Kufanya Katika Kazi Yenye Kuthawabisha

Mwanzoni, jitihada zetu hazikuonekana kuwa na matokeo kwa sababu wenyeji wa eneo hilo walitubagua sana. Ili kuwasaidia waelewe kazi yetu, tulipanga kuwaonyesha sinema zilizotayarishwa na Mashahidi wa Yehova, kama vile The New World Society in Action na The Happiness of the New World Society. Sinema hizo ziliwasaidia kutuelewa na kuelewa tengenezo letu, na hivyo kuona jinsi utendaji wetu unavyowafaidi watu ulimwenguni pote. Watu wengi walihudhuria maonyesho hayo.

Kwenye pindi fulani, Eero Muurainen, mwangalizi anayesafiri wa Mashahidi wa Yehova, alionyesha sinema The New World Society in Action katika ukumbi wa starehe wa eneo hilo. Ukumbi huo ulijaa sana watu hivi kwamba ilikuwa shida kupata nafasi katika kona niliyosimama. Ilinibidi kusimama kwa mguu mmoja nikiegemea ukutani kwani ule mguu mwingine haukuwa na mahali pa kukanyaga. Sinema hiyo ilipokwisha, watu wengi walitujia na kutuomba tuwatembelee.

Pia tulitumia redio kubwa kucheza hotuba za Biblia katika nyumba za mashambani. Pindi moja, tulikubali kucheza hotuba fulani saa moja jioni katika nyumba ya familia moja, nasi tulikuwa tumekaribisha kijiji kizima. Mapema asubuhi hiyo, tuliondoka kwa baiskeli zetu tukahubiri katika kijiji kilichokuwa umbali wa kilomita 25 hivi, tukifikiri kwamba tungerudi kabla ya jioni. Lakini wakati wa kurudi, barabara zilikuwa zimejaa matope kwa sababu ya mvua iliyonyesha.

Mwishowe, baiskeli zetu zilijaa matope hivi kwamba magurudumu hayangeweza kuzunguka na hivyo tukalazimika kuzibeba hadi nyumbani. Kwa sababu hiyo, hatungeweza kutoka nyumbani kwa ajili ya mkutano tuliopangia hadi baadaye usiku. Tulibeba redio yetu nzito na kufika huko mwendo wa saa nne usiku. Tulikuwa na hakika kwamba kila mtu alikuwa ameondoka. Lakini tulishangaa kukuta nyumba imefurika wanakijiji wakitusubiri! Baada ya hotuba hiyo, mazungumzo yenye kusisimua yalianza. Mwishowe tulipofika nyumbani usiku wa manane, tulikuwa tumechoka sana lakini tulikuwa na furaha tele!

Umbali kutoka kijiji kimoja hadi kingine ulikuwa mrefu sana hivi kwamba Mashahidi katika eneo hilo walitusaidia kununua gari fulani la zamani lililotengenezewa Urusi. Hilo lilifanya kazi yetu ya kuhubiri iwe rahisi. Baada ya muda, gari hilo likawa limejulikana sana hivi kwamba askofu wa dayosisi alipozuru, aliwaambia waumini wasitukaribishe katika nyumba zao. Alizungumza kuhusu wanawake wawili walio na gari la bluu. Mara moja maonyo hayo yakawachochea watu. Walitaka kujua wanawake hao wawili walikuwa akina nani na kilichowafanya kuwa hatari! Udadisi wao ulitusaidia kuwa na mazungumzo mazuri ya Biblia. Maneno ya nabii Isaya yalithibitika kuwa kweli: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa.”—Isaya 54:17.

Baada ya muda, kazi yetu ilizaa matunda. Tulianza kuongoza mikutano ya kila juma na kikundi kidogo cha watu wanaopendezwa. Mwishowe kikundi chetu kiliongezeka, na katika mwaka wa 1962 kutaniko lenye Mashahidi 18, wengi wao wakiwa wanawake, lilianzishwa. Miaka miwili baadaye, mimi na Anja tulihamishwa hadi mji wa Ylistaro katika eneo hilohilo.

Eneo Lenye Kuchochea

Tulifurahia sana mandhari ya vijijini iliyokuwa maridadi na tulivu katika mgawo huo mpya, lakini tulipendezwa hasa na watu wa huko. Kwa ujumla, walikuwa wakarimu na wenye urafiki. Ni kweli kwamba, wengi wao walikuwa watu wa dini sana na wazalendo, na nyakati nyingine walitufokea kwa ukali; lakini kuna wengine walioistahi sana Biblia. Mara nyingi tulipotoa Biblia, wanawake waliacha kazi zao za nyumbani ili wasikilize na wanaume walivua kofia zao, kofia ambazo kwa kawaida hazingevuliwa hata kidogo. Nyakati nyingine tulipojifunza Biblia, nyumba nzima, na hata majirani, wangekuja na kusikiliza.

Watu wanyoofu niliokutana nao katika utumishi walichochea usanii wangu. Nilipokuwa na wakati, ningechukua udongo na kuanza kuufinyanga. Kwa kuwa mimi huvutiwa hasa na sifa za wanadamu zenye uchangamfu na zinazofurahisha, vitu vingi nilivyotengeneza vilihusiana na watu. Vingi vilionyesha wanawake wakifanya kazi zao. Makala moja ya gazeti ilisema hivi kuhusu vitu nilivyotengeneza: “Mtu anapotazama sanaa hizo anahisi amani na usalama, na pia ucheshi na utulivu . . . Kupendezwa sana na watu pamoja na ustadi wa kisanii ndio humsaidia kutokeza sanaa hizo.” Hata hivyo, nilijitahidi sana nisikengeushwe na sanaa. Nilishikamana na uamuzi wangu wa kumtumikia Yehova wakati wote.

Mnamo 1973, nilipewa kazi ambayo singeweza kukataa. Niliombwa nitengeneze sanaa kubwa kwa kutumia udongo kwa ajili ya eneo la mapokezi la ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Finland huko Vantaa. Andiko la Zaburi 96:11-13 lilichaguliwa kuwa kichwa cha sanaa hiyo. Nilifurahi kama nini kutumia kipawa changu kumsifu Yehova!

Kwa kuwa nilifanya kazi ya usanii hasa kwa ajili ya kujifurahisha tu nilipokuwa nikifanya upainia, nilishangaa sana katika miaka ya mwishomwisho ya 1970 nilipokabidhiwa malipo ya uzeeni ya wasanii. Bila shaka, nilithamini kupata utegemezo huo wa kifedha, lakini nilijiuliza, ‘Je, ni hili tu ambalo ningekuwa nimetimiza ikiwa ningetumia maisha yangu katika sanaa? Yaani ningepata pesa kidogo tu za kunitegemeza baada ya kustaafu?’ Malipo hayo yalikuwa kitu kidogo tu yanapolinganishwa na thawabu ya uzima wa milele!—1 Timotheo 6:12.

Narudi Jijini

Mwaka wa 1974 ulileta mabadiliko makubwa katika maisha na utumishi wetu. Tulipewa mgawo mpya katika jiji kubwa la Turku. Wakati huo nyumba nyingi za ghorofa zilikuwa zikijengwa katika eneo hilo hivyo kukawa na uhitaji wa wahubiri wa Ufalme kwa kuwa watu wengi walihamia huko. Mwanzoni, hatukufurahia sana mgawo wetu mpya katika jijini hilo. Ilikuwa vigumu kuwahubiria wakaaji wa jijini kwani wengi wao hawakujali. Lakini polepole tulianza kuzoea eneo hilo jipya, na tuliwapata wengi ambao walithamini kweli za Biblia.

Mimi na Anja tumepata pendeleo la kusaidia zaidi ya watu 40 kuweka maisha yao wakfu kwa Yehova. Watoto hao wa kiroho hutuletea shangwe nyingi sana! (3 Yohana 4) Katika miaka ya karibuni afya yangu imezorota, lakini nimehisi zaidi utegemezo wa Yehova, upendo wa kutaniko, na “msaada wenye kunitia nguvu” kutoka kwa Anja, painia mwenzangu mpendwa. (Wakolosai 4:11; Zaburi 55:22) Nilipokutana na Anja karibu miaka 50 iliyopita, sidhani kama kuna yeyote kati yetu aliyefikiri kwamba tungeendelea kufanya upainia pamoja maisha yetu yote.

Kulingana na msemo mmoja maarufu, “Maisha ni mafupi lakini sanaa ni ya milele.” Hata hivyo, maneno hayo hayajawahi kuniongoza. Ninakubaliana na maneno ya mtume Paulo katika 2 Wakorintho 4:18: “Vitu vinavyoonekana ni vya muda, lakini vitu visivyoonekana ni vya milele.” Shangwe yote niliyopata kutokana na usanii, yaani, “vitu vinavyoonekana,” imekuwa ya muda. Haiwezi kamwe kulinganishwa na shangwe ambayo nimepata katika utumishi wa Yehova, na haiwezi kunipa uzima wa milele. Ninafurahi sana kwamba nilitumia maisha yangu kwa ajili ya “vitu visivyoonekana,” vitu vinavyodumu zaidi kuliko sanaa!

[Picha katika ukurasa wa 19]

Nikitengeneza sanaa ya mawe ya matale

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nikiwa na Anja (kushoto), 1957

[Picha katika ukurasa wa 22]

Nikiwa na Anja (kulia) leo