Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuzorota kwa Maadili Ulimwenguni Pote

Kuzorota kwa Maadili Ulimwenguni Pote

Kuzorota kwa Maadili Ulimwenguni Pote

“KILA mahali watu hudanganya,” anasema David Callahan, ambaye aliandika kitabu kuhusu mazoea ya watu kudanganya (The Cheating Culture) kilichotolewa hivi majuzi. Baadhi ya mambo anayotaja ambayo yanafanyika nchini Marekani ni, “wanafunzi wa sekondari na vyuo vikuu kuiba mitihani,” kutoa nakala za muziki na filamu bila idhini, “wizi kazini,” “ulaghai wa hali ya juu katika huduma za afya,” na kutumia dawa za kuongeza nguvu katika michezo. Anakata kauli hivi: “Mambo hayo yote pamoja na ukiukaji wa haki na sheria yanaonyesha kwamba maadili yamezorota sana.”

Gazeti The New York Times lilisema kwamba Tufani Katrina, ambayo ilikumba Marekani mwishoni mwa mwaka wa 2005, “ilitokeza mojawapo ya mbinu za ulaghai na mipango ya hila ya hali ya juu na maamuzi ya kipumbavu sana yaliyosababisha matumizi mabaya sana ya pesa za serikali katika nyakati za kisasa.” Seneta mmoja nchini Marekani alisema: “Ilishangaza sana kuona ulaghai huo wa wazi, ujasiri uliohusika kufanya mipango hiyo ya hila, na matumizi mabaya sana ya pesa za serikali.”

Bila shaka, bado kuna watu wasio na ubinafsi wanaoonyesha fadhili za kibinadamu. (Matendo 27:3; 28:2) Lakini mara nyingi tunawasikia watu wakisema: “Nitafaidikaje?” Inaonekana kwamba mtazamo wa ubinafsi na kujitanguliza ndio unaotawala.

Inasemekana kwamba wakati uliopita, ubinafsi na ukosefu mbaya sana wa maadili ulichangia kuporomoka kwa milki mbalimbali, kama vile Milki ya Roma. Je, mambo yanayotendeka sasa yanaweza kuwa dalili ya tukio kubwa zaidi? Je, si wazi kwamba ulimwengu mzima unaathiriwa na “kuongezeka kwa uasi-sheria,” ambao Biblia ilitabiri kuwa ungeonyesha mwisho wa mfumo huu wa mambo unakaribia?—Mathayo 24:3-8, 12-14; 2 Timotheo 3:1-5.

Hali Inazidi Kuzorota Ulimwenguni Pote

Likiripoti kuhusu “warsha juu ya kutendewa vibaya kingono na ponografia (picha au habari za ngono)” katika maeneo ya mabanda ya sehemu moja nchini Uganda, gazeti Africa News la Juni 22, 2006 (22/6/2006) lilisema kwamba “uzembe wa wazazi umefanya ukahaba na matumizi ya dawa za kulevya kuongezeka katika eneo hilo.” Gazeti hilo lilisema: “Ofisa anayesimamia Kitengo cha Ulinzi wa Watoto na Familia katika Kituo cha Polisi cha Kawempe, Bw. Dhabangi Salongo, alisema kwamba visa vya watoto kutendewa vibaya na jeuri nyumbani vimeongezeka sana.”

Daktari mmoja nchini India alisema kwamba “jamii inapoteza misingi yake ya kitamaduni.” Mwelekezaji mmoja wa filamu nchini humo alisema kwamba “kuongezeka kwa matumizi ya dawa za kulevya na ukosefu wa maadili katika ngono ni ishara nyingine inayoonyesha kwamba India inazama katika ‘upotovu wa maadili kama ule wa nchi za Magharibi.’”

Hu Peicheng, katibu-mkuu wa Shirika la Mambo ya Jinsia na Kujamiiana la China huko Beijing, alisema hivi: “Zamani katika jamii, tulijua kutofautisha lililo sawa na lililo kosa. Sasa tunaweza kufanya chochote tutakacho.” Makala moja katika gazeti China Today ilieleza hivi: “Siku hizi jamii inazidi kukubali ngono nje ya ndoa.”

Hivi karibuni, Gazeti Yorkshire Post lilisema: “Inaonekana kwamba watu wanapenda kuonyesha uchi wao katika programu za televisheni na makampuni ya biashara hutumia programu hizo ili kuuza bidhaa zao. Miaka fulani iliyopita, programu kama hizo zingezua kasheshe. Leo, tunazungukwa na picha nyingi chafu kutoka kila mahali na ponografia . . . imekubaliwa na jamii.” Gazeti hilo liliongeza kusema: “Habari ambazo wakati mmoja zilionekana kuwa zinafaa tu watu walio na umri wa zaidi ya miaka 18, leo huonwa kuwa zinafaa watu wote, na kulingana na maoni ya wanaopinga ponografia, habari hizo zinawalenga hasa watoto.”

Gazeti The New York Times Magazine lilisema hivi: ‘Baadhi ya vijana huzungumza kuhusu jinsi walivyofanya ngono kama tu wanavyozungumza kuhusu chakula watakachokula.’ Gazeti Tweens News, ambalo hutoa mwongozo kwa ajili ya wazazi walio na watoto wenye umri wa miaka 8 hadi 12, lilisema hivi: “Kwa mwandiko wa kitoto, msichana mmoja alikuwa ameandika ujumbe huu wenye kuhuzunisha sana: ‘Mama yangu ananilazimisha niwe na marafiki wa kiume na nifanye ngono. Nina umri wa miaka 12 tu . . . jamani nisaidieni!’”

Mambo yamebadilika sana. Gazeti Toronto Star la Kanada lilisema kwamba miaka michache iliyopita “wazo tu la watu wa jinsia moja kuishi pamoja waziwazi lingezua kasheshe.” Hata hivyo, Barbara Freemen, mwalimu wa historia ya jamii katika Chuo Kikuu cha Carleton, Ottawa, anasema: “Leo watu wanasema, ‘Maisha yangu ya faragha ni yangu tu. Mtu hapaswi kuyaingilia.’”

Kwa wazi, katika miongo michache iliyopita, maadili yamezorota haraka katika sehemu nyingi ulimwenguni. Ni nini kimesababisha mabadiliko hayo makubwa? Wewe binafsi unahisije kuhusu mabadiliko hayo? Na mabadiliko hayo yanaonyesha nini kuhusu wakati ujao?