Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa nini mimi hulinganishwa na wengine?

Kwa nini mimi hulinganishwa na wengine?

Vijana Huuliza . . .

Kwa nini mimi hulinganishwa na wengine?

“Mimi hukasirika sana wazazi na walimu wangu wanaponilinganisha na wengine.”—Mia. *

“Ninapolinganishwa, mimi hujihisi sifai kwa sababu tayari mimi huwa nimetamani kuwa kama mtu yule ninayelinganishwa naye.”—April.

SHULENI, mwalimu wako anakukemea kwa sababu huelewi hesabu kama mwanafunzi mwenzako. Nyumbani mzazi anakufokea kwa sababu wewe si nadhifu kama dada yako. Mtu fulani anakuambia, “Mama yako alikuwa mrembo sana alipokuwa na umri kama wako!” Maneno hayo ni yenye kuchoma kwani yanakufanya ujiulize ikiwa mtu huyo anaona una sura mbaya. Nyakati nyingine unahisi utalipuka hivi: “Kwani watu hawanioni mimi?” “Kwa nini kila mara ninalinganishwa na mtu mwingine?”

Kwa nini mtu huumia sana anapolinganishwa na wengine? Je, kuna manufaa yoyote ya kulinganishwa na wengine? Utafanyaje watu wanapokulinganisha na wengine?

Kwa Nini Kulinganishwa Kunaumiza?

Sababu inayofanya kulinganishwa kuumize ni kwamba mara nyingine unaguswa moja kwa moja. Labda kile ambacho watu wanasema ndicho ambacho wewe huwa unajiambia. Kwa mfano, Becky anakiri hivi: “Ningewaangalia watoto wanaopendwa na wengi shuleni na kujiambia, ‘Laiti ningekuwa kama wao, watu wengi wangenipenda.’”

Ni nini kinachosababisha hisia hizo? Fikiria mabadiliko unayopitia kimwili, kihisia, na kiakili. Huenda mwili wako unabadilika haraka. Inakuwa vigumu kudumisha uhusiano wako na wazazi. Labda mtazamo wako kuelekea watu wa jinsia tofauti umebadilika sana. Hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Je, mabadiliko haya ni ya kawaida?’

Huenda ukafikiria kwamba njia pekee itakayokusaidia ni kujilinganisha na vijana wengine wanaopitia hali kama zako. Na huo ni mtego! Ukiona ni kana kwamba wanakabiliana na hali zao kwa njia nzuri zaidi, unakuwa na wasiwasi. Kisha mtu fulani mwenye umri mkubwa anapokuuliza, ‘Kwa nini usiwe kama fulani?’ huenda ukahisi kwamba una kasoro!

April anataja sababu nyingine inayoweza kufanya kulinganishwa kuumize. “Watu wanapokulinganisha na mtu mwingine,” anasema, “hasa mtu wa karibu, unaweza kuanza kumwonea wivu au hata kuwa na kinyongo.” Mia anaelewa hali hiyo. Ni kana kwamba sikuzote wazazi na walimu wake humlinganisha na dada yake mkubwa. “Wao huniambia kuhusu mambo yote aliyofanya alipokuwa na umri wangu,” anasema Mia. Anahisije? “Mimi huhisi ni kama ninashindana na dada yangu. Nyakati nyingine mimi humchukia.”

Kwa kweli kulinganishwa kunaweza kuwa na matokeo mabaya. Fikiria kilichotukia kwa waandamani wa karibu wa Yesu. Jioni ya mwisho kabla ya kifo cha Yesu, ‘kulitokea bishano kali’ kati ya mitume wake. Kwa nini? Walikuwa wakijilinganisha na kubishana “juu ya ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mkuu zaidi ya wote.” (Luka 22:24) Bila shaka, nyakati nyingine watu wanapolinganishwa matatizo yanaweza kutokea. Lakini je, hilo linamaanisha watu hawapaswi kulinganishwa kamwe?

Kulinganishwa Kunakofaa

Fikiria kisa cha Danieli na waandamani wake watatu Waebrania, kinachosimuliwa katika Biblia. Vijana hao hawakutaka kula vyakula vitamu vya mfalme wa Babiloni vilivyokatazwa katika sheria ya Mungu. (Mambo ya Walawi 11:4-8) Ili kumsadikisha mlinzi wao awasaidie, Danieli alipendekeza wajaribiwe. Alipendekeza kwamba baada ya kula chakula kilichokubaliwa katika Sheria ya Mungu kwa siku kumi, mlinzi huyo awalinganishe vijana hao Waebrania na vijana wale wengine. Matokeo yakawaje?

Biblia inaeleza: “Mwishoni mwa zile siku kumi, sura [za Waebrania hao] zikaonekana kuwa bora na zilizonenepa kuliko za wale watoto wote waliokuwa wakila vyakula vitamu vya mfalme.” (Danieli 1:6-16) Ona kwamba hawakupata matokeo mazuri kwa sababu Danieli na waandamani wake walikuwa na sifa fulani za kipekee kuliko vijana wale wengine. Badala yake, ilikuwa hasa kwa sababu vijana hao Waebrania walichagua kutii sheria ambazo Mungu alikuwa amewapa watu wake.

Je, hali ya vijana hao Waebrania inaweza kufanana na yako? Ukiishi kupatana na kanuni za maadili za Biblia, utakuwa tofauti na vijana wengine. Huenda watu fulani wanaoona tofauti hizo wakashangaa na ‘kuendelea kukutukana.’ (1 Petro 4:3, 4) Hata hivyo, wengine wataona matokeo mazuri ya mwenendo wako mzuri, na huenda hata wakachochewa kujifunza kumhusu Yehova. (1 Petro 2:12) Katika hali hiyo, kulinganishwa na wengine kunaweza kufaa.

Pia, kulinganishwa na wengine kunaweza kuwa na manufaa mengine. Kwa mfano, huenda wewe ukahisi kwamba unatimiza sehemu yako ya kazi za nyumbani, hasa unapojilinganisha na ndugu au dada yako. Hata hivyo, huenda wazazi wako wasiwe na maoni kama yako. Ili wakusaidie kubadili maoni yako, wanaweza kutumia mfano wa Biblia na kukuuliza ulinganishe mtazamo na matendo yako na ya mtu fulani anayetajwa katika Biblia.

Kwa mfano, wanaweza kukukumbusha kwamba ingawa Yesu aliitwa Bwana na Mwalimu, aliosha miguu ya wanafunzi wake kwa hiari. (Yohana 13:12-15) Wanaweza kukutia moyo uige mtazamo wa unyenyekevu na bidii ambao Yesu alikuwa nao. Kwa kweli, Biblia inawatia moyo Wakristo wote, vijana kwa wazee, wajilinganishe kila wakati na Kristo na wajaribu ‘kufuata hatua zake kwa ukaribu.’ (1 Petro 2:21) Kujilinganisha kwa njia hiyo hutufanya tuwe wanyenyekevu na kutusaidia kusitawisha utu unaompendeza Yehova.

Unapolinganishwa Isivyofaa

Kusema kweli, inaweza kuumiza na kuvunja moyo unapolinganishwa isivyofaa na ndugu au dada yako au kijana mwenzio. Unaweza kukabilianaje na hali hiyo? “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake,” akasema Mfalme Sulemani. (Methali 19:11) Ufahamu unaweza kukusaidiaje? Labda mzazi au mwalimu anayekulinganisha na mwingine anakujali hata ingawa huenda wewe usidhani hivyo. “Mtu anaponilinganisha na wengine,” anasema Cathy, “mimi hujiuliza, ‘anataka kunisaidiaje?’” Cathy amegundua kwamba kuwa na mtazamo mzuri kunamsaidia asivunjike moyo au kukasirika.

Vipi ukihisi kwamba sikuzote unalinganishwa na wengine? Kwa mfano, huenda mzazi wako anapenda kukulinganisha isivyofaa na mmoja wa ndugu au dada zako. Labda unaweza kuzungumza na mzazi wako kwa heshima na kumweleza jinsi unavyohisi unapolinganishwa hivyo. Inawezekana hajatambua jinsi unavyoathiriwa unapolinganishwa kwa njia hiyo.

Hata hivyo, kumbuka kwamba kuna “wakati wa kusema” lakini pia kuna “wakati wa kukaa kimya.” (Mhubiri 3:7) Badala ya kulipuka kwa hasira unapolinganishwa tena, subiri hadi utulie, kisha uzungumze na mzazi wako au yule aliyekulinganisha isivyofaa. Ukifanya hivyo, maneno yako yatakuwa yenye kushawishi.—Methali 16:23.

Mara nyingi, kutambua sifa zako nzuri kunaweza kupunguza maumivu yanayotokana na kulinganishwa isivyofaa. Mtume Paulo alimwambia Timotheo: “Usiache mtu yeyote audharau kamwe ujana wako.” (1 Timotheo 4:12) Timotheo alikuwa kijana kwa kiasi fulani alipowekwa rasmi kuwa mwangalizi Mkristo. Kwa hiyo, labda wengine walikuwa wakimlinganisha isivyofaa na wanaume wengine wenye umri mkubwa na uzoefu zaidi. Lakini hakukuwa na msingi wa kumlinganisha kwa njia hiyo. Ingawa alikuwa kijana, Timotheo alipata uzoefu aliposafiri na Paulo. Timotheo alijua jinsi ya kulitumia Neno la Mungu kwa njia inayofaa. Naye aliwajali kikweli ndugu na dada zake wa kiroho.—1 Wakorintho 4:17; Wafilipi 2:19, 20.

Kwa hiyo, wakati mwingine mtu anapokulinganisha isivyofaa, jiulize, ‘Je, uchambuzi huo una msingi?’ Ikiwa kuna ukweli fulani katika jambo uliloambiwa, jaribu kujifunza kutokana nalo. Hata hivyo, ukilinganishwa kwa jumla tu, kwa maneno kama vile, “Kwa nini huwezi kuwa kama ndugu yako?” jaribu kuelewa kwa nini mtu huyo amesema maneno hayo. Jaribu kufikiria namna unavyoweza kutumia maneno hayo kwa manufaa.

Yehova Mungu hapimi thamani yako kwa kukulinganisha na mwanadamu mwingine asiyekamilika. (Wagalatia 6:4) Yeye hatazami tu sura ya nje bali anaelewa moyo wako ulivyo. (1 Samweli 16:7) Kwa kweli, Yehova haoni tu sifa ulizo nazo bali yeye huona pia sifa unazojaribu kusitawisha. (Waebrania 4:12, 13) Yeye hatazamii kwamba hutafanya makosa bali yeye huangalia sifa zako nzuri. (Zaburi 130:3, 4) Kujua tu mambo hayo kunaweza kukusaidia unapolinganishwa na wengine.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Wewe hukasirika unapolinganishwa kwa njia gani?

▪ Ikiwa sikuzote wazazi wako hukulinganisha na wengine, unaweza kukabilianaje na hali hiyo?

[Blabu katika ukurasa wa 12]

“Ningependa mtu anayenishauri asinilinganishe na mtu mwingine na kuniambia, ‘Kwa nini usiwe kama fulani,’ lakini, kwanza aniambie sifa zangu nzuri kisha kwa njia ya upendo anisaidie kuona udhaifu wangu.”—Natalie

[Picha katika ukurasa wa 13]

Huenda ikafaa kueleza kwa njia yenye heshima jinsi unavyohisi unapolinganishwa