Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ulimwengu Huu Unaelekea Wapi?

Ulimwengu Huu Unaelekea Wapi?

Ulimwengu Huu Unaelekea Wapi?

BIBLIA ilitabiri zamani sana kuhusu kuzorota kwa maadili tunakoona leo na ikafafanua hali hiyo hivi: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili . . . wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake.”—2 Timotheo 3:1-5.

Huenda ukakubali kwamba unabii huo wa Biblia unafafanua vizuri hali ya ulimwengu leo. Hata hivyo, ulirekodiwa karibu miaka 2,000 iliyopita! Unabii huo unaanza kwa maneno haya: “Katika siku za mwisho.” Maneno hayo, “siku za mwisho,” yanamaanisha nini?

“Siku za Mwisho” za Nini?

Maneno “siku za mwisho” yanatumika sana siku hizi. Katika Kiingereza peke yake, maneno hayo yanatumiwa katika vichwa vya vitabu vingi sana. Kwa mfano, fikiria kitabu cha karibuni, The Last Days of Innocence—America at War, 1917-1918 (Siku za Mwisho za Kutokuwa na Hatia—Marekani Vitani, 1917-1918). Dibaji ya kitabu hicho inaeleza wazi kwamba maneno “siku za mwisho,” yanapotumiwa katika kitabu hicho, yanarejelea kipindi fulani hususa ambacho kimekuwa na upotovu mkubwa wa maadili.

Dibaji hiyo inaendelea kusema hivi: “Mnamo 1914, nchi hiyo ilikuwa ikibadilika haraka zaidi kuliko wakati mwingine wowote katika historia yake.” Kwa kweli, mnamo 1914 ulimwengu ulitumbukia katika vita ambavyo havikuwa vimewahi kutokea. Kitabu hicho kinasema: “Hivyo vilikuwa vita kamili, si vita kati ya jeshi moja na jeshi lingine, bali vita kati ya taifa moja na lingine.” Vita hivyo, kama tutakavyoona, vilitukia mwanzoni mwa kile kipindi ambacho Biblia inakiita “siku za mwisho.”

Biblia inafundisha kwamba ulimwengu utapitia kipindi hususa kinachoitwa “siku za mwisho.” Kwa kweli, Biblia inasema kwamba kulikuwa na ulimwengu ambao ulipitilia mbali au ulikwisha. Inaeleza hivi: “Ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji.” Jambo hilo lilitukia lini, na ni ulimwengu upi huo uliokwisha? Ulikuwa ‘ulimwengu wa kale wa watu wasiomwogopa Mungu’ katika siku za mtu aliyeitwa Noa. Vivyo hivyo ulimwengu wa leo utakwisha. Hata hivyo, wale wanaomtumikia Mungu wataokoka mwisho wa ulimwengu huu, kama vile Noa na familia yake walivyookoka.—2 Petro 2:5; 3:6; Mwanzo 7:21-24; 1 Yohana 2:17.

Yale Ambayo Yesu Alisema Kuhusu Mwisho

Yesu Kristo pia alizungumza kuhusu “siku za Noa” wakati ‘gharika ilikuja na kuwafagilia mbali wote.’ Alilinganisha hali zilizokuwepo kabla ya Gharika, yaani, kabla tu ya ulimwengu huo kwisha, na hali ambazo zingekuwepo katika kipindi ambacho alitaja kuwa “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3, 37-39) Tafsiri nyingine za Biblia hutumia usemi “mwisho wa dunia” au “mwisho wa nyakati.”—Union Version, Zaire Swahili Bible, na Biblia Habari Njema.

Yesu alitabiri jinsi ambavyo maisha yangekuwa duniani kabla tu ya ulimwengu kwisha. Alisema hivi kuhusu vita: “Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.” Wanahistoria wamesema kwamba hilo lilitukia kuanzia mwaka wa 1914. Hiyo ndiyo sababu dibaji ya kitabu kilichotajwa ilisema kwamba 1914 ulikuwa mwanzo wa “vita kamili, si vita kati ya jeshi moja na jeshi lingine, bali vita kati ya taifa moja na lingine.”

Katika unabii wake, Yesu aliongezea hivi: “Kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya nchi mahali pamoja baada ya pengine. Mambo yote hayo ni mwanzo wa maumivu ya taabu.” Aliendelea kusema kwamba kungekuwa na mambo mengine mengi kutia ndani “kuongezeka kwa uasi-sheria.” (Mathayo 24:7-14) Kwa kweli tumeona mambo hayo yakitukia. Leo maadili yamezorota sana hivi kwamba yanatimiza unabii wa Biblia!

Tunapaswa kuishije katika siku hizi zenye maadili yaliyopotoka? Ona yale ambayo mtume Paulo aliwaandikia Wakristo huko Roma kuhusu kuzorota kwa maadili. Alitaja kuhusu “hamu za ngono yenye kufedhehesha” ambazo watu walikuwa nazo, akisema hivi: “Wanawake wao walibadili matumizi yao wenyewe ya asili kuwa yale yaliyo kinyume cha asili; na vivyo hivyo pia hata wanaume waliacha matumizi ya asili ya mwanamke na kuwakiana tamaa kali katika uchu wao kuelekeana wao wenyewe, wanaume kwa wanaume, wakitenda mambo machafu.”—Waroma 1:26, 27.

Wanahistoria wanasema kwamba wakati huo jamii ya wanadamu ilipokuwa ikizama katika upotovu wa maadili, “Wakristo wachache waliokuwapo walisumbua dhamiri za ulimwengu huo wa kipagani uliopenda anasa kwa sababu walimcha Mungu na walikuwa na mwenendo safi kiadili.” Hilo linapaswa kutufanya tutue kidogo na kujiuliza: ‘Namna gani mimi na marafiki ninaochagua? Je, tunaonekana kuwa tofauti, wenye maadili mazuri, tofauti na wengine walio na maadili mabaya?’—1 Petro 4:3, 4.

Jambo Tunalokabiliana Nalo

Biblia inatufundisha kwamba licha ya ukosefu wa maadili unaotuzunguka, tunahitaji kuwa “wasio na hatia, watoto wa Mungu wasio na dosari katikati ya kizazi kilicho kombo na kilichopotoka.” Ili kufanya hivyo, tunahitaji “kulishika sana neno la uzima.” (Wafilipi 2:15, 16) Maneno hayo ya Biblia yanaonyesha jinsi ambavyo Wakristo wanaweza kubaki bila doa kiadili. Wanahitaji kushika sana mafundisho ya Neno la Mungu na kutambua kwamba kufuata viwango vyake vya maadili ndiyo njia bora zaidi ya maisha.

“Mungu wa mfumo huu wa mambo,” Shetani Ibilisi, anajaribu kuvuta watu upande wake. (2 Wakorintho 4:4) Biblia inatuambia kwamba ‘anaendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru.’ Wahudumu wake, yaani, wale wanaomtumikia kwa kutenda kama yeye, hufanya vivyo hivyo. (2 Wakorintho 11:14, 15) Wanawaahidi watu uhuru na furaha, lakini Biblia inasema kwamba “wao wenyewe ni watumwa wa uharibifu.”—2 Petro 2:19.

Usijidanganye. Wale wanaopuuza viwango vya maadili vya Mungu wataona cha mtema-kuni. Mtunga-zaburi alisema: ‘Wokovu uko mbali sana na waovu, kwa maana hawajayatafuta masharti ya Mungu.’ (Zaburi 119:155; Methali 5:22, 23) Je, tunakubaliana na maneno hayo? Ikiwa ndivyo, acheni tulinde akili na mioyo yetu dhidi ya propaganda zinazoendeleza maadili mapotovu.

Hata hivyo, wengi huwaza hivi kwa njia isiyo ya hekima, ‘Ikiwa jambo ninalofanya halivunji sheria basi ni sawa.’ Lakini hilo si kweli. Kwa upendo Baba yetu wa mbinguni hatoi mwongozo kuhusu maadili ili afanye maisha yako yawe yenye kuchosha na yenye vizuizi vingi bali ili akulinde. ‘Anakufundisha ili ujifaidi mwenyewe.’ Anataka uepuke matatizo na ufurahie maisha. Naam, kama vile Biblia inavyofundisha, kumtumikia Mungu ‘kuna ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.’ Huo ni “uzima ulio wa kweli,” uzima wa milele katika mfumo mpya alioahidi!—Isaya 48:17, 18; 1 Timotheo 4:8; 6:19.

Kwa hiyo, linganisha manufaa ya kufuata mafundisho ya Biblia na maumivu ambayo huwapata wale ambao hawayafuati. Kupata kibali cha Mungu kwa kumsikiliza ndiyo njia bora zaidi ya maisha! Mungu anaahidi hivi: “Kwa habari yake mtu anayenisikiliza, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.”—Methali 1:33.

Jamii Inayofuata Maadili

Biblia inasema kwamba ulimwengu huu utakapopitilia mbali, “mtu mwovu hatakuwako tena.” Pia inasema: “Kwa maana wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake.” (Zaburi 37:10, 11; Methali 2:20-22) Hivyo, mabaki yote ya ukosefu wa maadili yataondolewa duniani, kutia ndani wote wanaokataa kufuata mafundisho yanayofaa ya Muumba wetu. Paradiso ya kidunia, kama ile ambayo Mungu aliwapa wanadamu wa kwanza, hatimaye itaenezwa duniani pote na wale wanaompenda Mungu.—Mwanzo 2:7-9.

Wazia shangwe ya kuishi katika dunia kama hiyo iliyo paradiso! Kati ya wale watakaopata pendeleo la kuiona watakuwa mabilioni ya wale watakaofufuliwa. Shangilia katika ahadi za Mungu: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Ulimwengu wa wakati uliopita ulipokwisha, watu fulani wanaomwogopa Mungu waliokoka

[Picha katika ukurasa wa 10]

Ulimwengu huu utakapokwisha, dunia itakuwa paradiso