Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Maisha Yako Yameamuliwa Mapema?

Je, Maisha Yako Yameamuliwa Mapema?

Maoni ya Biblia

Je, Maisha Yako Yameamuliwa Mapema?

Asubuhi moja wanaume wawili walikuwa wakisafiri ndani ya gari pamoja kwenda kazini walipoamua kupitia njia ya mkato kwenye mtaa ambao mmoja wao alikuwa akiishi zamani. Wakiwa njiani waliona nyumba ikiwa imeshika moto. Walisimamisha gari lao na wakatumia ngazi waliyokuwa nayo kumwokoa mama na watoto wake watano. “Labda jambo hilo lilikuwa limeamuliwa mapema,” ndivyo gazeti moja lilivyoripoti kuhusu tukio hilo.

WATU wengi wanaamini kwamba chochote kinachowapata, kiwe kizuri au kibaya, kimepangwa na nguvu fulani inayozidi uwezo wao. Kwa mfano, Mrekebishaji John Calvin aliyeishi katika karne ya 16 aliandika: “Twafasili kuamuliwa kimbele yatakayompata mtu kuwa mpango wa milele wa Mungu, ambao kwa huo aliamua kile alichotaka kufanya na kila mtu. Kwani hakuwaumba wote wakiwa na hali ileile, bali huamuru kimbele wengine kupokea uhai wa milele na wengine kupokea laana ya milele.”

Je, kweli Mungu huamua mapema matendo yetu na hali yetu ya baadaye itakavyokuwa? Biblia inafundisha nini?

Dhana ya Kuamuliwa Mambo Mapema

Watu wanaoamini kwamba mambo yote yameamuliwa mapema hutoa sababu hizi: Mungu anajua kila jambo. Kwa sababu hiyo, anajua pia kitakachotukia wakati ujao. Anajua jinsi ambavyo kila mtu atatumia maisha yake, naye anajua wakati hususa na njia ambayo kila mtu atakufa. Kwa hiyo, kulingana na maoni yao, wakati unapofika wa mtu kufanya uamuzi fulani, uamuzi huo hauwezi kuwa tofauti na ule ambao Mungu alikuwa ameona na kupanga; ikiwa sivyo, basi itaonyesha Mungu hawezi kujua mambo yote. Je, unafikiri maoni hayo yanapatana na akili? Fikiria maoni hayo yanaweza kumaanisha nini.

Ikiwa nguvu fulani imeamua tayari jinsi wakati wako unaokuja utakavyokuwa, kujaribu kujilinda ni kazi bure. Kuamua kama utavuta sigara au hutavuta hakuwezi kubadili afya yako au ile ya watoto wako. Kufunga mkanda wa usalama unaposafiri kwa gari hakuwezi kuamua ikiwa utakuwa salama au la. Lakini maoni hayo yamepotoka. Takwimu zinaonyesha kwamba watu ambao huchukua tahadhari, hawapatwi na madhara mengi. Lakini kutojali kunaweza kutokeza msiba.

Fikiria maoni mengine. Ikiwa Mungu huchagua kujua kila jambo, basi hata kabla ya kuwaumba Adamu na Hawa, angeweza kujua watakosa kumtii. Lakini Mungu alipomwambia Adamu kuwa hapaswi kula matunda ya “mti wa ujuzi wa mema na mabaya” au angekufa, je, tayari alijua kwamba Adamu angekula? (Mwanzo 2:16, 17) Mungu alipowaambia: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia,” je, alijua kwamba tarajio lao zuri la kuishi katika paradiso halingefanikiwa? Bila shaka la.—Mwanzo 1:28.

Tukifikiria dhana hiyo hata zaidi, wazo la kwamba Mungu anajua mapema maamuzi yote inaweza kumaanisha yeye ndiye anayesababisha mambo yote yanayotukia, kutia ndani vita, ukosefu wa haki, na kuteseka. Je, hilo linawezekana? Jibu la wazi linaonekana kutokana na yale ambayo Mungu husema kujihusu.

“Lazima Uchague”

Maandiko yanasema kwamba “Mungu ni upendo” na pia yeye ni “mpenda haki.” Sikuzote amewasihi watu wake hivi: “Chukieni yaliyo mabaya, pendeni yaliyo mema.” (1 Yohana 4:8; Zaburi 37:28; Amosi 5:15) Mara nyingi sana amewatia moyo watu wake waaminifu wachague njia inayofaa maishani. Kwa mfano, Yehova alipofanya agano na taifa la kale la Israeli, aliwaambia hivi kupitia Musa: “Nachukua mbingu na dunia kuwa mashahidi juu yenu leo, kwamba nimeweka uzima na kifo mbele yako, baraka na laana; nawe lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako.” (Kumbukumbu la Torati 30:19) Je, Mungu alipanga mapema maamuzi ambayo kila mmoja wao angefanya? Bila shaka la.

Yoshua, kiongozi wa watu wa Mungu wa nyakati za kale, aliwasihi hivi Waisraeli wenzake: “Jichagulieni leo yule mtakayemtumikia . . . Lakini mimi na nyumba yangu, tutamtumikia Yehova.” (Yoshua 24:15) Vivyo hivyo Mungu alimsihi pia nabii Yeremia hivi: “Itii sauti ya Yehova kwa habari ya mambo ninayokuambia, na itakuwa vema kwako, na nafsi yako itaendelea kuishi.” (Yeremia 38:20) Je, Mungu anayefuata haki na mwenye upendo angewatia moyo watu wafanye yaliyo sawa wakitazamia kwamba watapata thawabu ikiwa anajua watashindwa? La. Kuwatia moyo kwa njia hiyo kungekuwa unafiki.

Kwa hiyo, unapopatwa na mambo mazuri au mabaya, si kwa sababu mambo hayo hayangeweza kuepukika. Mara nyingi, ‘matukio yasiyotazamiwa’ hutokea kwa sababu ya maamuzi ya watu wengine, iwe kwa sababu maamuzi hayo ni ya hekima au si ya hekima. (Mhubiri 9:11) Kwa kweli, wakati wako unaokuja haujaamuliwa mapema, na maamuzi yako ndiyo yanayoamua wakati wako unaokuja wa milele utakuwaje.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Je, Mungu aliamua mapema kwamba Adamu na Hawa wangetenda dhambi?Mwanzo 1:28; 2:16, 17.

▪ Ni sifa zipi za Mungu zinazoonyesha kuwa hawaamulii wanadamu mambo mapema?Zaburi 37:28; 1 Yohana 4:8.

▪ Wewe una daraka gani?Yoshua 24:15.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Takwimu zinaonyesha kwamba watu wanaochukua tahadhari hawapatwi na madhara mengi