Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Tumaini Gani kwa Maskini?

Kuna Tumaini Gani kwa Maskini?

Kuna Tumaini Gani kwa Maskini?

HAKUNA ubaya wowote wa kufanya kazi ngumu ili kupata riziki, ikiwa mtu anayefanya kazi hiyo anapata malipo yanayofaa. Ona maelezo haya ya mwandishi fulani wa Biblia: “Nimekuja kujua kwamba hakuna jambo lingine bora . . . kuliko mtu kufurahi . . . na pia kwamba kila mtu ale, naam, anywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu. Hiyo ndiyo zawadi ya Mungu.”—Mhubiri 3:12, 13.

Lakini kama tulivyoona, mfumo wa kiuchumi wa ulimwengu hutazamia watu wafanye kazi ngumu lakini wanapata malipo yasiyotosha. Wengi hubaki wakiwa maskini, waking’ang’ana na maisha kila siku. Ni nadra sana wao “kufurahi” na “kufanya mema” kwa sababu ya maisha yao. Kuna utajiri mwingi sana ulimwenguni, lakini huenda nusu ya wanadamu hawafaidiki na utajiri huo.

Mungu Anapendezwa na Maskini

Muumba wa wanadamu, Yehova Mungu, hapendezwi na hali hiyo. Yehova anawahurumia maskini. Tunasoma hivi katika Biblia: “[Mungu] hatakisahau kilio cha wenye kuteseka.” (Zaburi 9:12) Yehova ni Mungu anayewajali maskini.

Kumhusu Yehova, Biblia inasema: “Mtu mwenye taabu, mvulana asiye na baba, anajikabidhi kwako. Wewe mwenyewe umekuwa msaidizi wake.” (Zaburi 10:14) Ona jinsi mstari huo wa Biblia unavyowataja wanaoteseka kama mtu mmoja-mmoja. * Naam, Mungu humtazama kila mtu na kufikiria mahitaji yake. Kwake kila mtu ana thamani na anastahili uangalifu. Yehova anawaalika watu wote wajifunze kumhusu na wafurahie urafiki wake haidhuru hali yao ya kiuchumi.

Jambo moja ambalo watu hujifunza kutoka kwa Mungu ni kuonyesha wengine huruma na hisia-mwenzi. Mashahidi wa Yehova hujiona kuwa familia kubwa ya kiroho. Wao huthaminiana, na kati yao kuna upendo wa kweli wa Kikristo. Wakati mmoja Bwana Yesu Kristo aliwaambia hivi wafuasi wake: “Ninyi nyote ni ndugu.” (Mathayo 23:8) Kwa hiyo, wote wanaokubali ibada ya kweli wanakuwa sehemu ya undugu usiobaguana kwa misingi ya utajiri. Kila mmoja humjali mwenzake, nao hutiana moyo nyakati za taabu.

Biblia ina kanuni zinazoweza kumsaidia mtu kupunguza madhara ya umaskini. Maandiko yanaonyesha kwamba Mungu hushutumu kuchafua mwili, kama vile kwa kutumia tumbaku na kutumia kileo vibaya. (Methali 20:1; 2 Wakorintho 7:1) Mtu anayeishi kupatana na kanuni hizo huweka akiba ya pesa ambazo zingepotezwa kupitia mazoea mabaya. Yeye huepuka magonjwa yanayosababishwa na uvutaji wa sigara na ulevi, na gharama ya matibabu ambayo ingesababishwa na magonjwa hayo. Pia Biblia inawafundisha watu kukataa kufikiri kwa njia ya kimwili na pupa. (Marko 4:19; Waefeso 5:3) Mtu anapoheshimu Neno la Mungu kuhusiana na mambo hayo, yeye huepuka pia kupoteza pesa zake kwa kucheza kamari.

Biblia hutoa kanuni zinazotusaidia kuishi vizuri hata tukiwa maskini. Ona mfano ufuatao:

Katika nchi ambayo watu wengi sana hawana kazi, mwanamke anayefanya kazi katika kiwanda fulani alihatarisha kazi yake kwa kuomba ruhusa ya kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Msimamizi wake angemwachisha kazi mara moja. Badala yake, alimshangaza mwanamke huyo na wafanyakazi wenzake kwa kumpa ruhusa. Isitoshe, msimamizi huyo alimwambia angependa aendelee kufanya kazi katika kiwanda chake na akamsifu kwa kuwa “mfanyakazi mzuri.” Kwa nini?

Mfanyakazi huyo ambaye ni Shahidi wa Yehova, anaishi kulingana na kanuni za Biblia. Akitamani “kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote,” hakusema uwongo au kuiba na hivyo akawa na sifa nzuri ya unyoofu. (Waebrania 13:18) Kupatana na kanuni iliyoongozwa kwa roho inayopatikana katika Wakolosai 3:22, 23, alifanya kazi yake “kwa nafsi yote.” Hilo linamaanisha alimtii mwajiri wake, na alihakikisha kwamba kila siku alifanya kazi kwa bidii ili astahili kulipwa.

Bila shaka, tunaishi katika mfumo wa kiuchumi ambao unaongozwa na ubinafsi na jambo kuu ni kupata faida. Huenda wengine ambao wanaheshimu sana kanuni za Biblia wakahitaji kung’ang’ana ili kupata chakula, mavazi, na makao wanayohitaji. Lakini wana dhamiri safi mbele za Muumba nao wanatazamia kwa uhakika kwamba kutakuwa na wakati ujao mzuri, kwa sababu Yehova ni “Mungu anayetoa tumaini.”—Waroma 15:13.

Suluhisho Kamili la Umaskini

Biblia inafunua hisia zenye nguvu za Yehova dhidi ya wale wanaochochea kuteswa kwa maskini. Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho linasema: “Ole wao wanaotunga masharti yenye kudhuru na wale ambao, wakiandika sikuzote, wameandika taabu tupu, ili kuwasukuma mbali watu wa hali ya chini kutoka kwenye kesi na kuwanyang’anya haki wale wanaoteseka . . . , ili wajane wawe nyara yao, na ili hata wapore wavulana wasio na baba!” (Isaya 10:1, 2) Iwe wanawapuuza maskini kwa kupenda au bila kujua, wale wanaoongoza mfumo wa kiuchumi wa jamii ya kibinadamu ni sehemu ya mfumo utakaoharibiwa na Mungu Mweza-Yote.

Nabii Isaya anawauliza wanyanyasaji hao swali lenye uzito: “Nanyi mtafanya nini katika ile siku ya kukaziwa uangalifu na wakati wa uharibifu, utakapokuja kutoka mbali?” (Isaya 10:3) Yehova atawaangamiza watu hao kwa kuharibu mfumo usiofuatia haki wanaoendeleza.

Lakini kusudi la Mungu linahusisha mengi zaidi ya kuchukua hatua dhidi ya wanyanyasaji. Atawapa wanadamu wenye mwelekeo unaofaa maisha yasiyokuwa na ukosefu wa haki. Atatumia mfumo bora zaidi wa kiserikali, naye atawaruhusu wanadamu kufurahia maisha yenye kuridhisha bila umaskini. Ili ufanikiwe wakati huo, hutahitaji kupata urithi mkubwa wa pesa, kujua watu wenye vyeo, au kuwa na ustadi wa kibiashara. Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba mabadiliko hayo yatatukia?

Yesu Kristo ambaye Yehova amemweka rasmi atawale wanadamu, alitaja wakati huo kuwa “uumbaji-mpya.” (Mathayo 19:28) Maneno hayo yanamaanisha kufanywa upya, kuanzishwa upya kwa uhai wa binadamu. Kwa kutumia maneno “uumbaji-mpya,” Yesu alikazia kwamba Yehova atawapa wanadamu waadilifu nafasi ya kuishi kama Muumba wetu mwenye upendo anavyotaka. Kati ya faida nyingi ambazo atawapa wanadamu wakati huo ni kuondolewa kwa matatizo ya kiuchumi yanayowakumba watu wengi sana leo.

Biblia ilitoa unabii huu kuhusu utawala wa Yesu Kristo: “Atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri, nayo damu yao itakuwa na thamani machoni pake.”—Zaburi 72:12-14.

Unaweza kuwa na wakati ujao mzuri kama huo. Lakini ili kutimiza matakwa ya Mungu ya kuishi katika ulimwengu huo mpya, ni muhimu kwanza ujifunze kisha ufanye mapenzi ya Mungu wa kweli. Fanya maamuzi yanayofaa kwa kutegemea ujuzi wa Neno la Mungu. Ishi ukitazamia wakati ujao mzuri ambao Mungu anawatolea wanadamu wote. Hutatamaushwa kamwe. Neno la Mungu linaahidi: “Maskini hawatasahauliwa sikuzote, wala tumaini la wapole halitaangamia kamwe.”—Zaburi 9:18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Mistari mingine miwili ya Biblia inayozungumzia jinsi Mungu anavyowahangaikia watu wanaoteseka ni Zaburi 35:10 na Zaburi 113:7.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Unaweza kuwa na wakati ujao mzuri

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Je, Nihamie Nchi Bora Zaidi Kiuchumi?

Neno la Mungu haliwaambii watu wanapaswa kuishi na kufanya kazi wapi. Hata hivyo, kanuni za Biblia zinaweza kumsaidia mtu kuamua ikiwa inafaa kuhamia nchi nyingine kwa sababu za kiuchumi. Chunguza maswali na kanuni za Maandiko zifuatazo.

1. Je, ninadanganywa na uvumi? Methali 14:15 inasema: “Mtu asiye na uzoefu hu- amini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” Baada ya kuhamia nchi tajiri, mtu mmoja kutoka Ulaya Mashariki alisema: “Nilisikia kwamba huku pesa huchipuka juu ya miti kama majani. Bado ninatafuta miti hiyo.”

2. Je, nina maoni yenye usawaziko kuhusu mahitaji ya familia yangu? Je, ninafuatia mahitaji ya lazima au ni tamaa zangu mwenyewe? Kichwa cha kila familia anapaswa kuandaa mahitaji ya kimwili ya mke na watoto. (1 Timotheo 5:8) Lakini akina baba wana daraka mbele za Mungu la kuwafundisha watoto wao kiadili na kiroho. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Waefeso 6:4) Huenda baba akafaulu kuandaa mahitaji mengi zaidi ya kimwili akihamia nchi nyingine. Lakini hawezi kuandaa mazoezi ya maadili na kiroho ya watoto wake ikiwa hatawaona kwa majuma kadhaa, miezi, au miaka.

3. Je, ninatambua kwamba kumwacha mke wangu kwa muda mrefu kunatokeza hatari ya sisi wawili kufanya uzinzi? Neno la Mungu linawaonya watu waliooana wafikirie mahitaji ya kingono ya wenzi wao.—1 Wakorintho 7:5.

4. Je, ninatambua kwamba kuingia nchi fulani bila kibali kunaweza kutokeza matatizo makubwa ya kisheria? Wakristo wa kweli wanapaswa kutii sheria za nchi.—Waroma 13:1-7.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Kanuni za Biblia zinafaa iwe sisi ni matajiri au maskini

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 7]

Top: © Trygve Bolstad/Panos Pictures