Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Asilimia 5 ya gharama ya umeme ya kila nyumba nchini Kanada, inatokana na umeme unaotumiwa na vifaa vinavyoachwa bila kuzimwa kabisa.—NATIONAL POST, KANADA.

Matokeo ya uchunguzi mmoja yalionyesha Warusi wanaamini kwamba mambo muhimu zaidi ambayo serikali inapaswa kushughulikia yanatia ndani kukabiliana na “ufisadi” na “kupunguza kuongezeka kwa gharama.”—PRAVDA, URUSI.

Kulingana na uchunguzi mmoja, asilimia 26.4 ya wanafunzi walio na umri wa miaka 12 hivi nchini Taiwan “wamewahi kufikiria kuhusu kujiua.”—THE CHINA POST, TAIWAN.

“Ingawa teknolojia imesaidia kupunguza muda ambao watu wanafanya kazi kwa asilimia 38 katika karne moja iliyopita, wafanyakazi hawana tena wakati wa kufanya mambo ya kibinafsi kwa sababu ya kusafiri kwa muda mrefu, masomo ya watu wazima, na kuongezeka kwa kazi za nyumbani.”—FORBES, MAREKANI.

Kutokezwa kwa gesi zinazoongeza kiwango cha joto duniani katika nchi zilizositawi kuliongezeka kwa asilimia 1.6 kati ya mwaka wa 2003 na 2004, kufikia “kiwango cha juu zaidi katika muda wa miaka kumi hivi.”—REUTERS, OSLO, NORWAY.

Shida ya Maji Nchini China

China ina tatizo la “uchafuzi wa maji na ukosefu wa maji safi.” Ingawa majiji mengi yana vituo vya kusafisha maji machafu, vituo vingi havina pesa za kutosha za kuviendeleza. “Mito mingi, maziwa, na mifereji huchafuliwa na maji machafu kutoka viwandani, nyumbani, na vilevile maji yenye kemikali za kuua wadudu kutoka kwenye mashamba,” linaripoti gazeti The Wall Street Journal. Isitoshe, “watu milioni 300 hivi hawawezi kupata maji safi ya kunywa.” Hali si nzuri, linasema gazeti hilo, na inazidi kuzorota.

“Ninyi Ni Nani? Mashahidi wa Yehova?”

Mwaka uliopita vijana Wakatoliki waliokubali mwito wa askofu wa dayosisi ya Massa Marittima-Piombino waliwaendea watalii kwenye fuo za Kisiwa cha Elba, Italia. Askofu huyo aliwaambia kwamba wakitaka kuwa Wakristo na kudumu wakiwa hivyo, wanapaswa kutangaza imani yao. Watalii hao walishangaa. Kulingana na gazeti Il Tempo, swali ambalo watu wengi waliwauliza vijana hao lilikuwa, “Ninyi ni nani? Mashahidi wa Yehova?”

Muziki Unahusianishwa na Ngono

Vijana wanaosikiliza muziki ulio na “maneno machafu ya ngono” huelekea “kuanza kufanya ngono mapema kuliko wale wanaosikiliza muziki mwingine,” ndivyo uchunguzi mmoja ulioripotiwa na shirika la habari la Associated Press unavyoonyesha. “Muziki unaowaonyesha wanaume kuwa watu wanaopenda kufanya ngono, wanawake kuwa wenye kuvutia tu kingono, na unaotaja matendo ya ngono waziwazi, unaweza kuchochea tabia za ngono kuliko muziki unaotaja mambo hayo kwa njia isiyo ya moja kwa moja na unaozungumzia mahusiano ya kudumu,” inasema ripoti hiyo. Iliongeza kusema kwamba “wazazi, walimu, na vijana wenyewe wanapaswa kufikiria kwa uzito kuhusu maneno yaliyo katika muziki.”

Wateja Waharibifu

Mnamo 2004, Waaustralia walitupa chakula cha dola bilioni 4.1 za Marekani, inaripoti taasisi ya utafiti ya Australia. Hiyo ni zaidi ya mara 13 ya kiasi cha pesa ambazo Waaustralia walichanga kwa ajili ya misaada ya kimataifa mwaka wa 2003. Jumla ya pesa ambazo Waaustralia hupoteza kwa bidhaa na huduma ambazo hazitumiwi kila mwaka ni zaidi ya dola bilioni 8.1 za Marekani. Hiyo ni zaidi ya pesa ambazo nchi hiyo hutumia kwa ajili ya vyuo vikuu na barabara.