Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kutafuta Pesa Kuna Madhara?

Je, Kutafuta Pesa Kuna Madhara?

Je, Kutafuta Pesa Kuna Madhara?

IKIWA ungetajirika ghafula, ungefanya nini? Je, ungetulia na kufurahia maisha? Je, ungeacha kufanya kazi na kutumia wakati mwingi zaidi pamoja na familia yako na marafiki? Au ungetafuta kazi nyingine unayofurahia zaidi? Inashangaza kwamba watu wengi wanaotajirika hawafanyi hivyo. Badala yake, wao huendelea kutafuta pesa zaidi ili kulipa madeni yao mapya au kujitajirisha zaidi.

Hata hivyo, wengine ambao wamefanya hivyo wametambua kwamba tamaa ya mali inaathiri afya yao, maisha ya familia, na tabia za watoto wao. Hivi karibuni, vitabu, makala mbalimbali, vipindi vya televisheni, na video zimewaonya watu kuhusu kuponda raha kupita kiasi, na badala yake zimependekeza watu waishi maisha yenye usawaziko. Habari mbalimbali zimeonyesha kwamba kutafuta mali sana kunaweza kumdhuru mtu kiakili, kihisia, na hata kimwili.

Bila shaka, kwa muda mrefu watu wamehangaikia hatari za kutafuta mali. Miaka 2,000 hivi iliyopita, Biblia ilisema: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu. Kwa maana kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:9, 10.

Je, hilo ni kweli? Je, kweli wale ambao kusudi lao kuu maishani ni kutafuta pesa na mali hupatwa na madhara? Au je, wana kila kitu, yaani, mali, afya, na familia zenye furaha? Hebu tuone.