Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna ubaya gani kuwa na uhusiano wa siri?

Kuna ubaya gani kuwa na uhusiano wa siri?

Vijana Huuliza . . .

Kuna ubaya gani kuwa na uhusiano wa siri?

Jessica * alikabili uamuzi mgumu. Kijana mmoja darasani anayeitwa Jeremy alianza kupendezwa naye. “Alikuwa na sura nzuri sana,” Jessica anasema, “marafiki wangu walisema kwamba huyo ndiye mvulana mzuri zaidi ambaye nitawahi kumpata. Wasichana kadhaa walikuwa wamejaribu kuanzisha uhusiano naye, lakini alikataa. Alinipenda mimi tu.”

Muda si muda, Jeremy alimwomba Jessica waende matembezi. Jessica anasema: “Nilimweleza kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova na siwezi kuruhusiwa kuwa na uhusiano na mtu ambaye si wa dini yangu. Lakini Jeremy alitoa wazo lingine. Aliuliza, ‘Mbona tusiwe na uhusiano bila wazazi wako kujua?’”

IKIWA mtu fulani ambaye unavutiwa naye angekuambia hivyo, wewe ungefanya nini? Huenda ukashangaa kujua kwamba mwanzoni Jessica alikubaliana na maneno ya Jeremy. Anasema: “Nilisadiki kwamba iwapo ningekuwa na uhusiano pamoja naye, ningeweza kumsaidia ajifunze kumpenda Yehova.” Matokeo yalikuwa nini? Tutaona baadaye. Kwanza, acheni tuone jinsi ambavyo kijana Mkristo kama Jessica anavyoweza kuingia katika mtego wa kuwa na uhusiano wa siri pamoja na mtu wa jinsia tofauti bila kujua.

Kwa Nini Wanakuwa na Uhusiano wa Siri?

Wavulana na wasichana huanza kufanya urafiki mapema sana. Susan kutoka Uingereza anasema, “Nimeona wavulana na wasichana wenye umri wa miaka 10 au 11 wakiwa na uhusiano na watu wa jinsia tofauti!” Kwa nini wanasisimuka sana hivyo? Mara nyingi ni kwa sababu ya kuvutiwa kiasili na watu wa jinsia tofauti na vilevile uvutano wa marafiki. Lois huko Australia anasema hivi: “Wakati huo homoni huongezeka na kila mtu shuleni huwa na uhusiano na mtu wa jinsia tofauti.”

Lakini kwa nini wengine huanzisha uhusiano wa siri? “Labda wanaogopa maoni ya wazazi wao,” asema Jeffrey kutoka Uingereza. Naye David wa Afrika Kusini ana maoni kama hayo. Anasema, “Wanajua kwamba wazazi wao hawatakubali, kwa hiyo hawawaambii chochote.” Msichana mmoja kutoka Australia anayeitwa Jane anaeleza sababu nyingine. Anasema, “Uhusiano wa siri huonyesha kwamba mtu ni mwasi. Kijana akihisi kwamba hatendewi kama mtu mzima, yeye huamua kufanya chochote anachotaka bila kuwajulisha wazazi wake. Ni rahisi kudumisha uhusiano huo ukiwa siri.”

Biblia inakuamuru uwatii wazazi wako. (Waefeso 6:1) Na ikiwa wazazi wako hawakuruhusu uanzishe uhusiano na mtu wa jinsia tofauti, bila shaka wana sababu nzuri. Kwa mfano ikiwa wao ni Mashahidi wa Yehova, wazazi wako watakuruhusu uanzishe uhusiano pamoja na mwamini mwenzako tu wakati ambapo nyote wawili mko tayari kufunga ndoa. * Hata hivyo, usishangae unapokuwa na maoni haya:

Ninaona kwamba ninakosa kitu fulani kwa sababu kila mtu ana uhusiano na mtu wa jinsia tofauti isipokuwa mimi.

Ninavutiwa na mtu ambaye si wa dini yangu.

Ningependa kuwa na uhusiano pamoja na Mkristo mwenzangu, ingawa sijafikia umri wa kufunga ndoa.

Huenda unajua maoni ya wazazi wako kuhusu mambo hayo. Nawe unaamini kwamba wazazi wako hawajakosea. Lakini huenda ukawa na maoni kama ya Manami anayeishi Japani, anayesema: “Mimi hushawishiwa sana niwe na uhusiano na mtu wa jinsia tofauti hivi kwamba nyakati nyingine mimi huwa na mashaka kuhusu msimamo wangu. Vijana wa leo wanaona ni lazima wawe na uhusiano na mtu wa jinsia tofauti.” Wengine wanaokabili hali kama hiyo wameanzisha uhusiano na mtu wa jinsia tofauti bila wazazi wao kujua. Jinsi gani?

“Tuliambiwa Hatupaswi Kufichua Siri Hiyo”

Kuwa na uhusiano wa siri pamoja na mtu wa jinsia tofauti ni aina ya udanganyifu. Watu fulani hudumisha uhusiano wao ukiwa siri kwa kuwasiliana kupitia simu au Intaneti. Wakiwa mbele ya watu wanaonekana kuwa marafiki tu, lakini unapochunguza barua-pepe wanazotumiana, ujumbe wao mfupi kwenye simu, na mazungumzo yao kwenye simu, utagundua kwamba wana uhusiano wa siri.

Caleb anayeishi Nigeria anataja mbinu nyingine ya ujanja. Anasema: “Vijana fulani walio na uhusiano wa siri hutumia maneno ya siri na majina bandia wanapokuwa na marafiki wao ili wengine wasielewe wanachozungumzia.” Mbinu nyingine ni kupanga tafrija inayohusisha kundi la vijana, kisha baadaye wale walio na uhusiano wa siri wanajitenga na wenzao. James anayeishi Uingereza anasema: “Wakati fulani tulialikwa mahali fulani tukiwa kikundi, lakini baadaye tukagundua kwamba tafrija hiyo ilipangwa ili vijana wawili waweze kuwa pamoja. Tuliambiwa tusifichue siri hiyo.”

Kama James alivyosema, mara nyingi uhusiano wa siri pamoja na mtu wa jinsia tofauti hufaulu kupitia msaada wa marafiki. Carol kutoka Scotland anasema: “Angalau rafiki mmoja hujua kinachoendelea lakini anaamua kunyamaza kwa sababu ya ‘kula kiapo cha kuweka siri.’”

Mara nyingi udanganyifu wa wazi unahusika. Beth kutoka Kanada anasema: “Wengi hudumisha uhusiano wao ukiwa siri kwa kuwadanganya wazazi wao kuhusu mahali ambapo wanakwenda.” Misaki kutoka Japani anakubali kwamba alifanya hivyo. Anasema: “Ilinibidi nitunge hadithi za uwongo. Nilikuwa mwangalifu nisiseme uwongo kuhusu mambo mengine isipokuwa tu uhusiano wangu wa siri ili wazazi wangu waendelee kuniamini.”

Hatari za Uhusiano wa Siri

Ukishawishiwa kuwa na uhusiano wa siri au ikiwa tayari umeanzisha uhusiano wa aina hiyo, inafaa ufikirie yafuatayo.

Udanganyifu wangu utakuwa na matokeo gani? Je, unakusudia kufunga ndoa pamoja na mtu huyo hivi karibuni? Evan kutoka Marekani anasema: “Mtu akianzisha uhusiano pamoja na mtu wa jinsia tofauti akiwa hana nia ya kufunga ndoa, ni kama mtu anayetangaza kitu ambacho hana nia ya kukiuza.” Methali 13:12 inasema: “Tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa.” Je, kweli ungependa kuumiza hisia za mtu unayemjali?

Yehova Mungu anahisije kuhusu yale ninayofanya? Biblia inasema kwamba “vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.” (Waebrania 4:13) Kwa hiyo, ikiwa unaficha uhusiano wako au wa rafiki yako, tayari Yehova anajua jambo hilo. Na ikiwa umedanganya, unapaswa kuhangaikia jambo hilo. Yehova Mungu anachukia sana udanganyifu. Kwa kweli, “ulimi wa uwongo” ni kati ya mambo ambayo Biblia inasema anayachukia.—Methali 6:16-19.

Kwa kweli, unapokuwa na uhusiano wa siri unakosa ulinzi ambao ungepata ikiwa uhusiano huo ungejulikana. Haishangazi kwamba wengine ambao wana uhusiano wa siri hutumbukia katika mwenendo mpotovu kingono. Jane kutoka Australia, anaeleza kuhusu rafiki yake aliyekuwa na uhusiano wa siri pamoja na mvulana shuleni naye alijifanya kuwa mzuri ingawa alikuwa akitenda dhambi. Jane anasema: “Kufikia wakati ambapo baba yake aligundua kwamba alikuwa na uhusiano na mvulana, tayari alikuwa na mimba.”

Bila shaka, ingekuwa vema uzungumze na wazazi wako au Mkristo mkomavu ikiwa una uhusiano wa siri. Na ikiwa una rafiki aliye na uhusiano wa siri, usishiriki matendo yake kwa kumsaidia kuficha uhusiano huo. (1 Timotheo 5:22) Ungehisije ikiwa uhusiano huo ungesababisha madhara? Je, hungehusika kwa kiasi fulani? Tuseme rafiki yako aliye na ugonjwa wa kisukari anakula peremende kwa siri. Utafanya nini ukijua jambo hilo lakini rafiki yako akusihi usimwambie mtu yeyote? Utachukua hatua gani—utaficha jambo hilo au utachukua hatua ambayo inaweza kuokoa maisha yake?

Ndivyo ilivyo ikiwa unamjua yeyote ambaye ana uhusiano wa siri na mtu wa jinsia tofauti. Usiogope kwamba urafiki wenu utavunjika! Baada ya muda, rafiki wa kweli atatambua kwamba ulichukua hatua kwa sababu unamjali.—Methali 27:6.

“Nilijua Nilichopaswa Kufanya”

Jessica, aliyetajwa mwanzoni, alibadili maoni yake kuhusu kuwa na uhusiano wa siri na mtu wa jinsia tofauti aliposikia kumhusu Christian ambaye alikuwa na tatizo hilo. Baada ya kusikia jinsi Christian alivyokomesha uhusiano huo,” Jessica anasema, “Nilijua nilichopaswa kufanya.” Je, ilikuwa rahisi kukomesha uhusiano huo? La! Jessica anasema: “Sijawahi kumpenda mvulana mwingine kama huyo. Kwa majuma kadhaa, nililia kila siku.”

Hata hivyo, Jessica alijua jambo lingine pia—kwamba anampenda Yehova na ingawa alikuwa amekengeushwa, alitaka sana kufanya lililo sawa. Baadaye, uchungu wa kuukomesha uhusiano huo ulipungua. Jessica anasema: “Sasa uhusiano wangu pamoja na Yehova umekuwa mzuri sana kuliko wakati mwingine wowote. Ninashukuru sana kwamba anatupa mwongozo tunaohitaji kwa wakati unaofaa!”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 9 Ona makala ya “Vijana Huuliza . . . Ninaweza Kuanza Urafiki wa Karibu na Mtu wa Jinsia Tofauti Lini?” kwenye gazeti la Januari (Mwezi wa 1) 2007.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Fikiria mambo matatu ambayo yameonyeshwa kwa maandishi mazito kwenye ukurasa wa 27. Ikiwa kuna lolote, ni lipi kati ya hayo linaloonyesha jinsi unavyohisi wakati mwingine?

▪ Unawezaje kukabiliana na jambo hilo bila kuwa na uhusiano wa siri?

[Sanduku katika ukurasa wa 28]

Ni Siri au Faragha?

Katika uhusiano pamoja na mtu wa jinsia tofauti, nyakati nyingine kuweka siri hakumaanishi udanganyifu. Tuseme mwanamume na mwanamke waliofikia umri wa kufunga ndoa wangependa kujuana vizuri zaidi lakini wanataka kufanya hivyo kwa siri kwa muda fulani. Labda kama kijana anayeitwa Thomas alivyosema, “hawataki kuulizwa-ulizwa maswali kama, ‘Mtafunga ndoa lini?’”

Mikazo kutoka kwa wengine inaweza kuwa hatari. (Wimbo wa Sulemani 2:7) Hivyo, mwanzoni mwa uhusiano, mwanamume na mwanamke wanaweza kuchagua kudumisha uhusiano wao ukiwa siri huku wakiwa waangalifu wasiwe peke yao. (Methali 10:19) Anna mwenye umri wa miaka 20 anasema: “Hilo huwawezesha watu wawili kuwa na wakati wa kuamua ikiwa wanataka kuendeleza uhusiano huo. Ikiwa ndivyo, basi wanaweza kuwajulisha wengine.”

Wakati huohuo, haifai kuwaficha watu ambao wana haki ya kujua kuhusu uhusiano huo, kama vile wazazi wako au wazazi wa yule mtu mwingine. Ikiwa hutaki uhusiano huo ujulikane, unapaswa kujiuliza sababu. Je, hali yako ni kama ya Jessica aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii? Je, unaamini kwamba wazazi wako wana sababu nzuri za kukataa?

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

TAARIFA KWA WAZAZI

Baada ya kusoma makala iliyotangulia, huenda ukajiuliza hivi, ‘Je, mwana au binti yangu anaweza kuwa na uhusiano wa siri bila mimi kujua?’ Ona mambo ambayo vijana fulani walimwambia mwandishi wa gazeti la Amkeni! yanayowafanya washawishiwe kuwa na uhusiano wa siri, kisha ufikirie maswali yafuatayo.

“Vijana fulani hawapati faraja nyumbani, kwa hiyo wanaamua kuwa na mfariji wa jinsia tofauti.”—Wendy.

Ukiwa mzazi, unaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba mahitaji ya kihisia ya watoto wako yanatoshelezwa? Je, unaweza kufanya mabadiliko fulani kuhusiana na jambo hilo? Ikiwa ndiyo, ni mabadiliko gani?

“Nilipokuwa na umri wa miaka 14, mwanafunzi mwenzangu aliniomba niwe rafiki yake wa kike. Nilikubali. Nilifikiri kwamba ni jambo zuri kuwa na mvulana anayenikumbatia.”—Diane.

Ikiwa Diane angekuwa binti yako, ungeshughulikiaje tatizo hilo?

“Simu za mkononi zinafanya iwe rahisi kuwa na uhusiano wa siri. Wazazi hawajui kinachofanyika!”—Annette.

Ni tahadhari gani unazoweza kuchukua ikiwa watoto wako wanatumia simu za mkononi?

“Uhusiano wa siri unaweza kudumishwa kwa urahisi iwapo wazazi hawajui watoto wao wanafanya nini na wanashirikiana na nani.”—Thomas.

Je, kuna njia ambazo unaweza kujihusisha katika maisha ya kijana wako huku ukimruhusu awe na uhuru wa kadiri fulani?

“Mara nyingi wazazi hawawi nyumbani pamoja na watoto wao. Au wanawaruhusu watoto wao kwenda sehemu mbalimbali pamoja na watu wengine bila kujali.”—Nicholas.

Mfikirie rafiki mkubwa wa mtoto wako. Je, kweli unajua wao hufanya nini wanapokuwa pamoja?

“Uhusiano wa siri unaweza kuanzishwa wakati wazazi ni wakali sana.”—Paul.

Bila kuvunja sheria na kanuni za Biblia, unaweza kufanyaje ‘usawaziko wako ujulikane’?—Wafilipi 4:5.

“Nilipokuwa na miaka 14 hivi, nilihisi sifai na nilitamani kupendwa. Nilianza kumtumia kijana katika kutaniko jirani barua-pepe na nikaanza kumpenda. Alinifanya nihisi kwamba mimi ni mtu wa pekee.”—Linda.

Je, unaweza kufikiria njia zinazofaa ambazo zingetumiwa kutosheleza mahitaji ya Linda nyumbani?

Unaweza kutumia makala hii na ukurasa huu kuwa msingi wa mazungumzo pamoja na mwana au binti yako. Njia bora ya kuzuia kufanya mambo kwa siri ni mawasiliano ya wazi yanayotoka moyoni. Utahitaji wakati na subira kutambua mahitaji ya kijana, lakini thawabu utakazopata zitakuridhisha.—Methali 20:5.