Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Niliacha Sarakasi

Kwa Nini Niliacha Sarakasi

Kwa Nini Niliacha Sarakasi

Simulizi la Marcelo Neím

NILIZALIWA Montevideo, Uruguay. Ingawa wazazi wangu walikuwa wacha-Mungu, hawakufuata dini yoyote. Mama yangu alikufa katika msiba nilipokuwa na umri wa miaka minne hivi, watu wa ukoo walinilea nao wakajaribu kunifundisha maadili mema. Nikiwa na umri wa miaka 20, niliamua kusafiri ili nipate kujua nchi na tamaduni mbalimbali.

Nikiwa nchini Kolombia nilianza kufanya kazi katika kikundi cha sarakasi nikiwa msaidizi. Nilitazama jinsi wanasarakasi walivyofurahi umati ulipowashangilia, nami nikataka kuwa mmoja wao. Hivyo, nikajizoeza mchezo wa baiskeli nikitumia baiskeli ndogo-ndogo mpaka nikaweza kucheza nikitumia baiskeli yenye urefu wa sentimita 12 tu, ambayo ni mojawapo baiskeli ndogo sana ulimwenguni. Ingetosha kwenye kiganja cha mkono wangu. Nikaanza kujulikana sana kotekote Amerika Kusini. Nikiwa na umri wa miaka 25, nilifika Mexico na kufanya kazi katika vikundi kadhaa vya sarakasi.

Maisha Yangu Yabadilika Ghafula

Nilipenda sarakasi sana. Kazi hiyo ilihusisha kusafiri, kukaa katika hoteli bora, na kula katika mikahawa ya hali ya juu. Hata hivyo, maisha yangu hayakuwa na maana, na sikuwa na tumaini la wakati ujao. Lakini alasiri moja maisha yangu yalibadilika. Msimamizi wa maonyesho ya sarakasi, alinipa kitabu alichokuwa amepokea chenye kichwa UfunuoUpeo Wao Mtukufu U Karibu! * Baada ya maonyesho hayo nilikisoma mpaka mapema asubuhi. Ingawa haikuwa rahisi kukielewa kitabu hicho, maelezo kuhusu mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu na kahaba wa Ufunuo yalinisisimua. (Ufunuo 17:3–18:8) Kisha, nilipokuwa nikisafisha lori nililokuwa nimenunua, nilipata kitabu kingine kilichotolewa na wachapishaji hao-hao, Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani.* Hakikuwa kigumu kueleweka, na mara moja nikatambua kwamba ninapaswa kuhubiri. Kwa hiyo, nikaanza mara moja kuwaeleza watu wote niliokutana nao mambo ambayo nilikuwa nimejifunza.

Baada ya muda, niliona kwamba ninahitaji kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova. Namba ya simu ya msichana Shahidi ambaye alimwachia rafiki yangu kitabu Upeo wa Ufunuo ilikuwa ndani ya kitabu hicho. Basi nikampigia simu, na baba yake akanialika kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Tijuana, Mexico. Nilifurahishwa sana na upendo nilioona huko nami nikasadikishwa kwamba hiyo ndiyo dini ya kweli. Mahali popote tulipoenda kwa ajili ya maonyesho ya sarakasi, nilihudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme na kupata vichapo vya kugawa isivyo rasmi.

Jambo fulani lililotukia lilinisadikisha hata zaidi kwamba sikuwa nimepotea. Mashahidi walinialika kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo na kunieleza kwamba ni muhimu Wakristo wahudhurie. Lakini ilikuwa siku ya kufungua maonyesho, nami nilifikiri haitawezekana kuhudhuria. Nilisali kwa Yehova kwa bidii kuhusu jambo hilo, na jambo la kushangaza likatukia. Saa mbili kabla ya maonyesho kuanza, umeme ulikatika! Hivyo, nilihudhuria Ukumbusho na kisha nikarudi kushiriki katika maonyesho. Kwa maoni yangu, Yehova alikuwa amejibu sala yangu.

Siku moja nilikuwa nikigawa trakti huku nikisubiri nihudumiwe kwenye benki. Mzee mmoja Mkristo aliniona na kunipongeza kwa bidii yangu. Alinitia moyo nianze kuhubiri kwa njia rasmi pamoja na kutaniko. Kwa upendo alinieleza kwamba nahitaji kufanya mabadiliko maishani ili nistahili. Nilipokuwa nikifikiria kufanya mabadiliko hayo, niliahidiwa kazi ya mshahara mnono katika kundi la sarakasi huko Marekani. Nilichanganyikiwa. Nilitaka kwenda Marekani, lakini ikiwa ningekubali kazi hiyo labda nisingeweza kufuatilia imani yangu mpya. Hilo lilikuwa jaribu langu la kwanza nami sikutaka kumhuzunisha Yehova. Ingawa wanasarakasi wenzangu walishangazwa na uamuzi wangu, niliacha kazi ya sarakasi, nikaanza kushirikiana rasmi na kutaniko, nikakata nywele zangu ndefu, nami nikafanya mabadiliko mengine maishani ili niweze kumtumikia Yehova.

Nimeridhika Maishani, Nami Sina Majuto

Mwaka wa 1997 muda mfupi kabla ya kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, nilikabili jaribu la pili. Nilipata nafasi nyingine ya kwenda Marekani ili kushiriki katika kipindi maarufu cha televisheni huko Miami, na ningelipiwa gharama zote. Lakini nilitaka kubatizwa na kuishi kupatana na wakfu wangu kwa Yehova. Kwa hiyo, nilikataa kwenda na jambo hilo liliwashangaza sana wawakilishi wa kipindi hicho.

Watu fulani huniuliza ikiwa ninajuta kuacha sarakasi. Mimi huwaambia kwamba siwezi kuacha kumpenda Yehova na kuwa rafiki yake ili nirudie maisha yangu ya awali. Ingawa katika kazi yangu mpya ya kuwa mhudumu Mkristo wa wakati wote sipigiwi makofi, sipati umashuhuri wala utajiri, maisha yangu yana kusudi. Nina tumaini zuri la kuishi katika paradiso duniani na kumkaribisha mama yangu atakapofufuliwa.—Yohana 5:28, 29.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.