Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mfuateni Kristo!”

“Mfuateni Kristo!”

“Mfuateni Kristo!”

Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova

Programu hii ya kusanyiko la siku tatu itaanza Marekani mwezi wa Mei (Mwezi wa 5) na kuendelea hadi mwaka wa 2008 katika mamia ya majiji ulimwenguni pote. Katika sehemu nyingi programu itaanza kwa muziki Ijumaa (Siku ya 5) saa 3.20 asubuhi. Programu nzima itakazia maisha ya Yesu.

Kichwa cha siku ya Ijumaa kinasema ‘Mtazameni kwa Makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa Imani Yetu, Yesu.’ (Waebrania 12:2) Hotuba ya kwanza ina kichwa “Kwa Nini Tumfuate ‘Kristo’?” Kutakuwa na mfululizo wenye sehemu tatu utakaoonyesha jinsi tunavyoweza “Kutambua Jukumu la Yesu Akiwa Musa Mkuu, Daudi Mkuu, na Sulemani Mkuu.” Kisha programu ya asubuhi itamalizika kwa hotuba ya msingi yenye kichwa, “Jukumu la Pekee la Yesu Katika Kusudi la Yehova.”

Hotuba ya kwanza Ijumaa alasiri itakuwa na kichwa “‘Tumempata Masihi’!” Baada ya hotuba hiyo kutakuwa na hotuba yenye kichwa “Kutafuta Hazina ‘Zilizofichwa kwa Uangalifu Ndani Yake.’” Kisha kutakuwa na mfululizo wa saa nzima wenye sehemu tano, “Iweni na Mtazamo wa Kristo Ndani Yenu” nao utatia ndani hotuba kama vile, ‘Aliwapokea kwa Fadhili,’ ‘Alikuwa Mtiifu Mpaka Kifo,’ na ‘Aliwapenda Mpaka Mwisho.’ Hotuba ya mwisho ina kichwa ‘Wanaendelea Kumfuata Mwana-Kondoo Popote Anapoenda.’

Kichwa cha programu ya Jumamosi (Siku ya Posho) ni “Kondoo Wangu Huisikiliza Sauti Yangu, . . . Nao Wananifuata.” (Yohana 10:27) Kutakuwa na mfululizo wa saa nzima wenye kichwa “Fuata Kielelezo cha Yesu Katika Huduma,” nao utatia ndani madokezo ya kuboresha huduma yetu. Kisha kutakuwa na hotuba mbili, “‘Alipenda Uadilifu na Kuchukia Uasi-Sheria’ —Namna Gani Wewe?” na “‘Mpinge Ibilisi’ Kama Yesu Alivyompinga.” Programu ya asubuhi itamalizika baada ya hotuba ya ubatizo, na wale wanaostahili watabatizwa.

Programu ya Jumamosi alasiri itaanza na mfululizo wenye kichwa “Msifuate . . . ” Itakuwa na sehemu sita yaani, “Umati,” “Mioyo Yenu na Macho Yenu,” “Vitu Visivyo vya Kweli,” “Walimu wa Uwongo,” “Hadithi za Uwongo,” na “Shetani.” Hotuba zinazofuata zitatia ndani “Mafundisho ya Yehova Hayana Kifani” na “Wasaidie Warudi Katika Kundi.” Programu ya siku hiyo itamalizika kwa kusikiliza hotuba yenye kusisimua, “‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu.’”

Kichwa cha Jumapili (Siku ya Yenga) ni “Endelea Kunifuata.” (Yohana 21:19) Baada ya hotuba yenye kichwa “‘Usitoe Visingizio’ vya Kutomfuata Kristo” kutakuwa na mfululizo: “Hazina za Mahubiri ya Mlimani” wenye sehemu sita ambao utakazia maneno ya Yesu kama vile “Wenye Furaha Ni Wale Wanaotambua Uhitaji Wao wa Kiroho,” “Kwanza Fanya Amani Yako Pamoja na Ndugu Yako,” na “Muwe na Mazoea ya Kuwapa Watu, na Watu Watawapa Ninyi.” Programu ya asubuhi itamalizia kwa hotuba ya watu wote yenye kichwa, “Ni Nani Walio Wafuasi wa Kweli wa Kristo?” Alasiri kutakuwa na drama yenye waigizaji inayotegemea simulizi la Biblia la Gehazi, mtumishi mwenye pupa wa nabii wa Mungu, Elisha. Hotuba ya mwisho ya kusanyiko ina kichwa, “Endeleeni Kumfuata Kristo, Kiongozi Wetu Asiyeweza Kushindwa!”

Fanya mipango sasa ili uhudhurie. Ili kujua kusanyiko lililo karibu nawe litafanyika wapi, tembelea Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova au waandikie wachapishaji wa gazeti hili. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi (Mwezi wa 3) 1, lina orodha ya mahali ambapo makusanyiko yote yatafanywa nchini Burundi, Kenya, Kongo (Kinshasa), Rwanda, Tanzania, na Uganda.