Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunapaswa Kuwa na Maoni Gani Kuhusu Pesa?

Tunapaswa Kuwa na Maoni Gani Kuhusu Pesa?

Maoni ya Biblia

Tunapaswa Kuwa na Maoni Gani Kuhusu Pesa?

BIBLIA inasema: “Pesa ni ulinzi.” (Mhubiri 7:12) Kwa kuwa zinaweza kununua chakula, mavazi, na nyumba, pesa ni ulinzi dhidi ya umaskini. Ndiyo, pesa zinaweza kununua mali zozote zile. Mhubiri 10:19 inasema hivi: “Pesa ndizo hutokeza jibu katika mambo yote.”

Neno la Mungu linatutia moyo kufanya kazi kwa bidii ili tushughulikie mahitaji yetu wenyewe na ya familia zetu. (1 Timotheo 5:8) Kufanya kazi kwa bidii na kwa unyoofu humwezesha mtu kupata uradhi, heshima, na usalama.—Mhubiri 3:12, 13.

Isitoshe, kufanya kazi kwa bidii hutuwezesha kuwasaidia wengine kifedha. Yesu alisema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35)Sisi hupata furaha hiyo tunapotumia pesa zetu kwa uchangamfu kuwasaidia wenye uhitaji, hasa Wakristo wenzetu, au kumnunulia zawadi mtu tunayempenda.—2 Wakorintho 9:7; 1 Timotheo 6:17-19.

Yesu aliwahimiza wafuasi wake wawe na ukarimu, waonyeshe ukarimu kila mara, si mara moja-moja tu. Alisema: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu.” (Luka 6:38) Kanuni hiyo inahusu pia kutoa ili kuendeleza masilahi ya Ufalme wa Mungu. (Methali 3:9) Kwa kweli, kuonyesha ukarimu kwa njia hiyo hutusaidia ‘kufanya urafiki’ pamoja na Yehova na Mwana wake.—Luka 16:9.

Jihadhari na “Kupenda Pesa”

Watu wenye ubinafsi hawana mazoea ya kuwapa wengine, na wakiwapa, huenda wakawa na nia mbaya. Mara nyingi tatizo lao ni kupenda pesa, na kinyume na matarajio yao, jambo hilo huwakosesha furaha. Andiko la 1 Timotheo 6:10 linasema: “Kwa maana kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.” Kwa nini kupenda pesa hakuridhishi na hata huumiza?

Sababu moja ni kwamba mtu mwenye pupa hatosheki na mali. Andiko la Mhubiri 5:10 linasema: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha.” Hivyo, watu wanaopenda pesa ‘hujichoma’ na mfadhaiko usiokwisha. Isitoshe, pupa yao huharibu mahusiano yao na watu wengine, huwafanya wakose furaha katika maisha ya familia, na hata hawapumziki vya kutosha. “Usingizi wa mtumishi ni mtamu, bila kujali kama anakula kidogo au kingi; lakini wingi alio nao tajiri haumruhusu kulala.” (Mhubiri 5:12) Zaidi ya yote, mtu anayependa pesa hukosa kibali cha Mungu.—Ayubu 31:24, 28.

Masimulizi ya Biblia na historia ya kilimwengu ina mifano mingi ya watu walioiba, waliopotosha haki, waliofanya ukahaba, walioua, waliowasaliti wengine, na kusema uongo ili tu wapate pesa. (Yoshua 7:1, 20-26; Mika 3:11; Marko 14:10, 11; Yohana 12:6) Katika huduma yake duniani, Yesu alimwalika mtawala kijana aliyekuwa “tajiri sana” amfuate. Kwa kusikitisha, kijana huyo alikataa mwaliko huo wa pekee kwa sababu angepata hasara ya kifedha. Kwa sababu hiyo Yesu alisema hivi: “Jinsi itakavyokuwa vigumu kwa wale walio na pesa kuingia katika ufalme wa Mungu!”—Luka 18:23, 24.

Katika hizi “siku za mwisho,” Wakristo wanapaswa kujihadhari sana kwa sababu kama ilivyotabiriwa, watu ni “wenye kupenda pesa.” (2 Timotheo 3:1, 2) Wakristo wa kweli ambao huendelea kuhangaikia uhitaji wao wa kiroho, hawaathiriwi na pupa kwa sababu wana kitu kilicho bora kuliko pesa.

Kitu Kilicho Bora Kuliko Pesa

Alipotaja kwamba pesa ni ulinzi, Mfalme Sulemani aliongeza kwamba “hekima ni ulinzi,” kwa sababu ‘inawahifadhi hai waliyo nayo.’ (Mhubiri 7:12) Alimaanisha nini? Sulemani alikuwa akizungumzia hekima inayotegemea ujuzi sahihi wa Maandiko na kumwogopa Mungu kwa njia inayofaa. Hekima hiyo inayotoka kwa Mungu ambayo ni bora kuliko pesa, inaweza kumsaidia mtu aepuke kifo cha mapema na matatizo mengi maishani. Pia, sawa na taji, hekima ya kweli huwatukuza walio nayo na kuwaletea heshima. (Methali 2:10-22; 4:5-9) Na kwa sababu inawezesha mtu kupata kibali cha Mungu, inaitwa “mti wa uzima.”—Methali 3:18.

Wale wanaotaka kikweli hekima hiyo na wale wanaotaka kuitafuta, hutambua kwamba inaweza kupatikana. “Mwanangu, ikiwa . . . utaita uelewaji na kupaaza sauti yako uite utambuzi, ikiwa utaendelea kuutafuta kama fedha, na kuendelea kuutafuta kama hazina zilizofichika, ndipo utakapoelewa kumwogopa Yehova, nawe utapata kumjua Mungu. Kwa maana Yehova mwenyewe anatoa hekima; kinywani mwake hutoka ujuzi na utambuzi.”—Methali 2:1-6.

Kwa kuwa wanaona hekima kuwa muhimu zaidi ya pesa, Wakristo wa kweli hupata uradhi, furaha, na usalama ambao watu wanaopenda pesa hawana. Andiko la Waebrania 13:5 linasema: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa. Kwa maana [Mungu] amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’” Pesa haziwezi kumhakikishia mtu ulinzi kama huo.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Ni kwa njia gani pesa ni ulinzi?—Mhubiri 7:12.

▪ Kwa nini hekima inayotoka kwa Mungu ni bora kuliko pesa?—Methali 2:10-22; 3:13-18.

▪ Kwa nini tuepuke kupenda pesa?—Marko 10:23, 25; Luka 18:23, 24; 1 Timotheo 6:9, 10.