Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Acha Mungu Akuongoze Kwenye “Uzima Ulio wa Kweli”

Acha Mungu Akuongoze Kwenye “Uzima Ulio wa Kweli”

Acha Mungu Akuongoze Kwenye “Uzima Ulio wa Kweli”

MTU yeyote ambaye hutoa mwongozo anapaswa kutegemeka. Wale wanaomjua Yehova, Mtungaji wa Biblia wanaamini kwamba yeye ni mwenye kutegemeka zaidi kuliko mtu mwingine yeyote. ‘Hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2; 2 Timotheo 3:16) Yoshua, mwanamume mwenye kumwogopa Mungu, ambaye aliwaongoza wana wa Israeli hadi kwenye Nchi ya Ahadi, alishuhudia kuhusu kutegemeka kwa Yehova. Alipokuwa akiwahutubia wana wa Israeli, Yoshua alisema hivi: “Mnajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.”—Yoshua 23:14.

Tangu wakati wa Yoshua, unabii mwingi wa Biblia umetimia. Kutimia kwa unabii huo wote kunatupa msingi imara wa kuamini unabii ambao bado haujatimia. Unabii mwingi kati ya huo unahusu kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia na wanadamu watiifu.

Je, Utafaidika Kutokana na Mwongozo wa Mungu?

Yehova ambaye ni wonyesho halisi wa upendo, anataka tuwe na furaha sasa na milele. (Yohana 17:3; 1 Yohana 4:8) Naam, Mungu anataka tufurahie “uzima ulio wa kweli,” yaani, uzima wa milele. (1 Timotheo 6:12, 19) Kwa sababu hiyo, zaidi ya Mashahidi wa Yehova milioni sita, wanatii sheria ya Mungu kwa kushiriki kwa shangwe “habari njema ya ufalme” na majirani wao. (Mathayo 24:14) Kwa sasa ni kana kwamba wanafanya kazi hiyo ulimwenguni pote kwani wanahubiri katika nchi 235!

Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni inayotawaliwa na Yesu Kristo. (Danieli 7:13, 14; Ufunuo 11:15) Chini ya uongozi wake watu wote waovu, ambao wanakataa kujitiisha chini ya mwongozo mwadilifu wa Yehova wataharibiwa. (Zaburi 37:10; 92:7) Baada ya hapo, dunia yote “hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

Hebu fikiria amani na umoja ambao utaenea wakati watu wote duniani watakapokuwa wakimwabudu Mungu “kwa roho na kweli” na kwa hiari wakijitiisha chini ya mwongozo wake wenye upendo na viwango vyake vikamilifu! (Yohana 4:24) Mwishowe, watu watafurahia “uzima ulio wa kweli” ulioahidiwa na Mungu!

Kama ilivyotabiriwa, ni watu wachache tu ambao watakubali mwongozo wa Mungu na kupata uzima. (Mathayo 7:13, 14) Je, ungependa kuwa mmoja wao? Ikiwa ndivyo, Mashahidi wa Yehova wanakukaribisha uchunguze Maandiko na umruhusu Mungu akuongoze. Kwa kufanya hivyo, ‘utaonja’ jinsi Yehova alivyo mwema. (Zaburi 34:8) Naam, kama tu ndege wanavyoongozwa na silika, Yehova ataongoza waaminifu wake kwenye uhai katika Paradiso.—Luka 23:43.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

“Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.”—MATHAYO 5:5

“Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—ZABURI 37:11

“Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu . . . Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena.” —UFUNUO 21:3, 4

“Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.” —METHALI 2:21, 22