Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Inatosha Tu “Kuwa Mwema”?

Je, Inatosha Tu “Kuwa Mwema”?

Maoni ya Biblia

Je, Inatosha Tu “Kuwa Mwema”?

“MIMI huishi vizuri kadiri niwezavyo, nami hujaribu kuwa mtu mwema,” anasema msichana aitwaye Allison. Watu wengi wana maoni kama hayo kwamba kuishi maisha ya aina hiyo kunampendeza Mungu.

Wengine wana uhakika kwamba hata wakifanya dhambi nzito Mungu hajali, maadamu maisha yao kwa ujumla ni mema. Wanaamini kwamba Mungu husamehe zaidi kuliko anavyohukumu.

Bila shaka, watu huwa na maoni tofauti-tofauti kuhusu maana ya “kuwa mwema.” Biblia inasema nini? Tunapaswa kufanya nini ili tuweze kukubaliwa na Mungu? Inamaanisha nini kuwa mwema machoni pa Mungu?

Kukubali Mwongozo wa Muumba Wetu

Akiwa Muumba, Yehova Mungu ana haki ya kutuongoza. (Ufunuo 4:11) Katika Biblia, Mungu ametoa sheria na kanuni za kuongoza matendo na ibada yetu. Mungu aliwaambia watu wake hivi: “Tiini sauti yangu, nanyi mfanye mambo kulingana na yote ninayowaamuru; nanyi hakika mtakuwa watu wangu nami nitakuwa Mungu wenu.”—Yeremia 11:4.

Kwa hiyo, kulingana na maoni ya Mungu, “kuwa mwema” kunamaanisha kujifunza viwango vyake na kurekebisha maisha yetu ili yapatane na viwango hivyo. Jaribu kuwazia kwamba unataka kuwa rafiki ya mtu fulani. Bila shaka ungependa kujua jinsi mtu huyo anavyotaka kutendewa, kisha utende kwa njia inayompendeza. Biblia inaonyesha kwamba kama tu mzee wa ukoo, Abrahamu, unaweza kuwa rafiki ya Mungu, yaani, mtu aliye na kibali chake. (Yakobo 2:23) Isitoshe, kwa kuwa Mungu ana viwango vya juu kuliko vyetu, hatuwezi kumtarajia afanye mabadiliko ili apatane nasi.—Isaya 55: 8, 9.

Umuhimu wa Utii

Je, kweli Mungu anaweza kutukataa ikiwa hatutii sheria zake “ndogo-ndogo”? Wengine wanafikiri kuwa kutii sheria “ndogo-ndogo” si muhimu. Hata hivyo, hakuna sheria ambayo imetungwa na Mungu inayopaswa kuonwa kuwa haina maana. Ona kwamba kwenye andiko la 1 Yohana 5:3, Biblia haitofautishi sheria hizo: “Kwa maana kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” Tukifanya yote tuwezayo kuzishika sheria za Mungu, tunathibitisha upendo wetu kwake.—Mathayo 22:37.

Yehova hadai ukamilifu kutoka kwetu. Tukisikitikia makosa yetu na kujaribu tusiyarudie, atatusamehe kwa hiari. (Zaburi 103:12-14; Matendo 3:19) Lakini je, tunaweza kupuuza sheria fulani tukifikiri kwamba utii wetu kwa mambo mengine utasawazisha? Mfano unaopatikana katika Biblia unaonyesha kwamba hatuwezi.

Mfalme Sauli wa Israeli aliamua kuchagua sheria atakazotii. Alipopigana na Waamaleki, aliagizwa asiache mnyama yeyote wa kufugwa akiwa hai. Alipaswa ‘kuwaua.’ Ingawa alifuata maagizo fulani, Sauli hakuwaangamiza “wanyama bora zaidi wa kundi na mifugo.” Kwa nini? Yeye na wote walioandamana naye walitaka kujihifadhia vitu hivyo.—1 Samweli 15:2-9.

Nabii Samweli alipomuuliza Sauli kwa nini hakutii sheria ya Mungu, Sauli alidai eti alitii. Alitaja mambo mazuri ambayo yeye na watu wake walikuwa wamefanya kutia ndani dhabihu walizomtolea Mungu. Samweli alimuuliza: “Je, Yehova hupendezwa sana na matoleo ya kuteketezwa na dhabihu kuliko kuitii sauti ya Yehova? Tazama! Kutii ni bora kuliko dhabihu, na kusikiliza kuliko mafuta ya kondoo-dume.” (1 Samweli 15:17-22) Kwa hiyo hatuwezi kulipia kutotii kwa kumtolea Mungu dhabihu au kwa kufanya mambo mengine mema.

Viwango vya Mungu Vinathibitisha Upendo Wake

Yehova hataki tukisie jinsi ya kumpendeza. Katika Biblia anatutolea mwongozo ulio wazi kuhusiana na maadili, ni kana kwamba anasema hivi: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.” (Isaya 30:21) Tunapofuata mwongozo wake, tunaepuka kukatishwa tamaa na mashaka yanayotokezwa na maoni ya kiadili ya wanadamu yanayotofautiana. Na tunaweza kuwa na hakika kwamba nyakati zote mwongozo wa Mungu ni kwa ajili ya faida yetu, kwani Yeye ‘anatufundisha ili tujifaidi wenyewe.’—Isaya 48:17, 18.

Kwa nini ni hatari kujiamulia kinachohitajiwa ili “kuwa mwema”? Sote tumerithi mwelekeo wa kutenda kwa ubinafsi. Mioyo yetu wenyewe inaweza kutudanganya. (Yeremia 17:9) Ni rahisi kupunguza umuhimu wa viwango vilivyotolewa na Mungu tunavyoona kuwa vigumu au vinavyotubana sana.

Kwa mfano, watu wawili ambao hawajaoana wanaweza kuamua kufanya ngono, wakifikiri kwamba kwa kuwa jambo hilo halimhusu mtu mwingine, basi ni uamuzi wa kibinafsi. Wanaweza kutambua kuwa wanachofanya hakilingani na viwango vya Biblia lakini wakate kauli kwamba ikiwa “hakuna mtu yeyote anayeumia,” Mungu hatapinga. Tamaa zao zinaweza kuwapofusha wasione madhara na matokeo kamili ya matendo yao. Biblia inaonya: “Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.”—Methali 14:12.

Sheria zote za Yehova huonyesha upendo wake kwa wanadamu na tamaa yake ya kutuepusha na kuteseka. Kutofuata viwango vya Mungu kuhusiana na ngono au matendo mengine, hakujawafanya wanadamu wawe na mafanikio au furaha zaidi. Wengi wamefanya maisha yao yawe magumu tu. Kwa upande mwingine, kufuata sheria za Mungu kunatusaidia kuishi maisha mazuri kwa sababu tunaepuka kujidhuru au kuwadhuru wengine.—Zaburi 19:7-11.

Ikiwa unatamani kuwa mtu mwema kwa maoni ya Mungu, jitahidi kufuata mwelekezo wake. Utajionea mwenyewe kwamba “amri za [Yehova] si mzigo mzito.”—1 Yohana 5:3.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Kwa nini tukubali mwongozo wa Yehova?Ufunuo 4:11.

▪ Ni lazima tutii amri zote za Mungu?1 Yohana 5:3.

▪ Kwa nini si jambo la hekima kujiwekea viwango vya maadili?Methali 14:12; Yeremia 17:9.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Je, una maoni kama ya Mungu kuhusu maadili?