Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa nini wengine hunitenga?

Kwa nini wengine hunitenga?

Vijana Huuliza . . .

Kwa nini wengine hunitenga?

“Kwenye miisho ya juma ni kana kwamba kila mtu huwa anafurahia maisha isipokuwa mimi.”—Renee.

“Vijana hukutana ili kujifurahisha bila kunihusisha!”—Jeremy.

NI SIKU nzuri, wewe huna mipango yoyote. Lakini, kila mtu ana mipango fulani. Marafiki wako wote wanafurahia siku yao. Lakini, kwa mara nyingine tena, wewe umesahauliwa!

Usipoalikwa unaweza kuhuzunika sana. Huenda ukaanza kujiambia, ‘Labda nina kasoro. Kwa nini hakuna yeyote anayetaka kushirikiana nami?’

Kwa Nini Jambo Hilo Linaumiza?

Ni jambo la kawaida kutamani kuwa na marafiki na kukubaliwa nao. Sisi tunahitaji kushirikiana na wengine. Kabla ya Hawa kuumbwa, Yehova alisema hivi kumhusu Adamu: “Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake.” (Mwanzo 2:18) Ni wazi kwamba watu waliumbwa washirikiane. Na hiyo ndiyo sababu mtu huumia sana anapotengwa.

Unaweza kuvunjika moyo ikiwa kila mara unatengwa au unahisi ni kama huwezi kufikia viwango vya watu unaotaka kuwa na urafiki nao. Msichana anayeitwa Marie anasema kwamba “kuna vikundi vya vijana ambao wamefanikiwa sana maishani, lakini unaweza kuhisi kwamba wao wanaona wewe hufai kuwa kati yao.” Wengine wanapokutenga, unajihisi mpweke.

Nyakati nyingine unaweza kujihisi mpweke hata ukiwa kwenye umati wa watu. Msichana mmoja anayeitwa Nicole anasema hivi: “Ingawa hilo linaonekana kama jambo la ajabu, ninakumbuka wakati mmoja nikijihisi mpweke sana wakati wa kikusanyiko fulani cha kirafiki. Nafikiri ni kwa sababu nilikuwa kati ya watu wengi lakini sikuwa na rafiki.” Wengine pia hujihisi wakiwa wapweke katika makusanyiko ya Kikristo. “Ni kana kwamba kila mtu anafahamiana na mtu isipokuwa mimi!” anasema Meagan. Msichana anayeitwa Maria ana maoni kama hayo. Anasema hivi: “Ni kana kwamba nimezungukwa na marafiki lakini sina marafiki.”

Hakuna yeyote ambaye hajihisi mpweke hata wale wanaodhaniwa kwamba wana furaha sana. Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Hata katika kicheko moyo unaweza kuwa na maumivu.” (Methali 14:13) Ikiwa upweke unaendelea kwa muda mrefu unaweza kukuathiri sana. Biblia inasema hivi: “Kwa sababu ya maumivu ya moyo roho hupata pigo.” Tafsiri nyingine inatafsiri mstari huo: “Huzuni inaweza kukuponda.” (Methali 15:13; Contemporary English Version) Ukijihisi umepondeka kwa sababu ya kutengwa, unaweza kufanya nini?

Kukabiliana na Upweke

Ili kukabiliana na upweke, jaribu kufanya mambo yafuatayo:

Fikiria sifa zako nzuri. (2 Wakorintho 11:6) Jiulize, ‘Ninaweza kufanya mambo gani vizuri?’ Fikiria una vipawa au sifa gani nzuri, kisha uziorodheshe hapa chini.

․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

Unapojihisi umetengwa jikumbushe mambo uliyoandika hapo juu. Ni kweli una udhaifu mbalimbali na unapaswa kuufanyia kazi. Lakini usiache udhaifu wako ukulemee. Badala yake, jifikirie kama nyumba nzuri ambayo inafanyiwa marekebisho. Huenda kila kitu hakiko sawa, lakini kuna mambo fulani ambayo yako sawa. Kazia fikira mambo hayo!

Panuka. (2 Wakorintho 6:11-13) Chukua hatua ya kwanza kufahamiana na watu. Ni kweli kwamba inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo. Liz, mwenye umri wa miaka 19, anasema: “Mtu anaweza kuona haya kuzungumza na kikundi cha watu, lakini ukimsalimu mmoja wao, mara moja unakuwa sehemu ya kikundi hicho.” (Ona sanduku “Mapendekezo ya Jinsi ya Kuanzisha Mazungumzo.”) Badala ya kulalamika kwamba unatengwa, hakikisha wewe humtengi yeyote, kama vile watu wenye umri mkubwa. “Nilipokuwa na umri wa miaka 10 au 11,” anakumbuka kijana anayeitwa Cori, “nilikuwa na rafiki mwenye umri mkubwa. Tulikuwa na uhusiano wa karibu, ingawa umri wetu ulikuwa umetofautiana sana.”

Fikiria watu wawili katika kutaniko lako wenye umri mkubwa ambao ungependa kufahamiana nao vizuri zaidi.

․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

Kwenye mkutano unaofuata, mbona usizungumze na mmoja kati ya watu uliowaandika hapo juu. Anzisha mazungumzo naye. Mwulize jinsi alivyoanza kujifunza Biblia. Kadiri unavyofahamiana zaidi na watu katika “ushirika mzima wa akina ndugu,” ndivyo utakavyopunguza hisia za upweke.—1 Petro 2:17.

Funua moyo wako. (Methali 17:17) Kumweleza mzazi au mtu mzima mwingine kuhusu wasiwasi wako kunaweza kupunguza hisia za upweke. Hivyo ndivyo msichana mwenye umri wa miaka 16 alivyogundua. Mwanzoni alihisi kwamba ametengwa. “Ningejiuliza ni kwa nini nilihisi kuwa wengine wamenitenga,” anasema, “na nilifikiria tena na tena yaliyofanyika. Kisha ningemweleza mama yangu, naye angenishauri jinsi ya kushughulikia hali hiyo. Kuzungumza husaidia sana.”

Unaweza kumwendea nani ukihitaji kuzungumza na mtu kuhusu hisia zako za upweke?

․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

Wafikirie wengine. (1 Wakorintho 10:24) Biblia inasema tunapaswa ‘twendelee kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yetu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’ (Wafilipi 2:4) Ni kweli, unapohisi kwamba wengine wanakutenga, ni rahisi kuhuzunika. Hata hivyo, badala ya kukata tamaa, kwa nini usimfanyie mtu mwenye uhitaji jambo fulani? Huenda ukaanzisha urafiki kwa njia hiyo!

Mfikirie mtu fulani, labda katika familia au kutaniko lenu, ambaye anaweza kufurahia kushirikiana nawe au kupata msaada wako. Andika jina la mtu huyo hapa chini, na ufafanue jinsi unavyoweza kumsaidia.

․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

Unapowafikiria wengine badala ya kujifikiria tu na kuwafanyia mambo, huwezi kujihisi mpweke. Kufanya hivyo kunaweza kukufanya uwe na mtazamo mzuri na mwelekeo unaofaa, na hivyo kukufanya uwe rafiki anayefaa. Methali 11:25 inasema: “Anayenywesha wengine kwa ukarimu yeye mwenyewe pia atanyweshwa kwa ukarimu.”

Chagua kwa uangalifu. (Methali 13:20) Ni vizuri kuwa na marafiki wachache wa kweli ambao wanakujali kuliko wengi wanaodai kuwa marafiki lakini wanaoweza kukuletea matatizo. (1 Wakorintho 15:33) Mfikirie kijana Samweli anayetajwa katika Biblia. Inawezekana kwamba alikuwa mpweke kwenye maskani. Alifanya kazi pamoja na watu kama Hofni na Finehasi, ambao matendo yao yaliwafanya wasiwe marafiki wazuri hata ingawa walikuwa wana wa kuhani mkuu. Ikiwa angeanzisha urafiki nao, Samweli angekufa kiroho! Lakini Samweli hakutaka kupatwa na hali hiyo! Biblia inasema hivi: “Na wakati huo wote mvulana Samweli alikuwa akiendelea kukua na kupendwa na Yehova na vilevile na wanadamu.” (1 Samweli 2:26) Wanadamu gani? Bila shaka hao si Hofni na Finehasi ambao huenda hata walimpuuza Samweli kwa sababu ya matendo yake mazuri. Sifa nzuri za Samweli zilimfanya apendwe na waliothamini viwango vya Mungu. Watu wanaompenda Yehova ndio marafiki wanaofaa!

Uwe na mtazamo mzuri. (Methali 15:15) Mara kwa mara kila mtu hujihisi mpweke. Unaweza kufanya nini? Badala ya kufikiria mambo yasiyofaa, jaribu kuwa na mtazamo mzuri. Kumbuka, ingawa hutaweza kudhibiti kila kitu kinachotendeka maishani mwako, unaweza kudhibiti maoni yako.

Unapohisi kwamba umetengwa, chukua hatua za kubadili hali unayokabili au hatua za kubadili maoni yako. Sikuzote kumbuka kwamba Yehova anajua jinsi ulivyoumbwa, hivyo anajua mahitaji yako na jinsi yanavyoweza kutimizwa vizuri. Ikiwa hisia za upweke zinaendelea, sali kwa Yehova. Uwe na hakika kwamba yeye “mwenyewe atakutegemeza.”—Zaburi 55:22.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Ninapaswa kuchukua hatua gani ikiwa ninahisi kwamba nimetengwa?

▪ Ni maandiko gani yanayoweza kunisaidia kujichunguza vizuri badala ya kujihukumu?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]

Mapendekezo ya Jinsi ya Kuanzisha Mazungumzo

Tabasamu. Uchangamfu wako unaweza kuwafanya wengine waongee nawe.

Jitambulishe. Watajie jina lako na mahali unakotoka.

Uliza maswali. Bila kuingilia maisha ya ndani ya mtu, uliza maswali hususa kuhusu historia ya mtu huyo.

Sikiliza. Badala ya kufikiria kile utakachosema mwenzako anapoongea, sikiliza. Swali au sentensi itakayofuata itakuja yenyewe tu.

Tulia! Maongezi yanaweza kukusaidia kuanzisha urafiki. Kwa hiyo furahia mazungumzo!