Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwongozo Bora Kuliko Silika

Mwongozo Bora Kuliko Silika

Mwongozo Bora Kuliko Silika

“Ikiwa kila mtu ataruhusiwa kujichagulia maadili yake, bila kuwa na kanuni za kuamua ikiwa maadili hayo ni sawa, basi lazima sheria itatumiwa kuhakikisha kwamba kuna tabia nzuri.” —DAKT. DANIEL CALLAHAN.

TUNAWEZA kuona ukweli wa maneno ya Callahan kwani watu wanazidi kupuuza kanuni za maadili hivi kwamba katika sehemu nyingi ulimwenguni, serikali zimelazimika kuweka sheria nyingi ili kuzuia uhalifu. Katika mkutano wa kwanza kabisa wa Kongamano la Akina Mama wa Nigeria, rais wa Nigeria alieleza mahangaiko yake kuhusu wakati ujao wa taifa hilo. Hakuwa akifikiria siasa au umaskini, bali “tatizo zito zaidi,” yaani, “kumomonyoka kwa . . . maadili ya msingi katika familia, kazini, katika jamii na hata katika taifa zima.”

Uchunguzi uliofanyiwa akina mama 1,736 nchini Uingereza ulionyesha kwamba “familia zinazorota kwa sababu ya kuporomoka kwa maadili na kuongezeka kwa familia zenye mzazi mmoja.” Vilevile, maadili yanaporomoka kwa kasi nchini China. Gazeti Time linaripoti kwamba watu wanaanza kufanya ngono mapema zaidi maishani na wana wapenzi wengi kuliko zamani. “Haya ni maisha yangu, nami naweza kufanya chochote ninachotaka,” akasema msichana mmoja Mchina ambaye alijivunia kuwa na zaidi ya wapenzi 100.

Kuporomoka kwa maadili kumewaathiri pia wenye mamlaka. “Watu hawawaoni viongozi wao kuwa mifano ya kuigwa kiadili,” akasema Javed Akbar katika gazeti la Kanada Toronto Star. Aliongezea kusema kwamba wanasiasa, wasimamizi wa mashirika, na pia viongozi wa kidini “wanaonekana kuwa hawana maadili mazuri.”

Kwa Nini Maadili Yameporomoka?

Mambo kadhaa yamechangia hali hiyo. Jambo moja ni roho ya kuasi kanuni ambazo zimekuwepo kwa muda mrefu. Kwa mfano, uchunguzi uliofanywa Kusini mwa Marekani ulionyesha kwamba wanafunzi wengi wa chuo kikuu waliamini “mtu anapaswa kujiamulia mwenyewe tofauti kati ya mema na mabaya.”

Mwandishi wa mambo ya kisiasa Zbigniew Brzezinski alitaja sababu nyingine. Aliandika kwamba watu leo “hukazia kutosheleza tamaa zao, na kwamba anasa ndilo jambo linaloamua jinsi tabia za watu zitakavyokuwa.” Uhuru na uwezo wa kufanya maamuzi yanayopatana na maadili, ubinafsi, na kujitosheleza tu kunaweza kukuvutia, lakini je, kunasaidia uwe na furaha ya kweli, uradhi, na uhusiano mzuri zaidi pamoja na wengine?

“Hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake,” akasema Yesu. (Mathayo 11:19) Je, kuporomoka kwa maadili kumewafanya watu wawe na furaha na uradhi zaidi? Fikiria matokeo kadhaa: kiwango cha kutowaamini wengine kimeongezeka, hakuna usalama, uhusiano unavunjika, watoto wanakua bila baba au mama, magonjwa ya kuambukiza yanayopitishwa kingono, mimba zisizotakiwa, uraibu wa dawa za kulevya, na jeuri. Mambo haya hayaonyeshi uradhi na kufanikiwa badala yake ni huzuni na kushindwa.—Wagalatia 6:7, 8.

Baada ya kuona matatizo kama hayo katika siku zake, nabii wa Mungu, Yeremia, alisema hivi: “Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Ndiyo, Mungu hakutuumba tujiongoze, yaani, tujiamulie mema na mabaya. Kinachoonekana kuwa kizuri kwetu kinaweza kudhuru. Methali 14:12 inasema: “Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.”

Adui Aliye Ndani Yetu!

Kwa nini tunahitaji mwongozo kuhusiana na maadili? Kwa sababu mioyo yetu inaweza kutudanganya. Biblia inasema hivi katika Yeremia 17:9: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?” Ukijua mtu ni mwenye hila na hatari, ungemwamini? La hasha! Hata hivyo, kila mmoja wetu ana moyo ambao una sifa hizohizo. Kwa hiyo, Mungu anatupa onyo hili: “Anayetegemea moyo wake mwenyewe ni mjinga, lakini yeye anayetembea katika hekima ndiye atakayeponyoka.”—Methali 28:26.

Hiyo ndiyo njia ya kufanikiwa: Badala ya kutegemea kutokamilika kwetu, tunahitaji kutembea kupatana na hekima ya kimungu na hivyo kujiokoa dhidi ya vikwazo vingi. Pia, wote wanaotaka wanaweza kupata hekima. “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.”—Yakobo 1:5.

Mtumaini Mungu “Kwa Moyo Wako Wote”

Ikimfafanua Muumba wetu, Biblia inasema: “Yeye Mwamba, kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki; yeye ni mwadilifu na mnyoofu.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Ndiyo, Yehova ni kama mwamba mkubwa. Tunaweza kumtegemea kikamili ili kupata mwongozo unaofaa wa kiadili na wa kiroho haidhuru ni mabadiliko gani yanayotokea. Methali 3:5, 6 inasema: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”

Kwa kweli, ni nani anayeweza kutupa mwongozo unaofaa isipokuwa Muumba wetu, ambaye huhesabu “nywele zenyewe za kichwa [chetu]”? (Mathayo 10:30) Isitoshe, amejionyesha kuwa rafiki wa kweli, anayetupenda vya kutosha kutueleza ukweli wakati wote, hata wakati ambapo ukweli huo unauma.—Zaburi 141:5; Methali 27:6.

Pia, Yehova hatulazimishi tufuate mwongozo wake. Badala yake, yeye hutuhimiza kwa upendo. “Mimi, Yehova, [ndiye yule] . . . anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake. Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.” (Isaya 48:17, 18) Je, huvutiwi na Mungu mwenye sifa hizo? Zaidi ya hayo, amefanya hekima yake ipatikane kupitia Neno lake, Biblia Takatifu, kitabu ambacho kimechapishwa kwa wingi kuliko kitabu kingine chochote ulimwenguni!—2 Timotheo 3:16.

Acha Neno la Mungu Liongoze Njia Zako

Akizungumza kuhusu Maandiko Matakatifu, mtunga-zaburi aliandika hivi: “Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru kwa barabara yangu.” (Zaburi 119:105) Taa ya mguu wetu hutuonyesha hatari za sasa, huku nuru kwa ajili barabara yetu ikituonyesha mambo ya wakati ujao. Kwa ufupi, Neno la Mungu linaweza kutuongoza kwa usalama maishani kwa kutusaidia kufanya maamuzi ya hekima yanayopatana na maadili katika mambo yote, maamuzi yanayoathiri mambo ya sasa na yanayoweza kutuathiri wakati ujao.

Kwa mfano, fikiria Mahubiri ya Mlimani. Katika hotuba hiyo fupi iliyorekodiwa katika Mathayo sura ya 5 hadi 7, Yesu Kristo alizungumza kuhusu furaha, upendo, chuki, maadili, sala, kufuatia utajiri, na mambo mengine yanayoweza kutusaidia leo kama yalivyowasaidia watu wakati huo. Maneno yake yalikuwa yenye kuelimisha sana hivi kwamba “umati ukashangazwa na njia yake ya kufundisha.” (Mathayo 7:28) Kwa nini usijisomee mahubiri hayo? Huenda wewe pia utavutiwa nayo.

“Endeleeni Kuomba” Msaada wa Mungu

Ni kweli kwamba kufanya kilicho sawa machoni pa Mungu si rahisi nyakati zote. Isitoshe, pambano lililo ndani yetu dhidi ya dhambi linafananishwa katika Biblia na vita. (Waroma 7:21-24) Hata hivyo, kwa msaada wa Mungu tunaweza kushinda vita hivyo. “Endeleeni kuomba,” Yesu akasema, “nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata . . . Kwa maana kila mtu anayeomba hupokea, na kila mtu anayetafuta hupata.” (Luka 11:9, 10) Naam, Yehova hatamwacha mtu yeyote anayejaribu kwa unyoofu kutembea katika barabara nyembamba inayoongoza kwenye uzima wa milele.—Mathayo 7:13, 14.

Fikiria mfano wa Frank, ambaye alikuwa na uraibu wa kutumia tumbaku alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Baada ya kusoma andiko la 2 Wakorintho 7:1 na kukata kauli kwa usahihi kwamba kwa maoni ya Mungu zoea lake lilikuwa “unajisi wa mwili,” Frank aliacha kuvuta sigara. Hata hivyo, haikuwa rahisi kudumisha uamuzi wake. Pindi moja alijikuta akitambaa sakafuni akitafuta vishungi vya sigara ili avute!

Tabia hiyo yenye kushusha heshima ilimwonyesha jinsi alivyokuwa mtumwa wa tumbaku. (Waroma 6:16) Hivyo, alisali ili apate msaada, akashirikiana kwa ukaribu na marafiki wenye kujenga wa kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova la kwao, naye akashinda zoea hilo.—Waebrania 10:24, 25.

Tosheleza Mahitaji Yako ya Kiroho

Kisa cha Frank ni moja tu kati ya visa vingi vinavyoonyesha kwamba Biblia inatoa mwongozo bora zaidi wa kiadili na wa kiroho, kutia ndani kichocheo cha kutenda kulingana na mwongozo huo. Si ajabu kwamba Yesu alisema: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.”—Mathayo 4:4.

Tunapokubali na kufuata kweli za Mungu zenye thamani, tunanufaika katika kila njia, iwe ni kiakili, kihisia, kiroho, na kimwili. Zaburi 19:7, 8 inasema: “Sheria ya Yehova ni kamilifu, huirudisha [au, kuifufua] nafsi. . . . Maagizo kutoka kwa Yehova ni manyoofu, huufanya moyo ushangilie, amri ya Yehova ni safi, huyafanya macho yang’ae [kwa tumaini na kwa sababu ya kuona wazi kusudi la Mungu].”

Yehova hutupa mengi zaidi ya mwongozo unaofaa wa maadili na maisha bora wakati huu, kupitia Neno lake. Yeye hutujulisha mengi kuhusu wakati ujao. (Isaya 42:9) Kama makala inayofuata inavyoonyesha, kuna wakati ujao mzuri kwa wote wanaokubali mwongozo wa Mungu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Mwongozo Wako wa Maadili

Wanadamu wana zawadi yenye thamani, yaani, dhamiri. Kwa sababu hiyo, watu wa kila taifa na kabila, kutia na kila enzi, wamekuwa na sheria za maadili zinazofanana. (Waroma 2:14, 15) Hata hivyo, haimaanishi kwamba dhamiri haiwezi kukuongoza vibaya; inaweza kuathiriwa na dini ya uwongo, falsafa za wanadamu, ubaguzi, na tamaa mbaya. (Yeremia 17:9; Wakolosai 2:8) Hivyo, kama vile rubani anavyohitaji kurekebisha vifaa vyake vya kumwongoza, tunahitaji kuchunguza, na inapohitajika, tunahitaji kurekebisha mwongozo wetu wa kiadili na wa kiroho kulingana na viwango vyenye uadilifu vya “Mpaji-sheria wetu,” Yehova Mungu. (Isaya 33:22) Tofauti na viwango vya maadili vya wanadamu vinavyoweza kubadilika kutoka kizazi kimoja hadi kingine, viwango vikamilifu vya Mungu vinadumu milele. Mungu anasema hivi: “Mimi ni Yehova; sikubadilika.”—Malaki 3:6.

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Mwongozo wa Kupata Mafanikio na Furaha

KUPATA FURAHA

“Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—MATHAYO 5:3.

“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—MATENDO 20:35.

“Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”—LUKA 11:28.

KUTEGEMEKA

“Semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake.”—WAEFESO 4:25.

“Mwizi asiibe tena.”—WAEFESO 4:28.

“Ndoa na iheshimiwe kati ya wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi.”—WAEBRANIA 13:4.

KUJITAHIDI KUWA NA MAHUSIANO MAZURI

“Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”—MATHAYO 7:12.

“[Mume] na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; . . . mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”—WAEFESO 5:33.

“Endeleeni . . . kusameheana kwa hiari.”—WAKOLOSAI 3:13.

KUEPUKA NA KUTATUA UGOMVI

“Msimlipe yeyote uovu kwa uovu.”—WAROMA 12:17.

“Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. . . . Hauweki hesabu ya ubaya.”—1 WAKORINTHO 13:4, 5.

“Jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.”—WAEFESO 4:26.