Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fundisha kwa Kuweka Kielelezo

Fundisha kwa Kuweka Kielelezo

Hatua ya 7

Fundisha kwa Kuweka Kielelezo

Kwa nini hatua hii ni muhimu? Matendo hufundisha. Mara nyingi maneno hueleza tu jambo. Kwa mfano, wazazi wanaweza kuwaambia watoto wao wawe na heshima na waseme ukweli. Hata hivyo, ikiwa wazazi haohao hufokeana au huwafokea watoto wao na kusema uongo ili kuhepa majukumu wasiyotaka kutekeleza, wanawafundisha watoto wao kwamba watu wazima wanapaswa kutenda hivyo. Kuwaiga wazazi ni “mojawapo ya njia bora ambazo watoto hujifunza,” anasema mwandishi Dakt. Sal Severe.

Tatizo: Wazazi si wakamilifu. “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu,” akaandika mtume Paulo. (Waroma 3:23) Kuhusu kudhibiti maneno yetu, mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Ulimi, hakuna hata mmoja wa wanadamu anayeweza kuufuga.” (Yakobo 3:8) Isitoshe ni jambo la kawaida kwa watoto kuwaudhi sana wazazi. “Nilishangazwa na jinsi watoto wangu walivyonifanya nikasirike sana,” anasema Larry, baba ya watoto wawili ambaye kwa kawaida huwa mtulivu na hujidhibiti.

Suluhisho: Jitahidini kuwa vielelezo bora, si wazazi wakamilifu. Na mtumie makosa mnayofanya mara kwa mara kuwafundisha watoto wenu. “Ikiwa ningewakasirikia watoto wangu au ikiwa ningefanya uamuzi mbaya ambao ungewaathiri,” anasema Chris baba ya watoto wawili, “ningekubali kosa langu na kuomba msamaha. Hilo liliwafundisha watoto wangu kwamba wazazi pia hufanya makosa na kwamba sisi sote tunapaswa kujitahidi kuboresha mwenendo wetu.” Kostas, aliyetajwa awali anasema: “Nimegundua kwamba ninapoomba msamaha kwa sababu ya kukasirika, binti zangu wanajifunza kuomba msamaha wao wanapokosea.”

Yehova Mungu anasema: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Waefeso 6:4) Mtu aliye na mamlaka anaposema jambo moja na kufanya kinyume, hilo huwakasirisha watoto kama, au hata zaidi ya, linavyowakasirisha watu wazima. Kwa hiyo, mbona usijiulize maswali haya kila siku: Ikiwa nisingesema chochote siku nzima, watoto wangu wangejifunza nini kutokana na matendo yangu? Je, hayo ndiyo mambo ninayojaribu kuwafundisha kwa maneno?

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe?”—Waroma 2:21

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mzazi anapoomba msamaha, mtoto anajifunza kufanya vivyo hivyo