Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kumwabudu Mungu Kunaweza Kufurahisha?

Je, Kumwabudu Mungu Kunaweza Kufurahisha?

Maoni ya Biblia

Je, Kumwabudu Mungu Kunaweza Kufurahisha?

MTU mmoja anayedai kuwa Mkristo aliandika hivi: “Mimi ninamwamini na kumpenda Mungu. Lakini . . . kwenda kanisani hunichosha sana.” Je, wewe una maoni kama hayo? Ukweli ni kwamba watu wameanzisha njia zao wenyewe za kumtumikia Mungu kwa sababu makanisa yamewachosha, hayajatosheleza mahitaji yao, na yamewakatisha tamaa.

Hivi karibuni gazeti moja lilisema kwamba watu wengi leo wanaanzisha tu njia zao za kuabudu. Lakini kufanya hivyo hakuwezi kumtosheleza mtu yeyote anayetaka kufurahia kumwabudu Mungu. Kwa nini? Kwa sababu anaweza kupatwa tena na hisia zilezile za kukata tamaa zilizomfanya atoke katika kanisa alilokuwa.

Hilo linatokeza swali, Je, kuishi kulingana na mafundisho ya Biblia kunachosha, na hakuleti shangwe? Bila shaka la! Kwa mfano, fikiria maneno haya ya mtunga-zaburi wa Biblia: “Njooni tumpigie Yehova vigelegele kwa shangwe! . . . Ingieni, tuabudu na kuinama; na tupige magoti mbele za Yehova Mtengenezaji wetu.”—Zaburi 95:1, 6.

Mtunga-zaburi mwingine wa Biblia alimwimbia Yehova hivi kwa uthamini: “Wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Katika Maandiko, Yehova anaitwa “Mungu mwenye furaha,” na mara nyingi waabudu wake, wa kale na wa leo, wameeleza kuhusu shangwe yao.—Zaburi 83:18; 1 Timotheo 1:11.

Sababu ya Kuwa na Shangwe

Sababu kuu ya kuwa na shangwe ya kweli katika ibada yetu ni kutambua kile ambacho Yehova amefanya kutuonyesha upendo. Amefanya nini? “Mungu aliupenda ulimwengu [wanadamu] sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee [Yesu Kristo], ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

Kwa hiyo, kama Biblia inavyosema, mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:3, 4) Hiyo haimaanishi kujua tu yale ambayo mistari fulani ya Biblia inasema. Badala yake, tunahitaji ‘kuelewa maana’ ya kile tunachosoma, na hivyo lazima tujifunze kwa makini sana. (Mathayo 15:10) Faida ya kufanya hivyo ni: “Utapata kumjua Mungu.” Hilo linaweza kufurahisha kama nini!—Methali 2:1-5.

Katika karne ya kwanza, watu katika jiji la Beroya huko Makedonia walipata shangwe kama hiyo. Mtume Paulo alipowafundisha Neno la Mungu, “walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.” Hawangekuwa na hamu kama hiyo ikiwa kujifunza Maandiko kungewachosha au hakungewafurahisha.—Matendo 17:11.

Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa watashibishwa.” (Mathayo 5:6) Kama watu walio na njaa ambao wameanza kula kwa kawaida, wengi leo wameshangilia kuona njaa yao ya kiroho ikitoshelezwa. Hivyo, kama Waberoya, “wengi kati yao [wamekuwa] waamini.”—Matendo 17:12.

Njia ya Maisha

Waabudu wa kweli katika karne ya kwanza walifuata “Ile Njia,” maneno yanayotumiwa katika Matendo 9:2 kumaanisha njia mpya ya maisha ambayo Wakristo wa mapema walifuata. Leo, wale wanaotaka kupata shangwe katika kumtumikia Mungu wanapaswa kufanya hivyo. Wanahitaji kuruhusu kweli za Biblia ziathiri kufikiri kwao na mwenendo wao wa kila siku.

Hivyo, mtume Paulo aliwahimiza watu huko Efeso: ‘Ondoleeni mbali utu wa zamani unaolingana na mwenendo wenu wa kwanza.’ Hata hivyo, mengi zaidi yanahitajika, kama Paulo alivyoendelea kusema: ‘Vaeni utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.’—Waefeso 4:22-24. *

Tunapotenda kulingana na mashauri hayo huku tukifanya mabadiliko maishani kupatana na mapenzi ya Mungu, tunakuwa na nafasi ya kupata shangwe na kuridhika. Mambo hayo yanapatikanaje? Paulo aliwaandikia Wakristo wa Kolosai kwamba walihitaji kufanya mabadiliko maishani ‘ili watembee kwa kumstahili Yehova kwa kusudi la kumpendeza yeye kikamili.’ (Wakolosai 1:10) Kwa kweli, kujua kwamba Mungu wa kweli anapendezwa na maisha yetu kunatufanya kuwa na shangwe! Isitoshe, Mungu hufanya iwezekane kumpendeza “kikamili.” Kwa njia gani? Kwa kutusamehe.

Kila mmoja wetu hufanya dhambi; sisi sote tunahitaji kusamehewa na Mungu. Paulo alisema hivi katika 1 Timotheo 1:15: “Kristo Yesu alikuja ulimwenguni ili kuwaokoa watenda-dhambi.” Yesu alipodhabihu uhai wake kwa ajili yetu, alifanya iwezekane kwetu kusamehewa dhambi. Hivyo, moyo wa mwabudu wa kweli hutulizwa kutokana na mzigo mzito wa hatia. Anaweza kuwa na dhamiri safi na ashangilie kwa sababu ya kuwa na hakika kwamba maadamu anafanya mapenzi ya Mungu, atasamehewa dhambi zake.

Sababu Nyingine ya Kuwa na Shangwe

Mtu anapoanza kumwabudu Mungu wa kweli, hayuko peke yake. Mtunga-zaburi wa Biblia Daudi aliandika: “Nilishangilia walipokuwa wakiniambia: ‘Na twende katika nyumba ya Yehova.’” (Zaburi 122:1) Kwa kweli, kukutana na watumishi wengine wa kweli kwa kawaida huongeza sana shangwe yetu.

Baada ya kuhudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova, mtu mmoja aliandika hivi: “Tulikaribishwa kwa fadhili na tukasaidiwa sana, na hilo linaonyesha kwamba kuna umoja kati ya wote waliohudhuria. Vijana waliokuwako walikuwa watulivu sana. Bila shaka wao na wazazi wao hujivunia jambo hilo. Ningependa kushukuru sana kwa kukaribishwa kwenye mkutano huo wenye kupendeza.”

Kama Daudi aliyeishi zamani, wewe pia unaweza kufurahia nafasi za kumwabudu Yehova. “Mtumikieni Yehova kwa kushangilia,” akasihi. “Njooni mbele zake kwa vigelegele vya shangwe.” (Zaburi 100:2) Wote ambao humtumikia Mungu kwa nia nzuri wanaweza kutazamia kwamba ibada yao itakuwa yenye kufurahisha.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Msingi wa ibada ya kweli ni nini?1 Timotheo 2:3-6.

▪ Dhabihu ya fidia ya Kristo hutusaidiaje kupata shangwe?1 Timotheo 1:15.

▪ Mikutano ya Kikristo inaweza kuchangiaje furaha yetu katika ibada?Zaburi 100:1-5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Ukisoma Waefeso sura ya 4 na Wakolosai sura ya 3, utaona wazi ni nini kinachohitajika ili kubadili utu.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kujiunga na wengine katika funzo la Biblia kunaweza kufurahisha