Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninapenda Muziki, Maisha, na Biblia

Ninapenda Muziki, Maisha, na Biblia

Ninapenda Muziki, Maisha, na Biblia

Limesimuliwa na Boris N. Gulashevsky

Hebu wazia mwanamume mwenye umri wa miaka 65 hivi, ambaye amepatwa na mshtuko wa moyo mara mbili. Huku machozi yakimtoka anamshukuru Mungu kwa kumruhusu amjue. Hayo ni matukio ya maisha yangu miaka 11 iliyopita.

NILIZALIWA mwaka wa 1930 huko Ukrainia katika kijiji cha Tsibulev katika wilaya ya Cherkassy. Mnamo 1937, wakati wa utawala wenye kukandamiza wa Stalin, baba yangu alikamatwa na kuhukumiwa kuwa “adui wa Serikali.” Nyumba yetu ilitaifishwa, na marafiki wengi walituepuka. Baadaye wengi wao walifungwa pia. Hizo zilikuwa nyakati zenye hofu, kutoaminiana, na kusalitiana.

Miezi miwili baada ya Baba kukamatwa, dada yangu, Lena, alizaliwa. Wakati wa majira ya baridi, mimi, Mama, Lena, na kaka yangu Nikolai, tuliishi katika chumba kidogo ambacho hakikuwa na madirisha wala jiko. Baadaye, tulienda kuishi na babu yangu. Mimi na Nikolai tuliitunza nyumba, tukapasua kuni, na kufanya ukarabati. Nilifurahia kufanya kazi kwa mikono yangu. Pia, nilitengeneza viatu na kufanya useremala. Kwa sababu nilipenda muziki, nilitengeneza ala ya muziki iitwayo balalaika kwa kutumia mbao na nikajifunza kuipiga. Baadaye, nilijifunza kupiga gitaa na gambusi.

Nilipokuwa mdogo nilibatizwa katika Kanisa Katoliki. Lakini kwa sababu sikuelewa mafundisho au desturi za kanisa hilo, niliona kwamba maoni ya kuwa hakuna Mungu yanapatana na akili. Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu nilijiunga na kikundi cha vijana Wakomunisti cha Komsomol, na wakati wowote tulipopata nafasi tulibishana na watu waliomwamini Mungu na kujaribu kuwathibitishia kwamba hakuna Mungu.

Napoteza Uwezo wa Kuona

Baada ya Wajerumani kushambulia Muungano wa Sovieti mnamo 1941, vita vingi vilipiganwa karibu na kijiji chetu wakati wa vita vya ulimwengu vya pili. Machi 16, 1944 (16/3/1944), nilijeruhiwa bomu moja lilipolipuka na nikawa kipofu. Nilianza kuwa na maumivu, kushuka moyo, na pia kukosa tumaini.

Vita viliposonga upande wa magharibi na Wajerumani wakalazimishwa kurudi nyuma, nilianza kutembea kwenye bustani na kusikiliza ndege wakiimba. Mama alianza kunipa vodka ninywe kwa sababu ya kunihurumia, nao majirani walinialika kwenye burudani zao ili niwapigie vyombo vya muziki. Nilivuta sigara, na ili kujiondolea huzuni nilianza kunywa pombe. Lakini baada ya muda nilitambua kwamba hilo halikusuluhisha matatizo yangu.

Shangazi yangu ambaye ni mwalimu, aliposikia kuhusu shule za vipofu, alimwomba Mama anipeleke katika shule moja kati ya hizo. Mnamo 1946, nilianza masomo yangu katika shule ambayo leo inaitwa Kam’yanets’-Podil’s’kyy. Nilijifunza kusoma na kuandika maandishi ya vipofu. Pia, niliendelea na masomo ya muziki, na nikatumia saa nyingi nikijifunza kupiga concertina. Baada ya kuona jitihada zangu, naibu wa mwalimu mkuu aliniruhusu nipige kodiani yake. Pia nilijifunza kupiga piano.

Najenga Nyumba Yangu

Mnamo 1948, nilimwoa mwalimu mmoja katika shule hiyo ambaye alikuwa amenisaidia katika masomo yangu. Mume wake alikufa wakati wa vita na kumwachia mabinti wawili wachanga. Baada ya kuhitimu, nilianza kuishi kwenye nyumba yake. Nilijaribu kuwa mume na baba mzuri na nilipata riziki kwa kupiga ala za muziki. Kisha mwaka wa 1952, tulipata mtoto.

Nilifanya mipango ya kujenga nyumba kwa ajili ya familia yetu, niliwaajiri watu wachimbe msingi na kujenga kuta, lakini mambo mengi nilijifanyia mwenyewe. Kwa sababu nisingeweza kuona, niliwazia na kugusa vitu ili kuvibuni. Ningeshika kipande cha mbao mkononi, nikiguse, kisha nikiwazie akilini. Baada ya hapo ningetengeneza vitu mbalimbali kutia ndani vifaa vya ujenzi vya mbao. Lakini nilinunua vifaa vya chuma kwenye viwanda. Nilitengeneza sehemu ya jiko la matofali, fanicha, na kufanya mambo mengine.

Okestra ya Filimbi

Niliendeleza masomo yangu ya muziki na nikawa nautumia kujipatia riziki. Baada ya kujifunza kupiga ala mbalimbali za muziki, nilijifunza kupiga filimbi. Wakati mmoja, nilirekebisha filimbi ndogo iliyotengenezwa kwa mianzi. Muda si muda, nilijifunza kutengeneza filimbi zangu mwenyewe. Wakati huo, wataalamu walifikiri haiwezekani kutengeneza filimbi zinazotoa sauti nzito kwani filimbi zilikuwa kubwa sana na hivyo sauti iliyotokezwa ilikuwa ya chini sana. Hiyo ndiyo sababu hakukuwa na okestra za filimbi.

Hata hivyo, nilifaulu kutengeneza filimbi yenye kifaa cha kuongezea mvumo, au sauti. Hilo lilimaanisha kwamba filimbi zenye sauti nzito zingeweza kutengenezwa. Baada ya muda, nilianza kutengeneza filimbi ambazo zingepigwa kwa mfuatano ili kutoa viwango mbalimbali vya sauti nzito.

Kabla ya hapo nilikuwa nimepanga okestra zilizotumia ala za kitamaduni. Mojawapo ya okestra zangu ilikuwa na wanamuziki vipofu peke yao. Mnamo 1960, nilipanga okestra ambayo ilipiga filimbi tu. Hiyo ilikuwa ya kwanza ya aina hiyo katika Muungano wa Sovieti au hata labda ulimwenguni pote.

Ugunduzi na Mashaka

Mnamo 1960, mtaalamu mmoja alinirekebishia ala fulani za muziki, naye alianza kuzungumza kuhusu dini. Kama kawaida, nilibishana naye na kudai kwamba hakuna Mungu. Aliniambia kwanza nisikilize kile ambacho angesoma katika Biblia. Na kwa sababu sikuwa nimeisoma Biblia, niliamua kusikiliza.

Niliguswa sana na simulizi la Yakobo ambalo linaeleza jinsi alivyofanya kazi kwa bidii ili atosheleze mahitaji ya familia yake. Nilitokwa na machozi niliposikiliza simulizi la Yosefu linaloeleza jinsi alivyouzwa na ndugu zake utumwani, majaribu yake, na jinsi alivyowasamehe ndugu zake. (Mwanzo, sura ya 37, 39-45) Pia niliipenda sana ile Kanuni Bora, inayosema tuwatendee wengine jinsi tunavyotaka watutendee. (Mathayo 7:12) Mambo hayo yalinifanya niijue Biblia na niipende.

Nilianza kuhudhuria ibada za Wabaptisti pamoja na rafiki yangu aliyenieleza kuhusu Biblia. Huko nilipewa “Agano Jipya” katika maandishi ya vipofu na nikaanza kuisoma kwa uangalifu. Hata hivyo, nilipoisoma, niligundua kwamba kuna tofauti kati ya yale ambayo Biblia inasema na mafundisho ya Wabaptisti. Kwa mfano, Biblia inamzungumzia Mungu na Yesu kuwa watu wawili tofauti na kwamba Mungu ni mkuu kuliko Yesu. (Mathayo 3:16, 17; Yohana 14:28; Matendo 2:32) Hata hivyo, Wabaptisti wanasisitiza kwamba hakuna tofauti kati ya Mungu na Yesu na kwamba wao ni sehemu ya Utatu. Nilisoma “Agano Jipya” mara nyingi, nikigusa kila neno lakini sikupata fundisho hilo.

Katika tafsiri ya Biblia tuliyokuwa nayo, maneno “moto wa mateso” yalitumiwa. Nilijaribu kuwazia moto huo ambao Wabaptisti waliufafanua kuwa mahali pa mateso. Hilo liliniudhi sana! Biblia inasema kwamba Mungu ni upendo, na nisingeweza kumwazia akitengeneza mahali kama hapo. (1 Yohana 4:8) Baada ya muda, mashaka yangu kuhusu moto wa mateso na mafundisho mengine ya Wabaptisti yaliongezeka.

Mabadiliko Makubwa

Kufikia mwaka wa 1968, binti zangu wa kambo walikuwa wameolewa na walikuwa na watoto. Wakati huo, mimi na mke wangu tulikuwa na matatizo makubwa katika ndoa yetu. Nikifikiria nyakati hizo, ninajuta kwamba hatukuonyeshana upendo na subira kama tulivyopaswa. Tulitalikiana, na ndoa zangu mbili zilizofuata ziliishia kwenye talaka pia.

Mnamo 1981, baada ya kuishi Kam’yanets’-Podil’s’kyy kwa miaka 35, nilihama na kwenda mji wa Yoshkar-Ola ulio kilomita 600 hivi mashariki mwa Moscow. Nikiwa huko niliendelea na ubunifu wangu. Okestra yangu moja ilikuwa na wanamuziki 45 waliopiga filimbi tofauti-tofauti. Kati ya hizo filimbi, nyingine zilikuwa na urefu wa sentimita 20 na zilitoa sauti nyembamba, nyingine za kipenyo cha sentimita moja, nazo nyingine zenye urefu wa mita tatu na kipenyo cha sentimita 20 na zilitoa sauti nzito. Maonyesho yetu yalitangazwa kwenye redio na kwenye televisheni, pia tulikuwa na maonyesho mengi kotekote nchini.

Katika mashindano yaliyohusisha vikundi vya muziki kutoka sehemu zote za Muungano wa Sovieti mwaka wa 1986, nilipewa cheti na medali kwa sababu ya kukuza muziki wa filimbi. Miaka mingi baadaye, sinema inayoitwa Solo for Pipe, or the Fairy Tale of a Musician ilitokezwa. Gazeti Mariiskaya Pravda liliripoti hivi: “Boris Nikolaievich Gulashevsky anayezungumziwa katika sinema hii, alipata cheti cha pekee kwa kuanzisha okestra ya filimbi kwa sababu hakuna nyingine kama hiyo nchini Urusi.”

Kuitafuta Kweli

Nilipohamia Yoshkar-Ola, nilijiandikisha kwenye maktaba moja iliyokuwa na vitabu vingi kwa ajili ya vipofu. Usomaji wangu ulinisaidia kujua mafundisho ya Wakatoliki, Wapentekoste, na Wamethodisti. Pia, nilihudhuria ibada ya Kanisa Othodoksi. Lakini nilishangaa kugundua kwamba walifundisha mambo yaleyale yasiyotegemea Biblia kama Wabaptisti.

Katika kitabu chake, Alexander Men, kasisi wa Kanisa Othodoksi, aliandika kwamba Mungu ana jina la kibinafsi—Yahweh. Pia aliandika kwamba wakati fulani Wayahudi walikuwa na ibada safi, lakini baadaye ilipotoshwa na mafundisho ya kipagani na ibada ya sanamu. Maandishi ya kasisi huyo yalinipendeza sana na kuimarisha tamaa yangu ya kuitafuta kweli.

Azimio Imara

Katika okestra yangu moja, kulikuwa na mwanamuziki aitwaye Liza ambaye alikuwa hawezi kuona vizuri. Tulioana mnamo 1990, naye pia akapendezwa na mambo ya kiroho. Mwaka huohuo, nilienda kumtembelea mama yangu ambaye aliishi na dada yangu Lena, huko Baranovichi, Belarus. Mama aliniomba niende kwenye Kanisa Katoliki na huko nilikula Sakramenti. Huo ulikuwa wakati wa mabadiliko ya kisiasa katika Muungano wa Sovieti yaliyoitwa perestroika, naye kasisi alitumia muda wake mwingi akizungumzia mabadiliko ya kisiasa katika mahubiri yake. Nilikuwa na hakika kwamba nilihitaji kitu tofauti.

Mnamo 1994, nilipatwa na mshtuko wa moyo mara mbili na nikawa mgonjwa sana. Mwaka huohuo mama yangu alikufa. Lakini licha ya hayo yote, niliendelea kuisoma Biblia. Tayari nilikuwa nimesoma “Agano Jipya” mara 25, kisha nikaacha kuhesabu. Jinsi nilivyoendelea kuisoma ndivyo nilivyopata maswali mengi zaidi. Nilitambua kwamba nisingeweza kuelewa kweli za Biblia peke yangu.

Nuru Yang’aa

Mnamo 1996, Mashahidi wa Yehova walifika nyumbani kwetu huko Yoshkar-Ola. Niliwashuku sana kwa sababu magazeti yalikuwa yamesema kwamba ni dhehebu hatari. Lakini baadaye nikafikiria, ‘Wanaweza kunifanya nini?’ Kwanza niliwauliza maoni yao kuhusu Utatu. Waliniambia kwamba hakuna neno au hata wazo hilo katika Biblia. Nilifurahi sana kwa sababu niliamini hivyo pia.

Niliposoma andiko la Kutoka 6:3 katika Biblia ya Kirusi tafsiri ya Sinodi na kupata jina la Mungu, Yehova, moyo wangu ulienda kasi. Nilishangaa kuona jinsi dini zilivyowadanganya watu kwa kulificha jina hilo. Nilipendezwa kujua kwamba Mashahidi wanaitwa kwa jina la Muumba na wanawaeleza wengine jina hilo.—Isaya 43:10.

Niliwauliza Mashahidi maswali mengi sana. Kwa mfano: “Kwa nini Biblia inazungumzia moto wa mateso? Kwa nini Biblia ya Kirusi tafsiri ya Sinodi inasema dunia itachomwa?” Ingawa nilikuwa na maswali mengi, nilipopata majibu ya Biblia niligundua kwamba nimeipata dini niliyokuwa ninatafuta kwa miaka mingi. Huku nikitokwa na machozi, nilipiga magoti na kumshukuru Mungu.

Muda si muda, Mashahidi walianza kunipeleka kwenye mikutano yao, na nilipendezwa na usikivu wao, na jinsi walivyofungua Biblia msemaji alipotoa sehemu yake. Msemaji alipotaja andiko, watu walilisoma kwenye Biblia zao. Sikuwa nimewahi kusikia kitu kama hicho. Katika mkutano huo Mashahidi waliimba wimbo unaotegemea andiko la Isaya 35:5 unaoanza kwa maneno haya: “Vipofu wanapoona.”

Nilianza kujifunza Biblia na Mashahidi mara nne kwa juma. Muda si muda nilijifunza ni kwa nini Mungu ameruhusu matatizo na vita, na jinsi atakavyoshughulikia matokeo yanayosababishwa na mambo kama hayo. Nilipendezwa hasa nilipojifunza kuhusu ahadi ya upendo ya Mungu kuhusu Ufalme wake ambao utafanya mapenzi yake ya uzima wa milele kwa ajili ya wanadamu watiifu yatimizwe katika dunia paradiso. (Mwanzo 1:28; Isaya 65:17-25; Ufunuo 21:1-5) Kweli za Biblia zikawa wazi zaidi kwangu na hivyo nikabatizwa kuonyesha wakfu wangu kwa Mungu Novemba 16, 1997 (16/11/1997).

Tunamtumikia Mungu Pamoja

Muda mfupi baada ya ubatizo wangu, Liza alianza kujifunza Biblia. Licha ya kuwa na ugonjwa wa kupooza, alifanya maendeleo ya kiroho haraka na kubatizwa mwaka wa 1998. Alihitaji kubebwa hadi kwenye kidimbwi cha ubatizo, lakini alikuwa ameazimia kumtumikia Mungu kwa nafsi yake yote. Tulilipa huduma za kumkanda Liza, naye pia alifanya mazoezi. Baada ya muda alipona. Sasa anahudhuria mikutano yote na kuhubiri nyumba kwa nyumba, hata katika maeneo ya mbali.

Kila wakati ninapoenda mahubiri, mimi husali niwe jasiri. Baada ya kusali, mimi huchukua fimbo yangu, natoka nyumbani, na kwenda kwenye stesheni ya basi ninayoijua vema. Nikisikia mtu anakaribia, ninaanza mazungumzo ya Biblia. Ninapopanda basi, mimi huketi katikati, nazungumza na watu kuhusu Biblia, na kuwaachia vichapo. Yeyote akipendezwa, tunapeana namba za simu.

Muda mfupi uliopita, nilizungumza na mwalimu aliyefundisha muziki katika hospitali moja. Alishangaa kuona hekima inayopatikana kwenye Biblia. Mtu huyo aliporudi kwao, alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Pia katika hospitali hiyo, nilikutana na mkurugenzi wa kiwanda fulani ambaye mwana wake ni kipofu. Nilimweleza kuhusu tumaini langu, naye akapendezwa na kuthamini kweli za Biblia alizosikia.

Tangu nibatizwe, nimewasaidia watu wanane wawe wahubiri wenzangu wa Ufalme na nimejifunza Biblia na wengine wengi. Yehova anaendelea kututegemeza mimi na mke wangu kupitia ndugu na dada zetu Wakristo. Wao hutusomea, nasi huzungumzia vichapo vinavyotegemea Biblia. Pia, wao hurekodi hotuba za kusanyiko na kutaniko kwa ajili yetu. Mambo hayo yametusaidia kukazia kweli moyoni mwetu na kushiriki kweli hizo na wengine. Kwa hiyo kutaniko limekuwa, ‘msaada wenye kututia nguvu.’—Wakolosai 4:11.

Nilitumia muda mwingi wa maisha yangu katika muziki na sasa ninaimba nyimbo za Ufalme kwa shangwe. Nimekariri baadhi ya nyimbo katika kitabu cha Kirusi cha Mwimbieni Yehova Sifa. Ninaamini kwamba Yehova alinipata katika ulimwengu huu mbovu na kunisaidia nipate njia ya kutoka kwenye giza la kiroho. Na hilo linanifanya niamini kwamba siku moja atanikomboa kutoka kwenye giza halisi.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Nikipiga filimbi ya sauti nzito ya “C-major”

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikipiga kodiani mnamo 1960

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Okestra ya filimbi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na Liza leo